Tuesday, May 21, 2013

HII NDIYO DAWA YA AMANI YA TANZANIA.



   Amani ni hali ya ukosefu wa inayohusu au kusababishwa na vurugu au mapigano ya aina fulani au uwepo wa vurugu au mapigano ya namna yoyote ile katika sehemu fulani. Kunapotea vuguvugu ya uwepo wa vurugu au mapigano baina ya pande mbili, watu wakiingiwa na hofu kuhusiana na kutegemewa kuwepo kwa vurugu au mapigano hayo, watu hao husemekana wamekosa amani. Hali kadhalika uwepo wa vurugu au mapigano yenyewe ndiyo kabisa watu hukosa amani.

Tunaposema mtu au watu wana amani ni lazima uwepo usawa baina ya watu hao katika nyanja mbali mbali kama; usawa kwa mambo ya kijamii, kiuchumi, kisiasa, kikabila, kiitikadi au kiimani za dini. Pasiwepo na mwenye kujiona ni bora na anafaa zaidi ya mwengine. Na pia ni lazima yawepo mahusiano mazuri baina ya mtu mmoja na mwengine.

Kunapotekea kutokuwepo kwa usawa na kuvumiliana katika siasa, manufaa ya mgawanyo wa faida zitokanazo na rasilimali za nchi, ukabila na hata tofauti za dini, amani huvunjika.

Amani inapovunjika husababisha mapigano ya wenyewe kwa wenyewe, yajulikanayo kama vita ya wenyewe kwa wenyewe. Ni tofauti ndogo tu, ambazo huonekana hazina matokeo hasi kwa jamii ndizo zilizopelekea ukosefu wa amani na vita ya wenyewe kwa wenyewe katika mataifa mengi tunayoyajua yana vita.

Na ili machafuko yatokee, ni lazima kuwepo na watu wanaosukuma na kuchochea machafuko hayo. Ni lazima awepo mtu mwenye kupindisha ukweli wa mambo au kama siyo kupindisha basi ni kufikisha ujumbe au ombi lake kwa njia yenye uchochezi wa machafuko yanayopelekea ukosefu wa amani.

Na wachochezi wa machafuko na uvunjifu wa amani ni watu wenye ushawishi mkubwa kwa kundi kubwa la watu, na watu wanaotumiwa ni wale ambao mara nyingi huwa hawafikirii matokeo ya kile wanachokwenda kukifanya.

Kumekuwa na kutokuelewana na kutovumiliana baina ya dini mbili hapa nchini kwetu, vurugu zinazoweza kusababisha machafuko na hata vita kama tu hatua za makusudi za kuitafuta amani na maelewano baina ya pande hizi hazitafanyika. Kwa sababu mataifa yaliyopo katika vita kutokana na tofauti za dini, yalianza hivi hivi na wahusika wakazifumbia macho chachu hizo kwa sababu waliziona ni kitu kidogo sana.

MATOKEO YA UVUNJIFU NA UKOSEFU WA AMANI.
Vifo. Machafuko ya aina yoyote, huambatanisha uwepo wa chuki baina ya pande mbili. Chuki hiyo hupelekea mapigano ya kutumia silaha aidha za jadi au silaha za moto. Na kama ilivyo ada, silaha inapotumika husababisha majera au kifo. Na idadi kubwa ya watu wanaokufa ni watoto na wanawake. 

Hivyo basi, kabla hatujaingia katika uvunjifu wa amani ni lazima tujue kuwa miongoni mwa watakao uwawa ni mama zetu, wake zetu, watoto wetu na hata wapendwa wetu.


Uharibifu wa miundo mbinu. Miundo mbinu tuliyoijenga kwa miaka mingi na fedha za madeni kutoka mataifa tajiri, tutakwenda kuiharibu ndani ya muda mfupi tu wa mapigano yasiyo na tija. Na katika kipindi chote cha vita na machafuko, uchumi wa nchi nao utakuwa unaporomoka. 

Njaa. Taifa lolote linaloingia katika mapigano ya wenyewe kwa wenyewe ni lazima litakumbwa na njaa, hii ni kutokana na hofu inayowakalia watu wake na kuwafanya wawe wakimbizi ndani ya nchi yao wenyewe. Na hii husababisha ukosefu wa ujasiri wa kwenda mashambani, masokoni na hata kufanya shughuli yoyote ya kujiingizia kipato, hivyo hukaribisha njaa. Na matokeo ya njaa ni kifo, hata wale walionusurika kufa kwa silaha za mapigano hufa kwa njaa.

Ubakaji. Tumekuwa tukisikia kutoka katika nchi zenye vita kuwa wanawake, mabinti na hata watoto walio chini ya umri wa miaka 18 wamekuwa wakibakwa hovyo pasipo msaada wowote. Na kitu cha kujiambia na ndiyo ukweli wenyewe ni huu; asipobakwa mama yako, atabakwa dada yako, kama sivyo basi mke wako au hata binti yako. Fikiri kabla ya kutenda!

Wakimbizi. Tumezoea kuitwa kisiwa cha amani na kuwapokea wakimbizi wanaozikimbia nchi zao kutokana na machafuko na vita ya wenyewe kwa wenyewe, kwa nini sasa tunajaribu kuivuruga amani yetu? Tunatamani kuwa miongoni mwa nchi zinazozalisha wakimbizi duniani? Labda ni fahari!?

Soko la viwanda vya kutengeneza silaha. Kuna mataifa makubwa yanayomiliki viwanda vya kutengeneza silaha, silaha za kila aina ambazo hazitumiki na haziuziki sana wakati wa amani. Taifa lolote linaloingia katika machafuko ya kivita hugeuzwa kuwa soko la mataifa hayo yanayotengeneza silaha. Ndiyo sababu utasikia wapiganaji wa serikali wanapata silaha kutoka taifa Fulani na waasi wanapata silaha kutoka taifa Fulani. Siyo kwamba wanapatiwa silaha hizo bure, wanazinunua iwe serikali au waasi na kama siyo kuzinunua ni kwa njia ya mabadilishano na rasilimali za nchi husika mfano mafuta, madini n.k. Tusikubali kuingia katika vita.

NINI CHA KUFANYA.
Dawa ya amani ya Tanzania ipo! Hatuhitaji kuyaita mataifa au chombo chochote cha kimataifa cha amani kutupa dawa, dawa tunayo sisi wenyewe. Haya yafuatayo ndiyo dawa ya amani yetu.

Vyombo vya dini. Hapa namaanisha dini zote mbili ni lazima zijiulize, miaka yote iliyopita ziliishi kwa amani na maelewano kuna nini sasa hata maelewano yale na kuvumiliana kule kukaondoka kirahisi hivyo? Lazima dini zote mbili zisimame imara kuhakikisha zinaitetea na kuidumisha amani ya Taifa letu kwa kuihubiri amani na upendo baina ya wafuasi wake na kati ya wafuasi wa dini nyingine.


Wanasiasa na viongozi wa serikali. Hawa nao ni watu wenye ushawishi mkubwa kwa wafuasi wa vyama vyao vya siasa na jamii kwa ujumla. Wanasiasa na viongozi wa serikali ni lazima wachunge ndimi zao, kwani kulopoka maneno yenye uchochezi wa uvunjifu wa amani haifai na sisi wananchi mwasiasa yoyote au kiongozi yoyote anayechochea uvunjifu wa amani yetu huyo hatufai leo wala kesho, hapaswi kuchaguliwa kabisa kuwa kiongozi wetu.

Wananchi na wafuasi wa dini. Sisi tusikubali kutumika kama chombo cha kutimiza matakwa ya wengine kwa manufaa yao binafsi, kama tuliweza kuishi kwa amani na upendo kama ndugu na tuendelee kuishi hivyo. Hatukupungukiwa na chochote na hatutapungukiwa na chochote, zaidi tutapata hasara na madhara yatokanayo na vita kama tulivyoona hapo juu. Tuiheshimu na kuitunza amani yetu kwa manufaa yetu binafsi na kizazi kijacho.

WAKRISTO.
“Mwanzo 1:27 Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba”. Ikiwa sote tuliumbwa kwa mfano wa Mungu basi sisi sote tu ndugu pasipo kuzingatia tofauti ya dini zetu.
“Warumi 12:18 mkae katika amani na watu wote “. Tunasisitizwa kuishi kwa amani na kila mtu pasipo kuzingatia tofauti ya dini yake kwetu, na ili tuishi kwa amani ni lazima tuitunze na kuilinda amani tuliyonayo na kuidumisha zaidi.
Kila Mtanzania ni lazima atafakari athari na matokeo ya uvunjifu wa amani mapema kabla hajakubali kutumika katika uvunjifu wa amani.
“MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU WABARIKI WATANZANIA, AMINA”.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts