Saturday, June 29, 2013

MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU (SEHEMU YA PILI).



YESU KRISTO ASIFIWE!

Mpendwa msomaji wangu karibu tena katika mwendelezo wa somo letu lenye kichwa kisemacho “MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU”, ikiwa leo ni sehemu ya pili. Nina imani utazidi kubarikiwa zaidi na somo hili, ikiwa ulikosa sehemu ya kwanza ya somo hili utaipata humu humu ndani ya blog hii.

Leo tunaangalia aina kuu za maombi na faida zake, na aina nyinginezo za maombi na faida zake. Ni matumaini yangu kwa msaada wa Roho Mtakatifu utajifunza vyema na Mungu atakuwa pamoja nawe.


Aina kuu za maombi na faida zake.

Maombi kabla. 
Haya ni maombi ambayo muhusika anaomba kabla hajafikwa na jambo, kwa mfano unapoamua kuombea maisha yako ya badae, familia (mke au mume na watoto) yako ya badae ilihali haujaoa au kuolewa. Unapofika wakati huo, unashangaa mambo yanaenda vizuri, ni kwa sababu ulishaomba kabla.

Mathayo 26:41a. “Kesheni mwombe, msije mkaingia majaribuni”

Yesu mwenye anasema kesheni mwombe siyo muwapo majaribuni, bali msije mkaingia majaribuni. Anamaanisha tuombe sasa, ili majaribu yajapo tusije tukaingia kwayo, kwa hiyo anatuambia tuombe sasa kwa ajili ya maisha yetu ya badae.

Waebrania 4:16. “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji”. 

Inawezekana kabisa kupata rehema na neema ya maisha na wakati wetu ujao sasa, ili tunapoyafikia maisha yetu ya baadae au kupata mahitaji katika wakati ujao tayari tunakuwa tumefunikwa na rehema na neema za Mungu na hivyo kutufanya tusimame imara. 

Faida ya maombi haya ni maombi yenye mafanikio sana, kwa sababu muombaji huomba kwa ile imani aliyonayo mbele za Mungu kupitia jina la Yesu Kristo. Hapa muombaji haombi kutokana na nguvu inayomsukuma kutoka nje, bali huomba kwa sababu anamwamini Mungu na kumfanya Mungu kuwa ndiye tumaini lake.


Maombi baada.
 
Haya ni maombi ambayo mwombaji huomba baada ya kuingia katika jambo analoliombea. Yaani mwombaji anakuwa ameingia katika shida, ndipo anamkumbuka Mungu tena baada ya njia nyingine zote kushindwa. Ina maana, anakuwa na imani na vitu vingine tofauti na Mungu, vile vitu vinaposhindwa ndipo anamtafuta Mungu.

Zaburi 69:1-2. “Ee Mungu uniokoke, maana maji yamefika mpaka nafsini mwangu. Ninazama katika matope mengi, pasipowezekana kusimama. Nimefika penye maji ya vilindi; mkondo wa maji unanigharikisha”.

Maombi haya siyo mazuri sana kama maombi kabla, kwa sababu muombaji huomba kutokana na msukumo anaoupata kutoka na shida, tatizo au hitaji alilonalo.


Maombi ya kawaida.

Ninaposema maombi ya kawaida ninamaanisha maombi yasiyoambatana na kufunga (not fasting prayers). Maombi haya yana majibu pia, hasa ukiyaambatanisha na imani na utakatifu na ukifuata vitu vya kuzingatia uwapo katika maombi au kabla ya maombi.
 

Maombi ya kufunga (fasting prayers).

Haya ni maombi ambayo muombaji huamua kuingia katika maombi pasipo kula au kunywa kwa kipindi cha muda maalumu. Kwa mfano inawezekana kufunga kwa muda wa masaa 12, 24, 48 au 72, n.k ikitegemea ukubwa na umuhimu wa kile unachokiombea.

Kufunga kunakufanya uoneshe ni jinsi gani una nia ya dhati kuelekea kile unachokiombea, na kunamfanya Mungu akutegee sikio la umakini zaidi na hivyo kuitimiza haja yako kwa wakati.

1 Wafalme 21:27-29. “Ikawa, Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa magunia mwilini mwake, akafunga, akajilaza juu ya magunia, akaenda kwa upole (mbele za Mungu). Neno la Bwana likaja kwa Eliya Mtishbi, kusema, Huoni jinsi Ahabu alivyojidhili mbele yangu? basi kwa sababu amejidhili mbele yangu, sitayaleta yale mabaya katika siku zake”.

Kwa njia ya maombi ya kufunga na ya unyenyekevu mbele za Mungu, Mungu akaiondoa hasira yake mbele za mfalme Ahabu.


 Aina nyingine za maombi.
 
Aina hizi za maombi zinaweza zikawa ndani ya aina mojawapo au mbili ya aina za maombi nilizoziongelea hapo juu katika aina kuu za maombi. Inaweza ikawa ni maombi kabla, au maombi kabla na ya kufunga ukiombea maisha yako ya baadae au watoto wako Mungu atakaokupa. 
Kwa mfano unaweza ukawa unafanya maombi ya kufunga na kufungua vifungo ambayo pia yakawa ni maombi kabla (unaombea maisha ya badae) halafu na ukawa umefunga, kwa hiyo hapo unakuwa umefanya maombi ambayo yamo ndani ya maombi makuu mawili; maombi kabla na maombi ya kufunga.

Aina hizo nyingine za maombi ni kama zifuatazo:-

Maombi ya Roho Mtakatifu.

Waefeso 6:18. “kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha katika jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote”.

Haya ni maombi ambayo muombaji anaomba akiwa amezama rohoni, na Roho Mtakatifu ndiye anayehusika kuomba kwa ajili ya muombaji. Kwa nini basi tuombe katika Roho, tuangalie kifungu cha Biblia hapa chini;

Warumi 8:26-27. “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo, aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu”.

Kuna sababu kubwa mbili za kutulazimu kuomba kwa Roho; hatujui kuomba ipasavyo na Roho hutuombea kama apendavyo Mungu. Kwa hiyo unaweza ukawa unafanya maombi ya Roho ukiombea maisha yako ya badae au familia yako au upate kazi.


Maombi ya kufunga na kufungua.

Hapa ninaposema maombi ya kufunga na kufungua simaanishi maombi ya kutokula wala kunywa, ni maombi ambayo mwombaji anatumia mamlaka aliyopewa na Yesu Kristo kuvifungia au kuvifungua vitu fulani katika maisha yake.

Mathayo 18:18. “Amini, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni, na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni”.

Kwa hiyo unaweza ukafunga kabisa magonjwa katika maisha yako na hutaweza kuugua, ama unaweza ukafungua mifereji ya baraka za rohoni na mwilini kwa watoto wako hakika watabarikiwa. Kanuni ni moja tu; imani, kwa sababu Yesu mwenyewe amesema, “amini, nawaambieni”. 

Unganisha utakatifu na vitu vingine vya kuzingatia katika maombi, ukiwa umebeba imani hakika utamuona Mungu katika viwango vya juu zaidi. Kwa hiyo unaweza ukawa unafanya maombi haya ukiyaambatanisha na maombi kabla na maombi ya kufunga.


Maombi ya kusukuma.

Haya ni maombi ambayo muombaji hung’ang’ana na kuomba hadi apokee majibu ya maombi yake, na mara nyingi waombaji wa maombi haya huwa kuna jibu wanalokuwa wanalitegemea kutoka kwa Mungu, hivyo hung’ang’ania kuomba hadi watakapolipata jibu hilo.

Luka 11:5-9. “Akawaambia, ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, rafiki yangu nikopeshe mikate mitatu kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, name sina kitu cha kuweka mbele yake; na yule wa ndani amjibu akisema, usinitaabishe, mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe? Nawaambia ya kwamba ijapokuwa aondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake. Nami nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa”.

Kabla hujaingia katika maombi haya ni vema ukamuuliza Mungu nini makusudi yake, kwani unaweza ukang’ang’ana kuomba majibu yasiyo yako, Mungu anaweza akawa amekukadilia mahali pa juu sana lakini kwa kutojua ukaomba maombi haya ukiwa umejikadilia mahali pa chini mno. Siyo kwamba Mungu hatakupa haki yako, utaopata lakini lazima uanzie kule ulikoomba ndipo upande juu.

Aina hii ya maombi, nayo unaweza ukaiambatanisha na mojawapo au zaidi ya aina zile kuu nne za maombi kutegemea na uhitaji wako.


Maombi kwa adui.

Hii ni aina ya maombi ambayo ni ngumu sana, na Wakristo wengi huwa hawaombi maombi ya aina hii. Haya ni maombi ambapo mwombaji huwaombea watesi na adui zake, huwaombea baraka, ushindi, mafanikio na ikiwezekana hata kuomboleza kwa ajili yao ili Mungu awape rehema.

Mathayo 5:43-44 na 48. “Mmesikia kwamba imenenwa, umpende jirani yako na umchukie adui yako, lakini mimi (Yesu Kristo) nawaambia, wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”.

Kuwaombea adui zetu, ni agizo la moja kwa moja kutoka kwa Yesu Kristo mwenyewe. Lakini ni Wakristo wangapi leo wanaowaombea adui zao? Na siyo tuwaombee laana, maisha mafupi, kukosa kibali, la hasha, tumeagizwa kuwaombea Baraka. Hebu tuangalie kifungu cha Biblia kifuatacho:-

Warumi 12:14. “Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani”.   

Hapa neno la Mungu halituagizi kubagua kwamba ni nani aliyetuudhi na awe amutuudhi nini, yeyote na chochote alichotuudhi, tumeagizwa kumbariki.


Maombi ya ushirika.

Haya ni maombi ambayo wanajumuiya, au Wakristo wa kanisa fulani wanashirikiana kwa umoja katika kuliombea jambo fulani; aidha linahusu kanisa au linamuhusu mshirika mmoja.

Matendo ya Mitume 1:12-14. “kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato. Hata walipoingia wakapanda orofani, walipokuwa wakikaa; Petro, na Yohana, na Yakobo, na Andrea, Filipo na Tomaso, Bartholomayo na Mathayo, Yakobo wa Alfayo, na Simoni Zelote, na Yuda wa Yakobo. Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake, na Mariamu mama yake Yesu, na ndugu zake”.

Faida ya maombi haya ni kwamba, yanaonesha umoja na ushirikianao wa kanisa au jumuiya na pia yana nguvu zaidi kuliko maombi ya mtu mmoja. Siyo lazima ufanye maombi ya ushirika na kanisa zima japo ni vizuri zaidi, lakini unaweza ukafanya na baadhi ya jamaa wachache.

Mathayo 18:19. “Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu (ushirika) watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu (Yesu) aliye mbinguni”.


Maombi kwa wengine.

Haya ni maombi ambayo muombaji hutenga siku maalumu au huamua kufanya maombi maalumu kwa ajili ya kuombea wengine, yeye hajihusishi kabisa katika maombi haya. Anakwenda mbele za Mungu akibubujika na kulia kwa sababu yaw engine.

Unaweza ukaliombea kanisa lote, Mungu alisimamishe imara na kulipa kibali, alizidishie upendo, tena ikiwezekana kwa kuwataja majina washirika wa kanisa hilo. Na siyo lazima liwe kanisa unaloabudia, unaweza hata kuliombea kanisa la jirani. Au hata kuiombea familia ya jirani yako, Mungu ailinde, aibariki na mambo mengine mazuru mengi.

Wakolosai 1:9. “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni”.

2 Timotheo 1:3. “Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavya wewe daima, katika kuomba kwangu, usiku na mchana”.

Kuombea wengine (tofauti na maombi ya kuombea adui), ni agizo kwa kanisa pia; kwa sababu tusipowaombea wengine, tunaonesha ubinafsi, na kama tutakuwa wabinafsi basi kumpenda Mungu hakupo ndani yetu. Na kama hatumpendi Mungu, tunafanya dhambi.

1 Samweli 12:23. “Walakini mimi, hasha! Nisimtende Bwana dhambi kwa kuacha kuwaombea ninyi; lakini nitawaelimisha katika njia iliyo njema, na kunyoka”.



Maombi ya sifa.

Haya ni maombi ambapo mwombaji anayatafakari matendo makuu ya Mungu aliyomtendea katika maisha yake, sehemu ngumu alizokuvusha amabzo kwa akili zako ilishindikana, wema wote ambao Mungu amekufanyia, kukuweka kuwa hai na wakati wapo uliozaliwa nao tarehe moja, mwezi mmoja au mwaka mmoja hawapo.

Ndipo muombaji hububujika na sifa mbele za Mungu wake, moyo wake humshangilia Bwana mchana na usiku.

Zaburi 34:1 na 3. “Nitamhimidi Bwana kila wakati, sifa zake zi kinywani mwangu daima. Mtukuzeni Bwana pamoja name, na tuliadhimishe jina lake pamoja”.

Sehemu nyingine katika Biblia, maombi haya ya sifa yamefananishwa na sadaka mbele za Mungu.

Hosea 14:2. “Chukueni maneno pamoja nanyi, mkamrudie Bwana; mkamwambie, ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema; na hivyo ndivyo tutakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe”. 


Maombi ya shukurani.

Maombi haya kidogo yafanane na maombi ya sifa, lakini tofauti yake ni kwamba maombi ya sifa unamtolea Mungu sifa za midomo yako kulingana na matendo yake wakati maombi ya shukrani ni kwamba unampa Mungu shukrani kwa mema yote aliyotenda kwako na hata kwa wanaokuzunguka.

Waefeso 5:20. “na kumshukuru Mungu Baba siku zote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo”.

Wakolosai 3:17. “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye (Yesu Kristo)”.

 Kwa imani niliyonayo na imani uliyonayo, Mungu akutendee sawa sawa na maombi yangu hapa chini,



"Ni maombi yangu, Bwana Mungu; afungue vilivyofungwa, arejeshe vilivyonyang’anywa, ainue huduma zilizolala, afufue huduma zilizo kufa, abariki palipo laaniwa, na akuinue mtumishi wake kutoka utukufu uliopo akupandishe juu zaidi, kwa jina la Yesu Kristo. Amina!".

Unapobarikiwa, fanyika baraka na kwa wengine. Tafadhari  shiriki somo hili katika ukurasa wako wa "twitter" na "facebook".

Usikose kamilisho la somo hili siku ya jumapili tarehe 7/7/2013, kuna kitu cha tofauti sana Mungu atakwenda kukutendea na kujibu maombi yako. Amina.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts