Friday, December 6, 2013

MANUNG’UNIKO HUGEUZA BARAKA ZA MUNGU MAISHANI MWAKO NA KUWA LAANA



Manung’uniko ni dalili ya kukata tamaa na kukiri kukosa tumani la jambo au hali ngumu anayoipitia mtu. Japokuwa mtu huyo anaweza asikiri kukata tamaa kwa kinywa chake, lakini kwa kupitia manung’uniko anakiri kukata tamaa na kukosa msaada japo siyo kwa ukiri wa moja kwa moja.
Katika maisha ya kiroho haipaswi kunung’unikia hali ya maisha au majaribu unayopitia, hasa haipaswi kumnung’unikia Mungu. Kwa sababu, kama nilivyokwisha kueleza hapo mwanzo, manung’uniko ni dalili ya kukiri kukata tamaa na kukosa mwelekeo.

Ni afadhari ujilaumu na kujinung’unikia nafsi yako wewe mwenyewe na siyo kumnung’unikia Mungu. Mtumishi wa Mungu, Ayubu alipofikwa na jaribu zito la kupotelewa na watoto, wanyama na kupata ugonjwa mbaya wa ajabu hakuthubutu kumlaumu au kumnung’unikia Mungu kwa kinywa chake au kwa moyo wake. Hebu tuangalie maandiko yafuatayo;

Ayubu 1:20. Ndipo Ayubu akainuka akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake,  na kuanguka na nchi na kusujudia; akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, name nitarudi tena huko uchi vile vile; Bwana alitoa na Bwana ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe. Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.
Ni neno la kuajabisha sana, baada ya Ayubu kupata habari ya kupotelewa watoto wake wote na mali yake yote, alirarua joho lake, akanyoa kichwa chake, akaanguka na kusujudu.  Kwa kurarua joho lake na kunyoa kichwa chake alionesha utii na unyenyekevu mbele za Mungu. 

Ayubu alionesha utii kwa Mungu kwa sababu alijua, watoto wake na mali zake alivipata kwa sababu Mungu alimbariki vitu hivyo. Na ndani ya moyo wake, Ayubu alimsujudia Mungu kwa sababu huyo ndiye aliyebaki naye, na Mungu ndiyo tumaini na msaada wake tu.

Ayubu 3:1. Baada ya hayo Ayubu akafunua kinywa chake, na kuilaani siku yake.
Ilipofikia wakati moya wa Ayubu ulipotaka kunung’unika na kusononeka, Ayubu aliona ni vema ailaani siku yake ya kuzaliwa lakini hakuthubutu kumlaani au kumnung’unikia Mungu wa mbinguni aliyemuumba.

Unapomnung’unikia au kumlaani Mungu kwa mambo magumu unayoyapitia au unayokutana nayo katika maisha yako, unafanya kosa kubwa sana. Ni busara endapo utamuuliza Mungu nini makusudi ya mapito haya, ili kama ni vita dhidi ya shetani, Mungu atakuelekeza jinsi ya kuvipigana na kwa Jina la Yesu Kristo utashinda kwa ushindi mkubwa.
Hebu tuangalie neno la Mungu (kutoka kinywani mwa Bwana) linasemaje kuhusu manung’uniko;
Hesabu 14:26-38. 26. Kisha Bwana akanena na Haruni na Musa na kuwaambia, 27. Je nichukuliane na mkutano mwovu huu uninung’unikiao hata lini? Nimesikia manung’uniko ya wana wa Israeli, waninung’unikiayo. 28. Waambieni, kama niishivyo, asema Bwana, hakika yangu kama ninyi mlivyonena masikioni mwangu, ndivyo nitakavyowafanyia ninyi; 29. Mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili,
30. Hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.
34. kwa hesabu ya hizo siku mlizoipeleleza ile nchi, yaani, siku arobaini, kila siku kuhesabiwa mwaka, mtayachukua maovu yenu, ndiyo miaka arobaini, nanyi mtakujua kufarikana kwangu.

Katika kifungu hicho cha Biblia hapo juu tunajifunza vitu vikuu vipatavyo vine, navyo ni kama vifuatavyo;

Manung’uniko ni uovu mbele za Mungu
“Nichukuane na mkutano mwovu huu uninung’unikiao hata lini?”, maneno hayo ya Mungu yanapatikana katika Hesabu 14:26. Maneno na mawazo yanayoambatana na manung’uniko ndiyo hufanyika uovu mbele za Mungu. Watu wengi wanapo nung’unika hutamka maneno au huwaza mawazo ya kumlaani Mungu, na wakati mwengine kuwalaani na kuwaumiza wengine. Hapo ndipo manung’uniko yanapokuwa ni uovu mbele za Mungu.

Na mara nyingi, manung’uniko yanaambatana na kukata tamaa, na kukata tamaa mar azote huwa ni chanzo cha kutenda dhambi kwa namna moja au nyingine. Kwa maana hiyo; manung’uniko huzaa kukata tamaa na kukata tamaa huzaa dhambi, dhambi ni uovu na chukizo mbele za Mungu.
Kwa mfano; mwanadamu anapo kata tamaa kutokana na ugumu wa maisha, hutafuta njia haramu ya kumuwezesha kuishi kama kufanya ukahaba, wizi na ujambazi, mauaji n.k. hayo yote huja baada ya mtu huyu kunung’unika kuhusu ugumu wa maisha, baada ya kukosa majibu hufikia kukata tamaa inayopelekea kuchukua maamuzi yasiyo sahihi ambayo ni dhambi na chukizo mbele za Mungu kama tulivyoona katika mfano hapo juu.


Manung’uniko husababisha kifo
“mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili”, Hesabu 14:29. Kuna aina mbili za vifo; kifo cha kimwili na kifo cha kiroho.
Maisha ya dhambi yanayotokana na kukata tamaa baada ya manung’uniko ya muda mrefu, hupelekea kifo cha kimwili na kiroho. Kifo cha kiroho ni kurudi nyuma baada ya kupokea wokovu wa Yesu Kristo, unapoishi maisha ya dhambi unakuwa umerudi nyuma kiroho au umeanguka dhambini. Na kifo cha kimwili hufuatia kama matokeo ya maisha ya dhambi unayoyaishi.

 Haimaanishi wasiotenda dhambi hawafi, la hasha, bali maisha ya dhambi humpeleka mtu kaburini pasi na umri timilifu (Ayubu 5:26, Ayubu 42:16-17). Yohana 8:21(b), nanyi mtakufa katika dhambi yenu. Kama tulivyoona hapo juu; manung’uniko huzaa kukata tamaa, kukata tamaa huzaa dhambi na dhambi huzaa kifo, kinachoweza kuwa cha kiroho au cha kimwili.


Kutofikia au kutotimiza malengo yako au makusudi ya Mungu katika maisha yako
“hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo”, Hesabu 14:30.
Hayo yalikuwa ni maneno ya Mungu kwa wana wa Israeli, na kama tulivyoona hapo juu; manung’uniko husababisha kukata tamaa na kukata tamaa husababisha kutenda dhambi na dhambi hupelekea mauti ya kiroho au ya kimwili au vyote kwa pamoja.

Unapokufa kiroho, unauwa makusudi ya Mungu katika maisha yako. Na Mungu asivyo na hasara wewe mmoja unaporudi nyuma, anainua jeshi kubwa la watu kumtumikia. 

Yesu Kristo alipoambiwa awatulize wanafunzi wake waliokuwa wakimsifu, na Mafarisayo; alijibu; “Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele”, hapo Yesu alikuwa akitufundisha kuwa, tunapokata tamaa na kuuwa huduma zetu, Mungu anainua watu wengine ili kuiendeleza kazi yake. Kazi ya Mungu haifi hata siku moja, ukizira wewe, atafanya mwingine, maadam utukufu umrudie Mungu.

Aidha unapokuwa na malengo katika maisha yako, kunung’unika kunakopelekea kukata tamaa inayosababisha dhambi na hatimaye kifo cha kimwili, kunazima malengo yako na kufuta kabisa ndoto zako maishani. Na kusababisha kizazi chako kifuatacho kurithi laana zako, isipokuwa kitatubu na kutakaswa kutoka katika vifungu na maisha ya laana.


Manung’uniko huchelewesha makusudi ya Mungu au mafanikio yako katika maisha
“kwa hesabu ya hizo siku mlizoipeleleza ile nchi, yaani, siku arobaini, kila siku kuhesabiwa mwaka”, Hesabu 14:34
Wana wa Israeli waliipeleleza nchi ya ahadi kwa muda wa siku arobaini, waliporudisha habari ya nchi hiyo ndipo walipomlalamikia na kumnung’unikia Mungu na kusema ingekuwa heri kama wangalikufa katika nchi ya utumwa ya Misri ama wangalikufa jangwani (Hesabu 14:1-3).

Hata wewe mpendwa msomaji wangu, inawezekana uko katika wakati mgumu, unapitia majaribu mazito unayodhani huwezi kuyavuka. Unafikia hatua unakata tamaa, unamlaumu Mungu kwa nini alikuumba, ni heri ufe sasa. 

Ninakwambia sasa, acha kumlaumu Mungu, acha sasa kumlaani Mungu, acha kukata tamaa, usithubutu kurudi nyuma, kwa Jina la Yesu Kristo, yupo Mungu ili akusaidie na utasema hakika wewe Mungu umekuwa ni Ebeneza kwangu.

Ikiwa Mungu anayo makusudi na maisha yako, mafanikio yako au baraka zako ni lazima akupitishe katika kipimo cha uvumilivu na uaminifu, unapofuzu mtihani huo ndipo Mungu anapoachilia kibari katika maisha yako, huduma yako na baraka zako.

Nataka nikupe angalizo katika somo hili; siyo kila mtihani au magumu unayopitia ni makusudi ya Mungu. Muulize Mungu nini chanzo, sababu na makusudi ya hali unayopitia.

Ikiwa ni uonevu wa ibilisi, mwambie Mungu akupiganie na akupe kuyashinda yote katika Jina la Yesu Krsito.

Ikiwa ni makusudi ya Mungu upitie hatua uliyopo sasa, imekupasa kuvumilia yote, usilalamike, usinung’unike, usikate tamaa wala usimlaani Mungu. Simama imara kuitetea imani yako.
Tukichukua mfano wa wana wa Israeli, Mungu aliwapitisha jangwani katika hali ngumu kwa makusudi maalumu;

Kutoka 7:16. “Nawe umwambie, Bwana, Mungu wa Waebrania, amenituma nije kwako, kusema, wape watu wangu ruhusa, ili wapate kunitumikia jangwani”,
Mungu hakuwapitisha wana wa Israeli jangwani kwa bahati mbaya, aliwapitisha kwa makusudi maalumu. Kumbuka Mungu aliahidi kuwapa nchi yenye maziwa na asali (nchi ya ahadi), ili kuifikia ile nchi, iliwapasa kupitia mtihani mzito jangwani.

Kule kuenenda kwao jangwani; kwa kumsifu Mungu aliyewatoa utumwani na sasa anakwenda kuwapa nchi ya ahadi au kwa kumlalamikia na kumnung’unukia Mungu, ndiko kuliamua ni nani ataingia na nani hataingia katika nchi ya ahadi.

Na hii ni kwako pia mpendwa mwenzangu, vile unavyomuona Mungu katika mtihani unaoupitia ndio kunaamua ni jinsi gani utafikia ahadi ya ukombozi ya Mungu iliyopo mbele yako. Ikiwa unamlalamikia, unamlaani Mungu au unakata tamaa, ni dhairi utashindwa kufikia baraka na mafanikio yako ambayo Mungu ameyaweka mbele zako baada ya kuimaliza safari ya mtihani unaoupitia, ama utaifikia kwa wakati wa kuchelewa hadi hapo Mungu atakapojiridhisha kuwa umekomaa.

Hebu tuangalie neno la Mungu kuhusu mitihani tunayoipitia; “Amri hii ninayokuamuru leo mtaishika kuitenda, mpate kuishi na kuongezeka, na kuingia katika ile nchi amabayo Bwana aliwaapia baba zenu; nanyi mtaimiliki. Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako, aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu, kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo”, Kumbukumbu la Torati 8:1-2.

Nikupe mfano mfupi; matajiri wengi wanaotumia fedha na mali zao kuwatunza yatima na maskini, historia ya maisha yao ni watu waliotokea katika hali ngumu sana za kiuchumi. Mungu anapo wabariki na kuwapa mali, anawakumbusha kule walikotokea kisha anaweka mzigo wa watu hao kumtumikia Mungu kwa kutumia fedha na mali zao katika kuwatunza yatima na maskini.

Ili Mungu akubariki baraka za kiroho ni lazima akupitishe katika mtihani wa kukataliwa, watumishi wakubwa unaowaona leo kuna kipindi kigumu walichokipitia hata kufikia hapo unapowaona wamefika na unapotamani na wewe ufikie. Wapo wachungaji walioanza kanisa na watu wa familia zao tu kwa miaka kadhaa kabla hawajafikia kuwa na wafuasi zaidi ya miatano.

Na wapo wahubiri wakubwa ambao wakihubiri maelfu ya watu wanaokoka, walianza kwa mikutano ambayo walihubiri na hakuna mtu hata mmoja aliyeokoka.

Nataka nikwambie, hawakukata tamaa, hawakumlaumu wala kumnung’unikia Mungu, bali waliendelea kumtukuza, kumuhimidi na kumtumaini Mungu katika huduma zao.

Vivyo hivyo, ili Mungu akubariki baraka za kimwili kama fedha na mali, ni lazima akupitishe katika mtihani wa dhiki ya kukosa fedha na mali. Ili akupie moyo wako una mtazamo gani kumuelekea Mungu. Ikiwa unakata tamaa, unamnung’unikia Mungu, ujue hutafikia baraka ambazo Mungu ameziweka mbele yako, na ikiwa kwa neema ya Mungu utazifikia baraka hizo, basi utachelewa sana.

Katika kumalizia, ninataka nikutie nguvu mpendwa, usikate tamaa, usimlaumu wala usimnung’unikie Mungu. Simama imara katika mtihani unaoupitia, yupo Mungu jina lake anaitwa Yehova, atakusaidia na kukutetea ikiwa tu utamtumainia na kumtegemea yeye. Hakika upo ushindi na baraka baada tu ya kuumaliza mtihani wako, usithubutu kurudi nyuma kiimani na kumuacha Mungu na wala usithubutu kukata tamaa ya maisha, shindig upo, katika Jina la Yesu Kristo. Amina.

Kudownload somo hili katika PDF, bonyeza HAPA

Saturday, October 12, 2013

KWANINI YESU KRISTO ALIPOTAKA KWENDA FARAGHA, KATIKA MAOMBI, AU ALIPOAMUA KUFANYA JAMBO LA KIPEKEE ALICHAGUA KUAMBATANA NA PETRO, YOHANA NA YAKOBO?



 Ukiyachunguza maandiko katika vitabu vya Biblia vya Injili zile nne; Injili ya Mathayo, Marko, Luka na Yohana utakutana na vifungu vingi vikionesha jinsi Bwana wetu Yesu Kristo alivyopenda kuambatana na Petro, Yohana na Yakobo.

Na alipenda kuambata na wanafunzi wake hao watatu; Petro, Yohana na Yakobo sehemu muhimu au katika shughuli muhimu. Kwa mfano, alipotaka kwenda faragha kwa maombi au alipoamua kufanya jambo la uponyaji lililohitaji imani kubwa.

Kuna sababu nyingi sana zilizomfanya Bwana wetu Yesu Kristo apende kuambatana na wanafunzi wake hao watatu katika faragha na sehemu muhimu mbali mbali.

Petro, Yohana na Yakobo richa ya kwamba walikuwa ndugu (Yakobo na Yohana - Mathayo 4:21) na marafiki (Marko 13:3, Matendo ya Mitume 3:1) walikuwa wana sifa za pamoja zinazofana na sifa za kila mmoja wao, ambazo kwa umoja wao walitengeneza timu iliyompendeza Yesu Kristo.

Hebu tuangalie baadhi ya vifungu vinavyo thibitisha kuwa Bwana wetu Yesu Kristo alipenda kuongozana zaidi na Petro, Yohana na Yakobo kwa maombi ya faragha au katika jambo la kipekee na umuhimu zaidi.

Mathayo 17:1. Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu yam lima mrefu faraghani (kwa maombi).

Marko 1:29. Na mara walipotoka katika sinagogi, walifika nyumbani kwa Simoni na Andrea, pamoja na Yakobo na Yohana. Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia (Yesu Kristo) habari zake.  (Yesu Kristo) Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia.

Marko 5:37. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo.

Luka 22:8. Akawatuma Petro na Yohana, akisema, Nendeni, mkatuandalie pasaka tupate kuila.

Marko 14:32-33. Kisha wakaja mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa muda niombapo. Akamtwaa Petro na Yakobo na Yohana pamoja naye, akaanza kufadhaika sana na kuhangaika.

Wednesday, August 21, 2013

HATUA NNE ZA KUPATA AMANI YA MOYO NA NAFSI (INNER PEACE).




Msongo wa mawazo na ukosefu wa amani moyoni na/au nafsini imekuwa ni tatizo linaloongezeka kwa kasi na kuwapata watu wengi sana. Na ubaya ama ugumu wa tatizo hili ni kwamba linagundulika baada ya matokeo ya ukosefu wa amani moyoni au nafsini na msongo wa mawazo.

Yaani ni hivi; watu wengi wasio na amani moyoni na nafsini huishi maisha ya kuigiza  na huwa vigumu sana kuwatambua watu hao, unaweza kumtambua mtu mwenye msongo wa mawazo kwa tabia yake ya kujitenga na kutoshirikiana na watu. Lakini unaweza usimtambue mtu asiye na amani moyoni au nafsini kwa sababu wengi wa watu hawa huvaa sura zenye tabasamu na furaha wawapo mbele za watu.

Ni watu wanaoyabeba maumivu yao wao wenyewe na kujaribu kutafuta suluhisho pasipo kuwashirikisha watu wengine. Na ndipo utakaposhangaa kuona mtu fulani amefanya jambo usilolitegemea alifanye, kwa mfano; kuua au kujiua wao wenyewe, kutukana matusi, au kufanya jambo la hatari ilihali anajua madhara yake pasipo kujihadhari.

Ndiyo, matokeo ya ukosefu wa amani moyoni au nafsini pamoja na msongo wa mawazo matokeo yake siku zote huwa ni hasara au maumivu kwa muhusika au watu wanao mzunguka. Wengi hutafuta njia za kutua mizigo iliyomo mioyoni na nafsini mwao kwa njia za mkato ambazo wengi hudhani kujiua au kuwaua wale wailowasababishia maumivu hayo ndiyo jibu sahihi.

Kuna nyakati ukosefu wa amani ya nafsi au moyo kunaambatana na chuki na visasi, yaani muhusika hubebea chuki na/au visasi dhidi ya mtu au watu waliomsababishia maumivu hayo. Kubeba chuki na visasi vya muda mrefu ndani ya mioyo na nafsi zilizokosa amani hupelekea matatizo ya kiafya kama shinikizo la damu (hypertension), mshituko (stroke), kupooza (paralysis) na hata kuzeeka mapema (early aging). Hii hutokea kwa watu ambao wana msongo wa mawazo, wamekosa amani moyoni na nafsini na huku wamebeba mizigo ya chuki na visasi dhidi ya watu wasioweza kuwalipia hicho kisasi.

Sisemi inatupasa kubeba chuki na visasi mioyoni na nafsini mwetu, hiki ni kitu kinachotupata nje ya uwezo wetu (involuntary action). Na kama jinsi tumekosa amani mioyoni na nafsini mwetu pasipo kupenda sisi wenyewe, ndivyo ilivyo ni vigumu kuitafuta amani ya nafsi na mioyo yetu sisi wenyewe pasipo msaada wowote.

Ni lazima utafute msaada, na msaada pekee na wa kuaminika ni Mungu (Yehova) peke yake. Ndiyo, kuna wanasaikolojia waliobobea ambao wanaweza wakakusaidia, lakini msaada wa Mungu kupitia Yesu Kristo ndiyo una uhakika wa asilimia mia moja (100%).

Sunday, July 21, 2013

UNAWEZA KUWA UNATEMBEA CHINI YA LAANA PASIPO WEWE MWENYEWE KUJUA.



YESU KRISTO ASIFIWE!

Ashukuriwe Mungu aliyetupa kibali cha mimi na wewe msomaji wangu kukutana leo ikiwa ni kwa mara ya kwanza au kwa mara nyingine tena. Leo tuna somo lenye kichwa kisemacho “UNAWEZA KUWA UNATEMBEA CHINI YA LAANA PASIPO WEWE MWENYEWE KUJUA”, katika somo hili tutaangalia kwa undani mambo yafuatayo:-


  • Maana ya laana.

  • Laana inaletwa/sababishwa na nani?

  • Kwa nini ulaaniwe?

  • Je, unaweza kuwa umelaaniwa pasipo wewe kujua?

  • Ni vitu gani vinaweza kulaaniwa?

  • Kuvunja laana na mikosi, kuomba baraka za Mungu (Yehova).

Hili ni somo zuri sana ambalo ukilifuatilia kwa ukaribu zaidi na ukijenga imani kwa Mungu kuna vitu (laana), Mungu anakwenda kuzivunja, kuzifuta na kuziharibu (1 Yohana 3:8) na kuyabadilisha maisha yako kabisa. Unakwenda kuishi maisha ya baraka na ushindi, nakuhakikishia lazima utazishuhudia baraka za Mungu katika maisha yako baada ya kumaliza somo hili.

Maana ya laana.
Laana ni bahati mbaya au maneno mabaya ya maapizo yanayotamkwa kumuelekea mtu fulani yeye mwenyewe au kitu fulani kinachomuhusu, kwa mfano; kazi, shamba, watoto, masomo n.k kwa makusudi ya kumdhuru mtu huyo au kitu kinachomuhusu. Kwa kifupi laana ni kinyume cha baraka.

Laana inaweza ikasababishwa kwa makusudi maalumu (mfano: laana ambayo ni matokeo ya dhambi za wanadamu) au pasipo kujua (mfano: laana ya kujitamkia sisi wenyewe), kwa njia zote hizi mbili laana inafanya kazi iwe kwa makusudi au pasipo kujua.

Laana, ili itende kazi ni lazima iwe imeunganishwa na nguvu fulani zisizo za kawaida, nguvu za ziada “supernatural powers”,  nguvu hizo ni lazima ziwe zinazidi nguvu za mtu au kitu kinacholaaniwa. Nachomaanisha hapa ni kwamba, mdogo hawezi kumlaani mkubwa; shetani hawezi kumlaani Mungu, na mtu aliyesimama katika kweli na haki ya Mungu hawezi kulaaniwa na shetani kutokana na ile nguvu ya Mungu iliyomo ndani yake.

Kwa maana hiyo, kwa maneno yetu wenyewe au ya watu wa karibu nasi na matendo ya maisha yetu ndiyo sababu kubwa ya laana katika maisha yetu na vizazi vyetu vijavyo. Kwa sababu kila tunachokitamka na tunachokitenda kinafuatiliwa kutimilizwa na falme mbili tofauti; ufalme wa Mungu na ufalme wa shetani. Ni hakika na kweli, ufalme wa shetani hufuatilia hasa mambo ambayo ni hasi kuyatimiliza katika maisha yetu, kuwa mwangalifu sana.

Monday, July 15, 2013

HII SI YA KUKOSA!!!

Nakusalimu kwa Jina la Yesu Kristo!

Natumaini u mzima wa afya, kama mimi nilivyo mzima pia, shukrani zimrudie Mungu mwenyewe anayetupa uhai bure.

Kuanzia jumapili ya tarehe 21/07/2013, tutaanza somo jingine lenye kichwa kisemacho;

"UNAWEZA KUWA UNAISHI NA LAANA PASIPO WEWE MWENYEWE KUJUA"

ni somo zuri sana, lenye pumzi ya Mungu. na kupitia somo hilo, Mungu anakwenda kukutoa mahali ulipo ambapo haustahili kuwepo na anakuinua na kukuketisha meza moja na wafalme, kwa kifupi utakwenda kuziona baraka za Mungu zakianza kufuatana na wewe kwani laana na mikosi yote inakwenda kuvunjwa na wewe kuwekwa huru, katika jina la Yesu Kristo, Amina.

Katika somo hilo tutakwenda kuangalia kwa undani zaidi mambo yafuatayo:-

  1. maana ya laana
  2. laana inaletwa/sababishwa na nani?
  3. kwanini ulaaniwe?
  4. vitu gani vinaweza kulaaniwa katika maisha yako?
  5. je unaweza kuwa umelaaniwa pasipo wewe mwenyewe kujua?
  6. kuvunja laana na mikosi kwa Jina la Yesu Kristo.
Hivyo basi usithubutu kulikosa somo hili, mtaarifu na mwenzako ili Mungu akubariki sana kwa kushiriki katika kuutangaza ufalme wake.

Saturday, July 6, 2013

MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU.



YESU KRISTO ASIFIWE!

Karibu tena ndigu msomaji wangu; sifa, heshima na shukrani ni kwake Mungu Baba wa mbinguni aliyetupa kibali tuweze kukutana tena katika sehemu ya mwisho ya somo letu lenye kichwa kisemacho “MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU”.

Ikiwa leo ndiyo mwisho wa somo hili, nina imani Mungu atakuwa amekuhudumia kwa namna ya pekee na utakwenda kupokea kitu kipya katika maisha yako ambacho kitafanyika baraka ya pekee katika maisha yako. Endelea!



Kuomba kwa kuzitaja ahadi za Mungu.

Isaya 55:10-11. “maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu (Bwana Mungu), litokalo katika kinywa change; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma”.

Hayo ni maneno ya Mungu mwenyewe, anasema neno (ahadi) lake ni kama mvua ishukavyo toka mbinguni kuinyeshea ardhi isivyorudi mbinguni, ndivyo neno (ahadi) lake lisivyokuja tupu pasipo kutimiza mapenzi yake yaliyopo ndani ya neno (ahadi) lake. 

Unaweza ukajiuliza kama neno la Mungu lazima litimize mapenzi yake, kwa nini basi tunapaswa kuomba? Ahadi ya Mungu ipo inatuzunguka wote, kama neno lake linavyosema yeye huwanyeshea mvua wote wenye haki na wasio haki (Mathayo 5:45). Lakini ili ahadi ya Mungu itimie katika maisha yako ni lazima uombe. Tuangalie kidogo neno:-

Isaya 43:26. “Unikumbushe (ahadi yangu); na tuhojiane (uiombe); eleza mambo yako, upate kupewa haki yako (kutimiziwa ahadi ya neno langu)”. 

Hapo juu pia ni maneno ya Mungu mwenyewe, kwa nini niende mbele za Mungu kuomba anitimizie ahadi ya neno lake? Kwa nini nimkumbushe, ina maana amesahau? La hasha, Mungu hajawahi kusahau na hatakuja kusahau, tunapokwenda mbele za Mungu, tunakili na kuthibitisha imani yetu kwake. Hicho ndicho kitu, Mungu anapenda kutoka kwetu. Ndiyo maana Yesu Kristo alipokuwa akiwaponya wagonjwa alikuwa akiitazama imani iliyomo ndani ya mioyo yao.

Mungu hajawahi kudanganya na hatakuja kudanganya, lakini lazima tuombe ili tuikili na kuithibitisha imani yetu kwake. Tofauti ya imani kati kati yetu, hufanya tofauti ya kupokea kwetu kutoka kwa Mungu. Unaweza ukawa hujanielewa, ni hivi; mwenye imani haba hupokea haba na mwenye imani nyingi hupokea vingi. Kwa sababu Mungu huwatendea wanadamu wote kulingana na imani ndani ya mioyo yao.

Hebu tuangalie mistari michache ya maombi yanayounganisha ahadi za Mungu;

Maombi ya Mfalme Daudi; 2 Samweli 7:27-29. “Kwa kuwa wewe, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi, mtumwa wako, ukisema, Nitakujengea nyumba (ahadi); kwa hiyo mimi, mtumwa wako, nimeona vema moyoni mwangu nikuombe dua hii. Na sasa, Ee Bwana Mungu, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ndiyo kweli (ahadi yako ni hakika), nawe umemwahidia mtumwa wako jambo hili jema; basi, sasa, uwe radhi, ukaibarikie nyumba ya mtumwa wako, ipate kudumu milele mbele zako; kwa maana wewe, Ee Bwana Mungu, umelinena (umeahidi); na kwa baraka yako nyumba ya mtumwa wako na ibarikiwe milele”.

Zaburi 119:170. “Dua yangu na ifike mbele zako, uniponye sawasawa na ahadi (ya uponyaji; Kutoka 23:25) yako”.


Kwa nini uombe kwa kuzitaja ahadi za Mungu.


  • Ahadi za Mungu zimehakikishwa (ahadi timilifu).
2 Samweli 22:31(b). Mungu, njia yake ni kamilifu; ahadi ya Bwana imehakikishwa; Yeye ndiye ngao yao wote wanaomkimbilia.


  • Mungu hasemi uongo.
Hesabu 23:19(a). Mungu si mtu, aseme uongo.


  • Mungu ni mwaminifu, hutekeleza alichoahidi.
Kumbukumbu 7:9. Basi jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu.


  • Tukiomba sawasawa na mapenzi (ahadi) yake, atusikia.
1 Yohana 5:14. Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake (sawa sawa na neno au ahadi yake), atusikia.


  • Ni lazima atimize ahadi yake kwanza, kwa sababu ameikuza kuliko jina lake.
Zaburi 138:2. Nitakusujudu nikilikabili hekalu lako takatifu, nitalishukuru Jina lako kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako, kwa maana umeikuza ahadi yako kuliko jina lako lote.


Ni maombi yangu, Bwana Mungu; afungue vilivyofungwa, arejeshe vilivyonyang’anywa, ainue huduma zilizolala, afufue huduma zilizo kufa, abariki palipo laaniwa, na akuinue mtumishi wake kutoka utukufu uliopo akupandishe juu zaidi, kwa jina la Yesu Kristo. Amina! 

Nina imani umebarikiwa sana, na umepokea kitu cha tofauti katika kukuinua kutoka hatua moja kwenda hatua nyingine mbele, utukufu ni kwa Mungu (Yehova) mwenyewe.

Ili kuweza ku-download PDF ya somo hili lote tangu mwanzo hadi mwisho, bonyeza HAPA.



Saturday, June 29, 2013

MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU (SEHEMU YA PILI).



YESU KRISTO ASIFIWE!

Mpendwa msomaji wangu karibu tena katika mwendelezo wa somo letu lenye kichwa kisemacho “MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU”, ikiwa leo ni sehemu ya pili. Nina imani utazidi kubarikiwa zaidi na somo hili, ikiwa ulikosa sehemu ya kwanza ya somo hili utaipata humu humu ndani ya blog hii.

Leo tunaangalia aina kuu za maombi na faida zake, na aina nyinginezo za maombi na faida zake. Ni matumaini yangu kwa msaada wa Roho Mtakatifu utajifunza vyema na Mungu atakuwa pamoja nawe.


Aina kuu za maombi na faida zake.

Maombi kabla. 
Haya ni maombi ambayo muhusika anaomba kabla hajafikwa na jambo, kwa mfano unapoamua kuombea maisha yako ya badae, familia (mke au mume na watoto) yako ya badae ilihali haujaoa au kuolewa. Unapofika wakati huo, unashangaa mambo yanaenda vizuri, ni kwa sababu ulishaomba kabla.

Mathayo 26:41a. “Kesheni mwombe, msije mkaingia majaribuni”

Yesu mwenye anasema kesheni mwombe siyo muwapo majaribuni, bali msije mkaingia majaribuni. Anamaanisha tuombe sasa, ili majaribu yajapo tusije tukaingia kwayo, kwa hiyo anatuambia tuombe sasa kwa ajili ya maisha yetu ya badae.

Waebrania 4:16. “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji”. 

Inawezekana kabisa kupata rehema na neema ya maisha na wakati wetu ujao sasa, ili tunapoyafikia maisha yetu ya baadae au kupata mahitaji katika wakati ujao tayari tunakuwa tumefunikwa na rehema na neema za Mungu na hivyo kutufanya tusimame imara. 

Faida ya maombi haya ni maombi yenye mafanikio sana, kwa sababu muombaji huomba kwa ile imani aliyonayo mbele za Mungu kupitia jina la Yesu Kristo. Hapa muombaji haombi kutokana na nguvu inayomsukuma kutoka nje, bali huomba kwa sababu anamwamini Mungu na kumfanya Mungu kuwa ndiye tumaini lake.


Maombi baada.
 
Haya ni maombi ambayo mwombaji huomba baada ya kuingia katika jambo analoliombea. Yaani mwombaji anakuwa ameingia katika shida, ndipo anamkumbuka Mungu tena baada ya njia nyingine zote kushindwa. Ina maana, anakuwa na imani na vitu vingine tofauti na Mungu, vile vitu vinaposhindwa ndipo anamtafuta Mungu.

Zaburi 69:1-2. “Ee Mungu uniokoke, maana maji yamefika mpaka nafsini mwangu. Ninazama katika matope mengi, pasipowezekana kusimama. Nimefika penye maji ya vilindi; mkondo wa maji unanigharikisha”.

Maombi haya siyo mazuri sana kama maombi kabla, kwa sababu muombaji huomba kutokana na msukumo anaoupata kutoka na shida, tatizo au hitaji alilonalo.


Maombi ya kawaida.

Ninaposema maombi ya kawaida ninamaanisha maombi yasiyoambatana na kufunga (not fasting prayers). Maombi haya yana majibu pia, hasa ukiyaambatanisha na imani na utakatifu na ukifuata vitu vya kuzingatia uwapo katika maombi au kabla ya maombi.
 

Maombi ya kufunga (fasting prayers).

Haya ni maombi ambayo muombaji huamua kuingia katika maombi pasipo kula au kunywa kwa kipindi cha muda maalumu. Kwa mfano inawezekana kufunga kwa muda wa masaa 12, 24, 48 au 72, n.k ikitegemea ukubwa na umuhimu wa kile unachokiombea.

Kufunga kunakufanya uoneshe ni jinsi gani una nia ya dhati kuelekea kile unachokiombea, na kunamfanya Mungu akutegee sikio la umakini zaidi na hivyo kuitimiza haja yako kwa wakati.

1 Wafalme 21:27-29. “Ikawa, Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa magunia mwilini mwake, akafunga, akajilaza juu ya magunia, akaenda kwa upole (mbele za Mungu). Neno la Bwana likaja kwa Eliya Mtishbi, kusema, Huoni jinsi Ahabu alivyojidhili mbele yangu? basi kwa sababu amejidhili mbele yangu, sitayaleta yale mabaya katika siku zake”.

Kwa njia ya maombi ya kufunga na ya unyenyekevu mbele za Mungu, Mungu akaiondoa hasira yake mbele za mfalme Ahabu.


 Aina nyingine za maombi.
 
Aina hizi za maombi zinaweza zikawa ndani ya aina mojawapo au mbili ya aina za maombi nilizoziongelea hapo juu katika aina kuu za maombi. Inaweza ikawa ni maombi kabla, au maombi kabla na ya kufunga ukiombea maisha yako ya baadae au watoto wako Mungu atakaokupa. 
Kwa mfano unaweza ukawa unafanya maombi ya kufunga na kufungua vifungo ambayo pia yakawa ni maombi kabla (unaombea maisha ya badae) halafu na ukawa umefunga, kwa hiyo hapo unakuwa umefanya maombi ambayo yamo ndani ya maombi makuu mawili; maombi kabla na maombi ya kufunga.

Aina hizo nyingine za maombi ni kama zifuatazo:-

Maombi ya Roho Mtakatifu.

Waefeso 6:18. “kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha katika jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote”.

Haya ni maombi ambayo muombaji anaomba akiwa amezama rohoni, na Roho Mtakatifu ndiye anayehusika kuomba kwa ajili ya muombaji. Kwa nini basi tuombe katika Roho, tuangalie kifungu cha Biblia hapa chini;

Warumi 8:26-27. “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo, aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu”.

Kuna sababu kubwa mbili za kutulazimu kuomba kwa Roho; hatujui kuomba ipasavyo na Roho hutuombea kama apendavyo Mungu. Kwa hiyo unaweza ukawa unafanya maombi ya Roho ukiombea maisha yako ya badae au familia yako au upate kazi.


Maombi ya kufunga na kufungua.

Hapa ninaposema maombi ya kufunga na kufungua simaanishi maombi ya kutokula wala kunywa, ni maombi ambayo mwombaji anatumia mamlaka aliyopewa na Yesu Kristo kuvifungia au kuvifungua vitu fulani katika maisha yake.

Mathayo 18:18. “Amini, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni, na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni”.

Kwa hiyo unaweza ukafunga kabisa magonjwa katika maisha yako na hutaweza kuugua, ama unaweza ukafungua mifereji ya baraka za rohoni na mwilini kwa watoto wako hakika watabarikiwa. Kanuni ni moja tu; imani, kwa sababu Yesu mwenyewe amesema, “amini, nawaambieni”. 

Unganisha utakatifu na vitu vingine vya kuzingatia katika maombi, ukiwa umebeba imani hakika utamuona Mungu katika viwango vya juu zaidi. Kwa hiyo unaweza ukawa unafanya maombi haya ukiyaambatanisha na maombi kabla na maombi ya kufunga.


Maombi ya kusukuma.

Haya ni maombi ambayo muombaji hung’ang’ana na kuomba hadi apokee majibu ya maombi yake, na mara nyingi waombaji wa maombi haya huwa kuna jibu wanalokuwa wanalitegemea kutoka kwa Mungu, hivyo hung’ang’ania kuomba hadi watakapolipata jibu hilo.

Luka 11:5-9. “Akawaambia, ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, rafiki yangu nikopeshe mikate mitatu kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, name sina kitu cha kuweka mbele yake; na yule wa ndani amjibu akisema, usinitaabishe, mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe? Nawaambia ya kwamba ijapokuwa aondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake. Nami nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa”.

Kabla hujaingia katika maombi haya ni vema ukamuuliza Mungu nini makusudi yake, kwani unaweza ukang’ang’ana kuomba majibu yasiyo yako, Mungu anaweza akawa amekukadilia mahali pa juu sana lakini kwa kutojua ukaomba maombi haya ukiwa umejikadilia mahali pa chini mno. Siyo kwamba Mungu hatakupa haki yako, utaopata lakini lazima uanzie kule ulikoomba ndipo upande juu.

Aina hii ya maombi, nayo unaweza ukaiambatanisha na mojawapo au zaidi ya aina zile kuu nne za maombi kutegemea na uhitaji wako.


Maombi kwa adui.

Hii ni aina ya maombi ambayo ni ngumu sana, na Wakristo wengi huwa hawaombi maombi ya aina hii. Haya ni maombi ambapo mwombaji huwaombea watesi na adui zake, huwaombea baraka, ushindi, mafanikio na ikiwezekana hata kuomboleza kwa ajili yao ili Mungu awape rehema.

Mathayo 5:43-44 na 48. “Mmesikia kwamba imenenwa, umpende jirani yako na umchukie adui yako, lakini mimi (Yesu Kristo) nawaambia, wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”.

Kuwaombea adui zetu, ni agizo la moja kwa moja kutoka kwa Yesu Kristo mwenyewe. Lakini ni Wakristo wangapi leo wanaowaombea adui zao? Na siyo tuwaombee laana, maisha mafupi, kukosa kibali, la hasha, tumeagizwa kuwaombea Baraka. Hebu tuangalie kifungu cha Biblia kifuatacho:-

Warumi 12:14. “Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani”.   

Hapa neno la Mungu halituagizi kubagua kwamba ni nani aliyetuudhi na awe amutuudhi nini, yeyote na chochote alichotuudhi, tumeagizwa kumbariki.


Maombi ya ushirika.

Haya ni maombi ambayo wanajumuiya, au Wakristo wa kanisa fulani wanashirikiana kwa umoja katika kuliombea jambo fulani; aidha linahusu kanisa au linamuhusu mshirika mmoja.

Matendo ya Mitume 1:12-14. “kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato. Hata walipoingia wakapanda orofani, walipokuwa wakikaa; Petro, na Yohana, na Yakobo, na Andrea, Filipo na Tomaso, Bartholomayo na Mathayo, Yakobo wa Alfayo, na Simoni Zelote, na Yuda wa Yakobo. Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake, na Mariamu mama yake Yesu, na ndugu zake”.

Faida ya maombi haya ni kwamba, yanaonesha umoja na ushirikianao wa kanisa au jumuiya na pia yana nguvu zaidi kuliko maombi ya mtu mmoja. Siyo lazima ufanye maombi ya ushirika na kanisa zima japo ni vizuri zaidi, lakini unaweza ukafanya na baadhi ya jamaa wachache.

Mathayo 18:19. “Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu (ushirika) watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu (Yesu) aliye mbinguni”.


Maombi kwa wengine.

Haya ni maombi ambayo muombaji hutenga siku maalumu au huamua kufanya maombi maalumu kwa ajili ya kuombea wengine, yeye hajihusishi kabisa katika maombi haya. Anakwenda mbele za Mungu akibubujika na kulia kwa sababu yaw engine.

Unaweza ukaliombea kanisa lote, Mungu alisimamishe imara na kulipa kibali, alizidishie upendo, tena ikiwezekana kwa kuwataja majina washirika wa kanisa hilo. Na siyo lazima liwe kanisa unaloabudia, unaweza hata kuliombea kanisa la jirani. Au hata kuiombea familia ya jirani yako, Mungu ailinde, aibariki na mambo mengine mazuru mengi.

Wakolosai 1:9. “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni”.

2 Timotheo 1:3. “Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavya wewe daima, katika kuomba kwangu, usiku na mchana”.

Kuombea wengine (tofauti na maombi ya kuombea adui), ni agizo kwa kanisa pia; kwa sababu tusipowaombea wengine, tunaonesha ubinafsi, na kama tutakuwa wabinafsi basi kumpenda Mungu hakupo ndani yetu. Na kama hatumpendi Mungu, tunafanya dhambi.

1 Samweli 12:23. “Walakini mimi, hasha! Nisimtende Bwana dhambi kwa kuacha kuwaombea ninyi; lakini nitawaelimisha katika njia iliyo njema, na kunyoka”.



Maombi ya sifa.

Haya ni maombi ambapo mwombaji anayatafakari matendo makuu ya Mungu aliyomtendea katika maisha yake, sehemu ngumu alizokuvusha amabzo kwa akili zako ilishindikana, wema wote ambao Mungu amekufanyia, kukuweka kuwa hai na wakati wapo uliozaliwa nao tarehe moja, mwezi mmoja au mwaka mmoja hawapo.

Ndipo muombaji hububujika na sifa mbele za Mungu wake, moyo wake humshangilia Bwana mchana na usiku.

Zaburi 34:1 na 3. “Nitamhimidi Bwana kila wakati, sifa zake zi kinywani mwangu daima. Mtukuzeni Bwana pamoja name, na tuliadhimishe jina lake pamoja”.

Sehemu nyingine katika Biblia, maombi haya ya sifa yamefananishwa na sadaka mbele za Mungu.

Hosea 14:2. “Chukueni maneno pamoja nanyi, mkamrudie Bwana; mkamwambie, ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema; na hivyo ndivyo tutakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe”. 


Maombi ya shukurani.

Maombi haya kidogo yafanane na maombi ya sifa, lakini tofauti yake ni kwamba maombi ya sifa unamtolea Mungu sifa za midomo yako kulingana na matendo yake wakati maombi ya shukrani ni kwamba unampa Mungu shukrani kwa mema yote aliyotenda kwako na hata kwa wanaokuzunguka.

Waefeso 5:20. “na kumshukuru Mungu Baba siku zote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo”.

Wakolosai 3:17. “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye (Yesu Kristo)”.

 Kwa imani niliyonayo na imani uliyonayo, Mungu akutendee sawa sawa na maombi yangu hapa chini,



"Ni maombi yangu, Bwana Mungu; afungue vilivyofungwa, arejeshe vilivyonyang’anywa, ainue huduma zilizolala, afufue huduma zilizo kufa, abariki palipo laaniwa, na akuinue mtumishi wake kutoka utukufu uliopo akupandishe juu zaidi, kwa jina la Yesu Kristo. Amina!".

Unapobarikiwa, fanyika baraka na kwa wengine. Tafadhari  shiriki somo hili katika ukurasa wako wa "twitter" na "facebook".

Usikose kamilisho la somo hili siku ya jumapili tarehe 7/7/2013, kuna kitu cha tofauti sana Mungu atakwenda kukutendea na kujibu maombi yako. Amina.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts