Wednesday, December 24, 2014

HERI YA KRISMASI NA FURAHA YA MWAKA MPYA WENYE MAFANIKIO, 2015

 Uongozi wa blogu ya "SILAGO2.BLOG", wachungaji walezi na wapendwa katika pendo liokoalo la Yesu Kristo, tunawatakia wasomaji wetu wote mahali popote mlipo "HERI YA KRISMASI NA FURAHA YA MWAKA MPYA WENYE MAFANIKIO, 2015".

Kwanza kabisa tunazo shukurani za dhati kwa Mungu aliye hai, aishiye milele, Yehova kupitia Jina la Yesu Kristo kwa kuwa nasi tangu kuanza mwaka wa 2014. Kwa uaminifu, neema na rehema zake ametuvusha salama na kwa imani tutauona mwaka wa 2015. Inawezekana umepoteza wapendwa wako, lakini huna budi kumshukuru na kumtukuza Mungu kwa neema na fadhili zake nyingi alizokutendea.

Pili, tunawashukuru wasomaji na wapenzi wetu wote kwa sababu uwepo wenu ndiyo uwepo wa blogu hii. Mungu wa mbinguni, Yehova awabariki wote na kuwajalizia haja za mioyo yenu kupitia Jina lipitalo majina yote la Yesu Kristo, Amina.

Tatu, tungependa kuwakumbusha kuwa siku kuu za Krismasi na Mwaka mpya zina maana tofauti na jinsi tunavyo zisherehekea. Krismasi ni siku ya kuzaliwa kwa Mfalme, mkombozi wa wanadamu kutoka utumwa wa shetani. hivyo basi, itumie siku hii kuutafakari upendo mkuu wa Mungu na Yesu Kristo kwako, na ukubali kujiachilia moyo wako wazi mbele za Mungu ili "Utatu mtakatifu wa Mungu" uingie na kuishi nawe.
Mwaka mpya ni siku kuu inayotukumbusha neema na rehema za Mungu kwetu, kwamba katika mwaka unaoisha kuna makosa tulimkosea Mungu, lakini bado kwa upendo wake ametuzawadia uzima na afya ambavyo hatukuvistahili kwa kuenenda kwetu katika kutimiza tamaa za miili yetu. Hivyo basi, hatuna budi kutubu, kutengeneza tena uhusiano mzuri na Mungu wetu kupitia damu iokoayo ya Yesu Kristo.

Katika kipindi hiki kifupi cha siku kuu za Krismasi na Mwaka mpya weka historia nzuri ya ushindi, tumia kipindi hiki kujenga umoja, ukaribu na mshikamano, mkiongeza chachu ya upendo na furaha katika familia. Kwa sababu familia yenye amani, furaha na upendo ndiyo familia yenye mafanikio ya kiroho na kimwili.

"KHERI YA KRISMASI NA FURAHA YA MWAKA MPYA WENYE MAFANIKIO, 2015"


Monday, August 4, 2014

MATENDO YAKO YAMECHAGUA NJIA GANI BAADA YA KIFO?



Torati 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako”

Hilo lilikua ni neno la Mungu mwenyewe akimwambia Musa na wana wa Israeli, neno hilo ni kwa ajili yako leo. Mungu anaweka mashahidi wawili, mbingu na nchi, anapoweka njia mbili mbele yako na kukushauri njia ya kuchagua.

Mungu anakushauri uchague uzima ili uwe hai, haimaanishi hutakufa, la hasha, bali siku ya ufufuo na hukumu ya haki ya Mungu utapata ufufuo wa uzima wa milele. Ikiwa utachagua mauti, utapata ufufuo wa hukumu ya uharibifu pamoja na dunia hii itakayokunjwa kama karatasi na kutupwa jehanamu kutakako kuwako kilio na kusaga meno.

Yohana 14:6 “Yesu akawaambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi”

Yesu Kristo ndiye njia, kweli na uzima. Kwa maana nyepesi, Mungu anakushauri kuichagua njia yenye uzima. Kwa maneno mengine, Mungu anakushauri kumchagua Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako. Kwa sababu Yesu Kristo ndiye njia pekee ielekeayo uzimani, kule Mungu anakushauri uchague.

Kama bado hujamchagua Yesu Kristo hujachelewa, wakati bado upo, fanya uamuzi sahihi sasa (bonyeza hapa). Kama umemchagua Yesu Kristo tayari, amekuwa Bwana na Mwokozi wako, umefanya vema.

Kuingia mbinguni (kupata uzima wa milele), kunaambatana na vitu vikuu viwili; Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako na matendo yako baada ya kumchagua Yesu Kristo hadi kifo chako cha mwili huu uharibikao.

Kwa sababu siku ya hukumu ya haki ya Mungu, kila nafsi itahukumiwa kutokana na matendo yake na italipwa kwa haki kulingana na ilivyotenda hapa duniani (Yohana Mtakatifu 5:28-29 na Mathayo Mtakatifu 16:27).

Matendo yako hapa duniani ndiyo yatachagua njia utakayoiendea baada ya kifo na hukumu ya haki ya Mungu. Kifo ni fumbo lililokosa ufumbuzi, huja wakati tusiodhani, wapo waliosema watajiandaa kutengeneza maisha yao yajayo na wakaendelea kufanya uovu wa kila aina, lakini wakapatwa na kifo ghafla pasipo kujiandaa.

Ikiwa umempokea Yesu Kristo, hakikisha unajitakasa kila iitwapo leo ili kujiweka tayari na safari isiyojulikana itakuwa lini. Na ikiwa bado hujampokea Yesu Kristo, nafasi ndiyo hii, amua sasa.

Hukumu ya jehanamu haitapendelea waliokiri kumpokea Yesu Kristo na hali matendo yao ni maovu. Anayestahili mapigo, atapata mapigo, hii ni kulingana na matendo ya kila nafsi hapa duniani (Luka Mtakatifu 12:45-48).

Sunday, May 18, 2014

NAMNA UNAVYOPITA KATIKA JARIBU NDIYO KUNAAMUA NAMNA YA USHINDI UTAKAOUTA



Maana na makusudi ya kujaribiwa
 Jaribu linasemekana kuwa ni mtaji wa kuinua imani ya mtu anayejaribiwa, lakini binafsi ninapenda kuirekebisha sentensi hii. Jaribu ni mtaji wa kuinua imani ya anayeshinda jaribu; kama umejaribiwa na jaribu likakuangusha, siyo sahihi kusema jaribu hilo lililokuangusha lilikuwa mtaji wa kuinua imani yako. Imani ipi? Kama umeshindwa kuitetea imani yako na kuangushwa, jaribu halikuwa mtaji kwako. 

Jaribu huja na makusudi mawili; moja, ni kumuimarisha kiroho na kuinua imani ya anayejaribiwa na kushinda jaribu. Pili, ni kumuangusha mtakatifu na kuharibu uhusiano wake na Mungu. Na mara nyingine jaribu au teso huwa ni kiboko cha Mungu cha kulirudi kanisa lake. Ninaposema kanisa ninamaanisha Mkristo.

Kuinua imani ya Mkristo. Nikupe mfano kwanza, kuna hekima ya Kimungu na hekima ya kibinadamu.  Hekima ya Kimungu hupewa mtu yoyote pasipo kujari umri, na hii huletwa na Yesu Kristo mwenyewe. Na hekima ya kibinadamu huja kutokana na uzoefu wa muda mrefu alionao mtu katika jambo fulani, na hekima hii wanayo wazee. Na imani ndivyo ilivyo, ili ikue ni lazima ipitishwe katika kujaribiwa, ipitishwe katika vitu ambavyo sayansi na akili ya kibinadamu haviwezekani. Ukiisha pita hapo kwa msaada wa Mungu kwa jina la Yesu Kristo ndipo imani yako inapokuwa. Ndipo unapozidisha imani na uhusiano wako na Mungu kupitia Yesu Kristo (Yohana 11:3-4, 14-15 na 1 Petro 1:6-7)

Kumuangusha mtakatifu. Hili ni jaribu linalosababishwa na shetani moja kwa moja, na makusudi yake huwa ni kumuangusha mtakatifu ili kuharibu na kufuta kabisa uhusiano wake na Mungu. Kwa mfano, Ayubu hakujaribiwa ili kuinua imani yake au kurudiwa na Mungu, alijaribiwa ili amkufuru Mungu, kwa Kiswahili chepesi ni ili avunje uhusiano wake na Mungu. Kwa hiyo kuna wakati shetani huwajaribu Wakristo ili awafarakanishe na Mungu (Yohana 2:10, Ayubu 2:4-5)

Kurudiwa na Mungu. Hapa naomba nieleweke, hili kwa upande mmoja siyo jaribu na kwa upande mwingine ni jaribu. Nina maana gani; kwa upande wa Mungu ni kiboko cha kulirudi kanisa lake kama ilivyo kwa mzazi anapomuadhibu mtoto aliyekosea. Kwa upande wa Mkristo, analiona kama jaribu. Na hili hutupata ikiwa tumekengeuka na kuiacha njia ya haki, tumemkosea Mungu. Na tukitubu na kuirudia njia ya haki, utaona mateso yote yanaondoka pia (Mithali 3:11-12, Ayubu 5:17)

Nini cha kufanya uwapo katika jaribu
Kuna makosa makubwa mawili ambayo Wakristo wengi tunayafanya tuwapo katika majaribu. Na makosa haya ndiyo yanayogharimu uhusiano wetu na kutufarakanisha na Mungu. Makosa hayo ndiyo yanayofanya tunaangushwa na majaribu.

Kosa la kwanza; tunatumia akili zetu kutafuta ufumbuzi wa jinsi gani tutavuka jaribu tunalopitia kwa ushindi na kumuacha Mungu kando ambayo ndiye msaada wetu. Hapa ni lazima uelewe, Mungu pekee ndiye anayetushindia majaribu, kwa akili zetu na nguvu zetu na maarifa yetu hatuwezi kamwe kujinasua katika majaribu. Uwapo katika jaribu ni lazima umkabidhi Mungu njia zako na jaribu lako, Yeye ndiye ushindi wako kwa Jina la Yesu Kristo (2 Petro 2:9, Zaburi 37:5)

Kosa la pili; kuwaangalia wanadamu wanafanya nini na wanasema nini tunapopita katika jaribu hasa wapendwa au wakristo wenzetu. Kitu tunachojisahau hapa ni kwamba tunategemea wingi wa marafiki tunaokuwa nao wakati wa furaha ndio hao hao tutakao kuwa nao wakati wa majaribu, sivyo! Uwapo katika shida au jaribu kama kuna mkristo mwenzako atabaki na wewe hiyo ni neema tu ya Mungu, lakini wengi kama siyo wote watakuacha peke yako.

Unajua kwa nini watakuacha peke yako? Jaribu siyo lao ni lako, anayepaswa kushinda siyo weo ni wewe. Kwa hiyo ni lazima upite peke yako ili ushinde peke yako na tuzo ya ushindi utapata peke yako. Hupaswi kuwaangalia wapendwa na hupaswi kulalamika iwapo watakuacha upite katika jaribu peke yako.

Wednesday, April 16, 2014

KUFANYIKA RAFIKI WA MUNGU

Bwana Yesu Asifiwe mpendwa msomaji wangu, karibu tumalizie somo letu. nina imani Mungu atakufundisha kitu kipya. Karibu.



Yohana 1:12. “Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio Jina lake”.

Katika mstari huo juu, tunajifunza vitu vikubwa viwili kulingana na somo letu. Moja, kufanyika watoto wa Mungu. Pili, kuliamini Jina la Yesu Kristo au kumuamini Yesu Kristo. Kumbuka somo letu linasema “kuukulia wokovu na neema ya Mungu”, katika somo la kwanza tuliona namna ya kumuamini Mungu (Yehova) na Yesu Kristo. Kupitia imani hiyo ndipo tunapata haki ya wokovu.



Kwa maana hiyo, tunapoamini na kupata wokovu tunafanywa kuwa wana wa Mungu aliye hai (Yehova). 

Kuwa mtoto wa tajiri na kuwa mtoto wa tajiri na wakati huo huo rafiki wa moyoni ni vitu viwili tofauti na kuna faida tofauti. Utanielewa baada ya vifungu vifuatavyo vya Biblia.

Isaya 41:8. “Nawe, Israeli, mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu (Mungu)”

Yakobo 2:23.”Maandiko yale yakatimizwa yaliyonena, Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa Mungu

Katika mstari wa kwanza tumejifunza kuwa ukimwamini Mungu na Yesu Kristo unafanyika mtoto wa Mungu, lakini katika mistari miwili ya hapo juu tunaona kuwa kuna watu ambao Mungu anawaita rafiki zake.

Hata wewe leo hiii ukiamua kuendelea mbele zaidi na uhusiano wako na Mungu kutoka kuwa mtoto wa Mungu hadi kufikia kuwa rafiki wa Mungu, INAWEZEKANA, hebu tuangalie mstari ufuatao kwa uthibitisho;

Yohana 15:14. “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo”.

Kwa hiyo katika mstari huo hapo juu tunaona jinsi Yesu Kristo anavyokiri kuwa kuna watu wanaoweza kuwa rafiki wa Mungu. Lakini ipo gharama katika kuwa rafiki wa Mungu, gharama hiyo ni kutenda kila Mungu analokuamuru kulitenda pasipo kuchagua.

Na, kufanyika rafiki wa dunia ni kufanyika adui wa Mungu. Kutenda kwa kufuatisha namna na mwenendo wa dunia unaopendeza na kuvutia macho ambao ndani yake kuna udhalimu ni kujifanya rafiki na dunia. Na kwa njia hiyo (kuwa rafiki wa dunia) tunajiondolea haki na nafasi ya kuwa rafiki wa Mungu (Yakobo 4:4, Warumi 8:7)

Kuna faida katika kuwa mtoto na rafiki wa Mungu, kumbuka mfano wangu wa kwanza. Ukiwa mtoto na rafiki wa Mungu, Mungu hatakuficha kitu (Yohana 15:15).

Kumbuka, Mungu alipowatuma Malaika kuiharibu miji ya Sodoma na Gomora; wale Malaika walipokelewa na Ibrahimu na Lutu. Lakini Mungu alimfunulia siri hiyo Ibrahimu kwanza, ni kwa sababu Ibrahimu alikuwa rafiki wa Mungu (Mwanzo 18:17).

Katika kumalizia somo letu lenye kichwa “HATUA ZA KUUKULIA WOKOVU NA NEEMA YA MUNGU”, tunamalizia na HATUA YA KUFANYIKA RAFIKI WA MUNGU.

KUDOWNLOAD PDF YA SOMO LOTE, BONYEZA HAPA

KUMPOKEA YESU KRISTO KUWA BWANA NA MWOKOZI WAKO, BONYEZA HAPA

Thursday, March 27, 2014

2. KUMJUA MUNGU, MUNGU KUKUJUA NA KUMJULISHA MUNGU KWA WENGINE

Bwana Yesu asifiwe sana mpendwa msomaji wangu!

Tunaendelea na somo letu lenye kichwa, "HATUA ZA KUUKULIA WOKOVU NA NEEMA YA MUNGU", na sasa tupo sehemu ya pili. ni imani yangu kuwa Roho wa Mungu atakuhudumia. Endelea...



(a). Kumjua Mungu
Yeremia 9:23-24. Bwana asema hivi, mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekima yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake; bali ajisifuye na ajisisfu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni Bwana, nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo, asema Bwana.

Unapochukua uamuzi wa kuokoka au kuamua kuwa mfuasi wa Mungu na Yesu Kristo, ni lazima umjue huyo Mungu unayemtumikia kwa kina na marefu. Ni lazima uujue uwezo wake, nguvu zake, neema zake, rehema zake na kila kitu kumuhusu yeye. Kama utakuwa unamuabudu na kumtumikia Mungu usiyemjua, ni lazima utakuwa mfuasi wa dini na siyo mfuasi wa Mungu unayedai kumtumikia. Na kwa taarifa yako, ukikubali kuwa mfuasi wa dini na siyo Mungu aliye hai, Yehova na Yesu Kristo basi unapoteza muda wako.

Kumjua Mungu siyo jambo jepesi kiasi unachoweza kufikiria, ni kazi ngumu kama kazi ngumu nyingine unazozijua. Inahitaji uvumilivu na nia thabiti ya moyo katika kumjua Mungu ipasavyo(Kutoka 33:13). Kwa tabia za waumini wa siku hizi, za kwenda nyumba ya ibada na kusubiri kusikiliza mahubiri na shuhuda mbali mbali za watu ni vigumu kumjua Mungu wanayemtumikia.

Kinachohitajika hapa ni muumini au mfuasi wa Mungu na Yesu Kristo kuchukua hatua thabiti na kuvaa moyo wenye nia ya kumjua Mungu, wewe mwenyewe unatakiwa kumtafuta Mungu ipasavyo (Mithali 8:17), Mungu mwenyewe anasema wale wanitafutao kwa bidii wataniona.

Kumjua Mungu ni lazima uwe rohoni, kwa sababu Mungu ni Roho na anafunuliwa kwa watu waliopo rohoni tu kupitia Roho Mtakatifu. Kwa hiyo ni lazima ukubali kuwa rohoni na ukubali kuongozwa na Roho Mtakatifu ili umjue Mungu (1 Wakorintho 2:9-12).

Kutokumjua Mungu unayemtumikia kuna hatari kubwa sana; kwanza hutomwabudu katika roho na kweli, hutomuamini kwa kiwango kinachotakiwa. Pili utayumbishwa na imani zinazoibuka kila leo. Na tatu, unaweza kuabudu miungu na siyo Mungu pasipo wewe kujua. Chukua hatua ya kuamua kumjua Mungu ipasavyo.

Wednesday, March 12, 2014

HATUA ZA KUUKULIA WOKOVU NA NEEMA YA MUNGU



 Tangu kutungwa kwa mimba hadi mtoto anapozaliwa, kuna hatua mbali mbali za ukuaji na majina ya hatua hizo hutofautiana kutoka hatua moja hadi hatua nyingine. Inapotokea mtoto amezaliwa, lakini haongezeki kimo, uzito, ufahamu licha ya kuongezeka kwa idadi ya miaka, hicho ni kiashilia tosha kuwa mtoto huyo ana matatizo ya ukuaji kiafya. Ni lazima wazazi wa mtoto huyo watafute msaada wa kitabibu haraka sana iwezekanavyo.

Katika ulimwengu wa kiroho pia, mtu yoyote anapompokea Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wa maisha yake, anakuwa amepokea wokovu. Wokovu unalingana na ukuaji wa mwanadamu, ni lazima mtu huyu aukulie wokovu na neema ya Mungu kutoka hatua ya kwanza kabisa hadi kufikia hatua ya mwisho ambayo ni ufufuo wa uzima wa milele.

Katika somo letu hili lenye kichwa, “hatua za kuukulia wokovu na neema ya Mungu”, tutajifunza hatua kuu tatu ambazo mtu aliyeokoka ni lazima azipitie. Ni maombi yangu kwamba, Roho Mtakatifu akufundishe kwa utulivu na undani ili upate kuelewa na kujitambua uko hatua ipi na unatakiwa kwenda hatua ipi, na ufanye nini ili kuifikia hatua iliyopo mbele yako.

Hatua za kuukulia wokovu na neema ya Mungu, nimezigawa katika hatua kuu tatu ambazo zina hatua nyingine ndogo ndogo ndani yake kulingana na vile Roho Mtakatifu alivyonijalia;

Kuamini na kuokoka

Kumjua Mungu, kumjulisha Mungu kwa wengine na Mungu kukujua wewe

Kufanyika rafiki wa Mungu

1. KUAMINI NA KUOKOKA

(a). kuamini
Marko 16:16, aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini atahukumiwa
Yohana 3:16, kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu (mwanadamu), hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele (wokovu)
Katika mistari miwili hiyo hapo juu, kuna kitu tunajifunza. Kitu hicho ni lazima kuamini ndipo wokovu upatikane. Kwa sababu hiyo huwezi kupata wokovu pasipokumuamini Mungu na Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wa maisha yako.

Siyo kila mtu anayemjua Mungu na Yesu Kristo, anamuamini Mungu na Yesu Kristo. Na siyo kila anayemuamini Mungu anamuamini na Yesu Kristo. Na ndiyo sababu siyo wanadamu wote tunaolisikia neno la Mungu tumeokoka.

Kwa sababu hiyo, ni lazima mtu aamini kuwa Mungu yupo, anaishi milele, Yesu Kristo ni mwana wa Mungu (Mathayo 16:16, Luka 1:35), aliyekufa msalabani na kufufuka ili atuokoe (Mathayo 26:28).
Na siyo kuamini tu Mungu yupo, ni lazima ijulikane kuwa Mungu unayemuamini ni Yehova (ndilo Jina lake), tena anaishi milele. Ninasema hivi kwa sababu, hata wanaoabudu sanamu, wanyama au miti mikubwa nao pia wana Imani kuwa hivyo vitu wanavyoviabudu ndiyo miungu yao.

(b). kuokoka
Kuokoka ni kuamini kuwa Yesu Kristo ni Bwana na Mwokozi wa maisha yako, kukiri kwa kinywa imani hiyo na kubadilika kutoka kuishi maisha ya dhambi na kuishi maisha matakatifu ya kupendeza Mungu.

Kwa maana hiyo, imani peke yake haitoshi kumpa mtu wokovu, ni lazima aikiri imani hiyo kwa maneno ya kinywa chake pasipo kulazimishwa au kushawishiwa (Warumi 10:9)

Haitakiwi mtu apate wokovu kwa kulazimishwa au kushawishiwa; kwa mfano mtu anaamua kuokoka ili amuoe au aolewe na mtu fulani aliyeokoka. Wengi wa watu wa aina hii hawawezi kuukulia wokovu kwa viwango vinavyostahili, kwa sababu hawakuokoka ili kumpokea Yesu Kristo bali waliokoka ili wampate mtu fulani. Wengi wao wanakuwa na wokovu wa kifafa.

(c). Hatua za kuokoka
(i). kuisikia injili ya Yesu Kristo
Ni lazima uisikie injili ya Yesu Kristo kwanza ili upate kumjua Mungu na Yesu Kristo kisha ujenge Imani itakayo kupelekea kuupata wokovu (1 Petro 1:23, Marko 16:15-16).

(ii). Kuamini
Baada ya kuisikia injili, kinachofuata ni kujenga imani ya ile injili uliyoisikia (Wagalatia 3:26). Na hapa ndipo penye tatizo, kama umeisikia imani potofu basi utakuwa ukiamini na kuabudu watu, vitu, wanyama; vitu visivyo Mungu wa kweli aliye hai. 

Kwa sababu hiyo, kabla ya kuamini ni vema ukachunguza ni Mungu yupi anayehubiriwa hapo, siyo kila mungu anayehubiriwa anastahili kuabudiwa. Ni Mungu mmoja tu ndiye anayestahili kuabudiwa, jina lake Yehova ambaye kupitia Yesu Kristo tunapata wokovu na uzima wa milele.

(iii). Kuokoka
Baada ya kuisikia injili ya Yesu Kristo, unapata Imani ya injili uliyoisikia, hatua inayofuata ni kuokoka kwa kuikiri imani uliyoisikia na kufanyika mwanafunzi wa Yesu Kristo ukiacha njia zote ovu na kufuata njia ya haki kama lisemavyo neno la Mungu (Warumi 10:10).

(d). Imani ni lazima ikue au iongezeke
Baada ya kuamini na kupokea wokovu, hutakiwi kubaki pale pale kama jinsi siku ya kwanza ulipoamini na kuokoka ulivyokuwa. Unatakiwa kuilinda imani na wokovu wako, na imani yako ni lazima ikue au iongezeke, kutoka kiwango hadi kiwango, kutoka chini kupanda juu (2 Korintho 10:15 na 2 Thesalonike 1:3).

Mpendwa msomaji wangu ni imani yangu kuwa kuna kitu kipya Roho Mtakatifu amekufundisha, usikose sehemu ya pili ya somo hili. Mungu akubariki sana, na akubariki zaidi kwa kushiriki na wengine masomo haya. Amina. 

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts