Saturday, September 1, 2012

AMRI KUU


  Mathayo 22:37-38 “…Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu tena ni ya kwanza.”
Katika Biblia habari hii inaanza baada ya Yesu Kristo kuulizwa swali la kujaribiwa na mmoja katika Mafarisayo, ambao walikuwa wanaijua torati kamili ya manabii kwa habari ya sheria na amri zake. Walimuuliza swali wakimjaribu ili awaambie ni amri ipi iliyokuu katika torati, na ndipo Bwana Yesu akawapa jibu tofauti na walilolitegemea. Akawaambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote na kwa akili zako zote. Kibinadamu jibu hili ni kama halina mantiki yoyote na limekaa kimzaha zaidi, kwani hakuna mtu asiyempenda Mungu wake.
Lakini ukitazama kiundani zaidi, na kama utapata msaada wa Roho Mtakatifu utagundua kuwa jibu hili linatuhusu na kugusa imani zetu moja kwa moja na siyo wale Mafarisayo tu. Labda tuangalie na kuchambua maana ya vipengere vikubwa vitatu katika mstari wa 37 wa kitabu hicho cha injili.
Kwa moyo wako wote. Neno kwa moyo wako wote linamaanisha kukipa sehemu yote ya moyo wako kitu unachokipenda. Kama umeamua kukipenda kitu fulani, basi ukipende kwa kumaanisha, usikichanganye na kitu kingine. Wala usiwe na mbadala wa hicho unachokipenda.
Kwa roho yako yote, ni kuamua kujitoa hata maisha yako kwa ajili ya hicho unacho kipenda. Kutokuyathamini maisha yako zaidi ya unachokipenda. Sehemu nyingine neno la Mungu linasema atakaye kunifuata na ajikane mwenyewe, sasa kumpenda Mungu kwa roho yote ni kujikana nafsi yako.
Kwa akili zako zote, ni kumfanya Mungu achukue sehemu kubwa ya mawazo yako pasipo kujari sehemu ama wakati uliopo. Kuna watu wakiwa na wapendwa nao ni wapendwa, wakiwa mbali na wapendwa basin a upendwa wao wanauvua.
Kuamua kumpenda Mungu kwa moyo wote, na roho yote, na akili zote, ni kumpenda Mungu pasipo kumchanganya na dhambi, kumpenda Mungu kwa kujikana nafsi zetu na kumpenda Mungu kwa mawazo yetu.
Kuna watu wanawapenda wanandoa wao zaidi ya kumpenda Mungu, wanawapa sifa zinazozidi uzuri wa malaika lakini watu hao hao ukiwakuta kwenye nyumba za ibada wakati wa kipindi cha kumsifu Mungu unawedha ukadhani ni wagonjwa. Na wapo watu wanaowapenda wanadamu kwa roho zao zote kiasi cha kuzirai wakipewa taarifa za vifo vyao lakini kumpenda Mungu hakumo ndani yao. Na wapo watu ambao wanajikana nafsi zao kwa ajili ya watu wengine au mambo mengine. Watu hawa watakwambia hawana muda wa kuhudhuria nyumba za ibada kwa kisingizio cha maisha yanabana au shule ngumu lakini ni mabingwa wa kutenga muda wa kwenda klabu na kumbi mbali mbali za starehe na marafiki lakini muda wa kuongea na Mungu wao hawana.
Kuna aina ya maisha ambayo ni kusudi la shetani moja kwa moja, kama kutoa muda wako mwingi katika vipindi vya televisheni, kusoma vitabu vya hadithi na magazeti, kufanya kazi hadi za “over time”. Lakini linapofika suala la kujitoa kwa Mungu anaye kupa uhai bure, unajibu uko “busy”, hata kusoma biblia yako ni hadi jumapili kanisani, na usomaji wenyewe ni ule wa kufuatisha neno la mhubiri wa siku hiyo.
Hatuna budi kuyatafakari maisha tunayo ishi kuwa ni maisha ya namna ama aina gani, je tunampa Mungu kipaumbele anachostahili katika maisha yetu ya kila siku? Mpenzi msomaji, hebu jiulize swali hilo je mfumo wako wa maisha unampa Mungu kipaumbele anachostahili? Na kama jibu ni ndiyo basi Mungu akuzidishe zaidi, na ikiwa jibu ni siyo basi Mungu akusaidie ili umpe nafsi yake anayostahili katika maisha yako.
Kama tunavyo oona katika mstari ule wa 38 wa injili hii, Yesu aliwajibu wale Mafarisayo kuwa amri hii ndiyo kuu tena ni ya kwanza. Kuvunja amri kuu ni kutenda kosa kuu.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts