Thursday, March 27, 2014

2. KUMJUA MUNGU, MUNGU KUKUJUA NA KUMJULISHA MUNGU KWA WENGINE

Bwana Yesu asifiwe sana mpendwa msomaji wangu!

Tunaendelea na somo letu lenye kichwa, "HATUA ZA KUUKULIA WOKOVU NA NEEMA YA MUNGU", na sasa tupo sehemu ya pili. ni imani yangu kuwa Roho wa Mungu atakuhudumia. Endelea...



(a). Kumjua Mungu
Yeremia 9:23-24. Bwana asema hivi, mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekima yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake; bali ajisifuye na ajisisfu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni Bwana, nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo, asema Bwana.

Unapochukua uamuzi wa kuokoka au kuamua kuwa mfuasi wa Mungu na Yesu Kristo, ni lazima umjue huyo Mungu unayemtumikia kwa kina na marefu. Ni lazima uujue uwezo wake, nguvu zake, neema zake, rehema zake na kila kitu kumuhusu yeye. Kama utakuwa unamuabudu na kumtumikia Mungu usiyemjua, ni lazima utakuwa mfuasi wa dini na siyo mfuasi wa Mungu unayedai kumtumikia. Na kwa taarifa yako, ukikubali kuwa mfuasi wa dini na siyo Mungu aliye hai, Yehova na Yesu Kristo basi unapoteza muda wako.

Kumjua Mungu siyo jambo jepesi kiasi unachoweza kufikiria, ni kazi ngumu kama kazi ngumu nyingine unazozijua. Inahitaji uvumilivu na nia thabiti ya moyo katika kumjua Mungu ipasavyo(Kutoka 33:13). Kwa tabia za waumini wa siku hizi, za kwenda nyumba ya ibada na kusubiri kusikiliza mahubiri na shuhuda mbali mbali za watu ni vigumu kumjua Mungu wanayemtumikia.

Kinachohitajika hapa ni muumini au mfuasi wa Mungu na Yesu Kristo kuchukua hatua thabiti na kuvaa moyo wenye nia ya kumjua Mungu, wewe mwenyewe unatakiwa kumtafuta Mungu ipasavyo (Mithali 8:17), Mungu mwenyewe anasema wale wanitafutao kwa bidii wataniona.

Kumjua Mungu ni lazima uwe rohoni, kwa sababu Mungu ni Roho na anafunuliwa kwa watu waliopo rohoni tu kupitia Roho Mtakatifu. Kwa hiyo ni lazima ukubali kuwa rohoni na ukubali kuongozwa na Roho Mtakatifu ili umjue Mungu (1 Wakorintho 2:9-12).

Kutokumjua Mungu unayemtumikia kuna hatari kubwa sana; kwanza hutomwabudu katika roho na kweli, hutomuamini kwa kiwango kinachotakiwa. Pili utayumbishwa na imani zinazoibuka kila leo. Na tatu, unaweza kuabudu miungu na siyo Mungu pasipo wewe kujua. Chukua hatua ya kuamua kumjua Mungu ipasavyo.


(b). Mungu naye akujue
Kuna aina tatu za watu Mungu anaowajua, jichunguze wewe Mungu anakujua kwa aina ipi? Kisha rekebesha ikistahili.

Moja; ni wale watu ambao Mungu anawajua kwa uovu wao uliofika katika kiti chake cha enzi, watu ambao Mungu amewageuzia kisogo asiuone uovu wao (Ufunuo 3:1)

Pili; ni wale watu ambao Mungu anawajua kwa kuchanganya mambo, leo wameokoka kesho hawajaoko, keshokutwa wamerudi, mtondogoo wameanguka tena (Ufunuo 3:15). Watu hawa wanakiri kumpenda Mungu lakini wanatenda mapenzi ya shetani.

Tatu; ni wale watu ambao Mungu anawajua kwa matendo mema, wanampendeza Mungu kwa kutii na kutenda amri na sheria zake (Ufunuo 2:19).

(c). kumjulisha Mungu kwa wengine
Kumjulisha Mungu na Yesu Kristo kwa wengine ni jambo la lazima mara tu baada ya kuchukua uwamuzi wa kuokoka. Kumwambia mwengine siri ya mafanikio ni uwamuzi wako, ukipenda utamwambia na usipopenda hutamwambia. Lakini kumjulisha Mungu na Yesu Kristo kwa wengine ni lazima na siyo uamuzi wako, kwa sababu ni agizo la Yesu Kristo mwenyewe (Marko 16:15).

Kuna njia nyingi za kumjulisha Mungu kwa wengine; kuhubiri, kufundisha, kuimba. Unaweza kuitumia njia moja wapo katika hizo ili mradi injili ya Mungu isonge mbele. Cha muhimu hapa, ni kutengeneza matendo yako kwanza, kwa sababu matendo yana nguvu katika kuhubiri kuliko kelele za mwaka mzima. Na kumuhubiri Mungu na Yesu Kristo ni jambo endelevu, halina ukomo au likizo (Yohana 17:26a).

Mungu aishiye milele, Yehova na akubariki sana kwa kushiriki sehemu hii ya somo hili, kwa Jina la Yesu Kristo. Amina.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts