Monday, August 4, 2014

MATENDO YAKO YAMECHAGUA NJIA GANI BAADA YA KIFO?



Torati 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako”

Hilo lilikua ni neno la Mungu mwenyewe akimwambia Musa na wana wa Israeli, neno hilo ni kwa ajili yako leo. Mungu anaweka mashahidi wawili, mbingu na nchi, anapoweka njia mbili mbele yako na kukushauri njia ya kuchagua.

Mungu anakushauri uchague uzima ili uwe hai, haimaanishi hutakufa, la hasha, bali siku ya ufufuo na hukumu ya haki ya Mungu utapata ufufuo wa uzima wa milele. Ikiwa utachagua mauti, utapata ufufuo wa hukumu ya uharibifu pamoja na dunia hii itakayokunjwa kama karatasi na kutupwa jehanamu kutakako kuwako kilio na kusaga meno.

Yohana 14:6 “Yesu akawaambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi”

Yesu Kristo ndiye njia, kweli na uzima. Kwa maana nyepesi, Mungu anakushauri kuichagua njia yenye uzima. Kwa maneno mengine, Mungu anakushauri kumchagua Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako. Kwa sababu Yesu Kristo ndiye njia pekee ielekeayo uzimani, kule Mungu anakushauri uchague.

Kama bado hujamchagua Yesu Kristo hujachelewa, wakati bado upo, fanya uamuzi sahihi sasa (bonyeza hapa). Kama umemchagua Yesu Kristo tayari, amekuwa Bwana na Mwokozi wako, umefanya vema.

Kuingia mbinguni (kupata uzima wa milele), kunaambatana na vitu vikuu viwili; Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako na matendo yako baada ya kumchagua Yesu Kristo hadi kifo chako cha mwili huu uharibikao.

Kwa sababu siku ya hukumu ya haki ya Mungu, kila nafsi itahukumiwa kutokana na matendo yake na italipwa kwa haki kulingana na ilivyotenda hapa duniani (Yohana Mtakatifu 5:28-29 na Mathayo Mtakatifu 16:27).

Matendo yako hapa duniani ndiyo yatachagua njia utakayoiendea baada ya kifo na hukumu ya haki ya Mungu. Kifo ni fumbo lililokosa ufumbuzi, huja wakati tusiodhani, wapo waliosema watajiandaa kutengeneza maisha yao yajayo na wakaendelea kufanya uovu wa kila aina, lakini wakapatwa na kifo ghafla pasipo kujiandaa.

Ikiwa umempokea Yesu Kristo, hakikisha unajitakasa kila iitwapo leo ili kujiweka tayari na safari isiyojulikana itakuwa lini. Na ikiwa bado hujampokea Yesu Kristo, nafasi ndiyo hii, amua sasa.

Hukumu ya jehanamu haitapendelea waliokiri kumpokea Yesu Kristo na hali matendo yao ni maovu. Anayestahili mapigo, atapata mapigo, hii ni kulingana na matendo ya kila nafsi hapa duniani (Luka Mtakatifu 12:45-48).

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts