Sunday, May 18, 2014

NAMNA UNAVYOPITA KATIKA JARIBU NDIYO KUNAAMUA NAMNA YA USHINDI UTAKAOUTA



Maana na makusudi ya kujaribiwa
 Jaribu linasemekana kuwa ni mtaji wa kuinua imani ya mtu anayejaribiwa, lakini binafsi ninapenda kuirekebisha sentensi hii. Jaribu ni mtaji wa kuinua imani ya anayeshinda jaribu; kama umejaribiwa na jaribu likakuangusha, siyo sahihi kusema jaribu hilo lililokuangusha lilikuwa mtaji wa kuinua imani yako. Imani ipi? Kama umeshindwa kuitetea imani yako na kuangushwa, jaribu halikuwa mtaji kwako. 

Jaribu huja na makusudi mawili; moja, ni kumuimarisha kiroho na kuinua imani ya anayejaribiwa na kushinda jaribu. Pili, ni kumuangusha mtakatifu na kuharibu uhusiano wake na Mungu. Na mara nyingine jaribu au teso huwa ni kiboko cha Mungu cha kulirudi kanisa lake. Ninaposema kanisa ninamaanisha Mkristo.

Kuinua imani ya Mkristo. Nikupe mfano kwanza, kuna hekima ya Kimungu na hekima ya kibinadamu.  Hekima ya Kimungu hupewa mtu yoyote pasipo kujari umri, na hii huletwa na Yesu Kristo mwenyewe. Na hekima ya kibinadamu huja kutokana na uzoefu wa muda mrefu alionao mtu katika jambo fulani, na hekima hii wanayo wazee. Na imani ndivyo ilivyo, ili ikue ni lazima ipitishwe katika kujaribiwa, ipitishwe katika vitu ambavyo sayansi na akili ya kibinadamu haviwezekani. Ukiisha pita hapo kwa msaada wa Mungu kwa jina la Yesu Kristo ndipo imani yako inapokuwa. Ndipo unapozidisha imani na uhusiano wako na Mungu kupitia Yesu Kristo (Yohana 11:3-4, 14-15 na 1 Petro 1:6-7)

Kumuangusha mtakatifu. Hili ni jaribu linalosababishwa na shetani moja kwa moja, na makusudi yake huwa ni kumuangusha mtakatifu ili kuharibu na kufuta kabisa uhusiano wake na Mungu. Kwa mfano, Ayubu hakujaribiwa ili kuinua imani yake au kurudiwa na Mungu, alijaribiwa ili amkufuru Mungu, kwa Kiswahili chepesi ni ili avunje uhusiano wake na Mungu. Kwa hiyo kuna wakati shetani huwajaribu Wakristo ili awafarakanishe na Mungu (Yohana 2:10, Ayubu 2:4-5)

Kurudiwa na Mungu. Hapa naomba nieleweke, hili kwa upande mmoja siyo jaribu na kwa upande mwingine ni jaribu. Nina maana gani; kwa upande wa Mungu ni kiboko cha kulirudi kanisa lake kama ilivyo kwa mzazi anapomuadhibu mtoto aliyekosea. Kwa upande wa Mkristo, analiona kama jaribu. Na hili hutupata ikiwa tumekengeuka na kuiacha njia ya haki, tumemkosea Mungu. Na tukitubu na kuirudia njia ya haki, utaona mateso yote yanaondoka pia (Mithali 3:11-12, Ayubu 5:17)

Nini cha kufanya uwapo katika jaribu
Kuna makosa makubwa mawili ambayo Wakristo wengi tunayafanya tuwapo katika majaribu. Na makosa haya ndiyo yanayogharimu uhusiano wetu na kutufarakanisha na Mungu. Makosa hayo ndiyo yanayofanya tunaangushwa na majaribu.

Kosa la kwanza; tunatumia akili zetu kutafuta ufumbuzi wa jinsi gani tutavuka jaribu tunalopitia kwa ushindi na kumuacha Mungu kando ambayo ndiye msaada wetu. Hapa ni lazima uelewe, Mungu pekee ndiye anayetushindia majaribu, kwa akili zetu na nguvu zetu na maarifa yetu hatuwezi kamwe kujinasua katika majaribu. Uwapo katika jaribu ni lazima umkabidhi Mungu njia zako na jaribu lako, Yeye ndiye ushindi wako kwa Jina la Yesu Kristo (2 Petro 2:9, Zaburi 37:5)

Kosa la pili; kuwaangalia wanadamu wanafanya nini na wanasema nini tunapopita katika jaribu hasa wapendwa au wakristo wenzetu. Kitu tunachojisahau hapa ni kwamba tunategemea wingi wa marafiki tunaokuwa nao wakati wa furaha ndio hao hao tutakao kuwa nao wakati wa majaribu, sivyo! Uwapo katika shida au jaribu kama kuna mkristo mwenzako atabaki na wewe hiyo ni neema tu ya Mungu, lakini wengi kama siyo wote watakuacha peke yako.

Unajua kwa nini watakuacha peke yako? Jaribu siyo lao ni lako, anayepaswa kushinda siyo weo ni wewe. Kwa hiyo ni lazima upite peke yako ili ushinde peke yako na tuzo ya ushindi utapata peke yako. Hupaswi kuwaangalia wapendwa na hupaswi kulalamika iwapo watakuacha upite katika jaribu peke yako.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts