Monday, April 16, 2018

TUNAOWAPENDA SANA NDIYO WANAOTUUMIZA SANA: NAMNA YA KUYASHINDA MAUMIVU HAYO


Nakusalimu kupitia jina la Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo.

Binti wa umri wa miaka 5 alitenda kosa mara moja, mama yake akamchapa viboko vitatu huku akimkanya kwamba alichofanya ni kosa asilotakiwa kulirudia tena, yule binti mdogo alilia akisema, “mama nimekosa, sitarudia tena”. Kwa mara nyingine yule binti mdogo alikosea tena, siku hii baba alikuwa nyumbani, binti yule kipenzi cha baba alipokosea. Baba akamchapa binti yake kiboko kimoja na kumkanya kutorudia tena kosa lile. Yule binti mdogo alilia sana, kwa uchungu na hakutaka kubembelezwa na mtu yoyote yule isipokuwa baba yake aliyemchapa.
Katika simulizi hiyo hapo juu tunajifunza mambo makuu mawili. Mosi; binti mdogo alilia zaidi alipochapwa kiboko kimoja na baba kuliko alipochapwa viboko vitatu na mama. Hii ni sababu yule binti mdogo ni kipenzi cha baba zaidi ya mama. Alipochapwa na mama hakujali sana, aliona anafundishwa kutokosea. Lakini alipochapwa na baba aliona ameonewa, kwa upendo mkubwa wa dhati baina yake na baba yake, haikupaswa baba amuadhibu kwa kukosea kwake. Pili; binti mdogo hakutaka kubembelezwa na mtu yoyote isipokuwa baba yake aliyemuadhibu kwa sababu, kubembelezwa na baba ni sawa na baba kuomba msamaha kwa kumuadhibu binti yake, jambo ambalo lingempa faraja binti mdogo yule.
Wanadamu wote tuna tabia inayofanana na huyu binti mdogo katika simulizi hii, hivyi ndivyo tulivyoumbwa tangu utoto wetu. Tukikosewa au kutendwa na tunaowapenda sana, tunaumia sana mioyoni mwetu na kubeba maumivu ambayo hudumu mioyoni mwetu kwa muda mrefu sana kuliko tukikosewa na watu wasio karibu nasi au wapendwa kwetu. Uchungu hujaa mioyo yetu kwa sababu hatutegemei wale tunaowapenda sana kutuumiza, tunajizuia sana kutowaumiza ili tusiwapoteze, tunategemea nao wafanye sawa na hivyo. Hatuwezi kutua mzugo wa uchungu uliojaza mioyo yetu hadi pale tutakapo sikia neno la kuomba msamaha kutoka kwa waliotuumiza. Kila siku unatamani na kusubiri aliyekuumiza akwambie samahani, pole, sitakuumiza tena. Nafsi yako ipate furaha na amani.
Kuna watu wamefanya maamuzi magumu, hata kujiumiza zaidi katika miili yao au kujitoa uhai kwa sababu ya kushindwa kuvumilia na kuyashinda maumivu yaliyosababishwa na wanaowapenda sana. Katika somo hili utajifunza kupokea maumivu kutoka mtu yoyote na namna ya kuyakabili maumivu hayo ili kuepuka madhara yanayoweza kusababishwa na maumivu hayo ikiwemo kuchanganyikiwa akili au kujitoa uhai.

Mtu yoyote anaweza kukuumiza nafsi
Tunawaamini sana wanadamu wenzetu, kiasi kwamba hatudhani kama wanaweza kutusababishia maumivu makubwa na yenye madhara kwetu. Tunadhani, endapo tutawatendea wema nao wataturudishia wema na kumbe sivyo, wanaweza kutulipa ubaya wenye kuumiza zaidi. Kuna mtu alisema, “wewe kutomla simba haimaanishi simba kutokukula wewe” au “not eating a lion doesn’t mean a lion won’t eat you”. Kutowatendea mabaya tunaowapenda haimaanishi wao pia hawatatutendea sisi mabaya katika hatua moja au nyingine ya maisha yao. Ukweli huu ndio unaotufanya tuumizwe sana endapo tunaowapenda watatutenda ubaya, kwa sababu hatutegemei kupokea mabaya kutoka kwao. Kuna watu wameumizwa hata wakasema hawata samehe kamwe kwa sababu tu waliowaumiza ni waliowapenda zaidi. Kusamehe ni lazima. Ufundishe moyo wako kutegemea chochote; ubaya au wema kutoka kwa yoyote. Anayetuwazia na kutupatia mema siku zote za uhai wetu ni Mungu pekee.

Mara baada ya kuumizwa na uliyempenda sana, samehe kwa dhati
Hakuna mwanadamu aliyemkamilifu kwa namna moja au nyingine, sote tuna mapungufu isipokuwa Mungu pekee. Katika maisha yetu ya kila siku, mtu mmoja anaweza kummumiza mtu mwingine kwa kutokukusudia au kwa kukusudia. Baada ya kusababisha maumivu anaweza kuomba msamaha au hata asiombe msamaha tena kwa makusudi hasa kama akitambua aliyekuumiza huwezi kumuumiza kwa kulipa kisasi (makusudi) au bahati mbaya. Uambie moyo wako usamehe na kuachilia mzigo wa hasira na maumivu uliyoyabeba. Tunaposamehe ni kwa faida yetu kwanza, Waefeso 4:31-32 na Mathayo 6:14-15 (tunajiponya nafsi na kupata kibali cha msahama mbele za Mungu) na faida ya tunaowasamehe. Ndio, faida ya tunaowasamehe. Wapo wasioweza (wanaokosa ujasiri) kuomba msamaha kwa sababu wao pia huumia mara baada ya kuona wamewaumiza wanaowapenda sana.

Usitake kujua sababu ya kuumizwa kwako
Wanadamu wengi tunapenda kujua sababu ya kuumizwa kwetu tukidhani itasaidia kutoumizwa tena. Lakini nikufahamishe, wengi wanaotuumiza huwa hawana sababu madhubuti za kutuumiza, na endapo tutahitaji kujua sababu, hawataweza kutupatia sababu madhubuti vile vile. Hivyo, siyo muhimu kujua sababu ya kuumizwa zaidi ya kusamehe na kuachilia.

Usilipe kisasi
Usiwe na tabia ya kulipa kisasi kwa waliokutendea ubaya. Kulipa kisasi ni kuumia zaidi, hasa utakapotambua aliyekuumiza hakukusudia kufanya hivyo. Nafsi yako itakuwa imeumia mara mbili kwa kuiumiza nafsi isiyo na hatia. Moyo wako utajaa chuki na hasira dhidi yako binafsi. Hasira au chuki binafsi “self denial” ina madhara makubwa sana. Idadi kubwa ya wanadamu wanojitoa uhai wanakuwa chini ya utawala wa hii roho chafu “self denial”. Mungu anatuagiza tusilipe kisasi, kwa sababu kisasi ni chake (Warumi 12:19 na Mithali 24:29) na siyo chetu.

Waombee na kuwapenda wanaokutenda ubaya
Hili ni agizo la Mungu (1 Petro 3:9), tuwaombee na kuwapenda wanaotutenda ubaya. Hii ni kwa sabau kubwa mbili, moja; Mungu hutubariki na kutuinua na pili; huwafanya waliotutenda ubaya kujifunza wema wa Mungu kupitia maisha yetu. Tunapowaombea waliotuudhi tunainuliwa kiimani, waombe heri na siyo laana. Pia Mungu huachilia baraka zake kwetu maradufu zaidi ya tuombavyo, kwa sababu huonesha roho, moyo na nafsi iliyopondeka na kunyenyekea mbele za Mungu zaidi ya maumivu tuliyonayo mioyoni. Tunapowalipa mema waliotutenda ubaya, inawapa fundisho la kuuona wema wa Mungu kupitia maisha yetu. Inakufanya ufanyike baraka kwa wote, wema na waovu kwako, hii ni tabia halisi ya Mungu, huwanyeshea mvua wema na waovu.

Dumu katika sala na maombi, ni nguzo madhubuti ya kuishi maisha yenye amani, furaha na upendo. Amina.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts