Monday, December 24, 2012

X-MAS SIYO CHRISTMAS.

Ni jambo la kawaida kwa wa-Kristo wengi kuchukulia mambo katika hali ya kawaida pasipo kuchunguza uwepo na/au makusudi ya jambo au mambo hayo. Mfano mzuri na ndiyo ukweli halisi ni matumizi ya neno ‘X-mas’, ‘X-MAS’ au ‘Xmas’. Hilo ni neno moja isipokuwa ni tofauti ya matumizi ya herufi; herufi kubwa au herufi ndogo, lakini neno hilo linatumika kuwakirisha neno ‘Christmas’.

Mimi pia nilikuwa ni mmoja wa watumiaji wa neno hilo la kifupi (Xmas) kuwakilisha neno Christmas, inawezekana unalitumia neno hilo pasipo kujua unamaanisha nini au unalitumia kwa sababu unafikiri unaokoa wakati kwa kuiandika Christmas kwa neno fupi. Asante kwa dada yangu aliyenifumbua macho na kunifanya nilifuatilie neno hilo haraka sana.

Ukweli ni kwamba, X inawakilisha thamani, namba au kitu kisichojulikana katika hisabati (mathematics), na ukiliangalia neno Christ-mas na X-mas utapata kutambua kuwa herufi X inawakilisha neno Christ. Na kama X ni thamani, namba au kitu kisichojulikana katika hisabati (mathematics) na kwetu wa-Kristo, je ni halali kuitumia herufi isiyojulikana thamani yake kumuwakilisha Kristo? Kwamba hatumjui au hatuijui thamani ya Kristo?

Funguka macho, acha uvivu, hakikisha unaandika neno kamili, “Christmas”, tena linaandikwa kwa kuanza na herufi kubwa ‘C’.

Na jambo la pili nililojifunza ni kumtumia “Santa Claus” katika kipindi hiki cha kumbukumbu ya kuzaliwa Yesu Kristo badala ya kumuadhimisha Yesu Kristo mwenyewe. Labda ni kwa sababu tunahamasisha kupeana zawadi, lakini ukweli ni kwamba tunapaswa tumtamke Yesu Kristo ambaye ni zawadi tosha maishani mwetu.

Na jambo la mwisho kwa leo ni jinsi wa-Kristo wengi tunavyosherehekea msimu huu wa sikukuu ya “Christmas” na mwaka mpya. Tunasherehekea tofauti na inavyotupasa tuisherehekee, tunasherehekea kwa matendo ya anasa na kujisahau, tumekuwa sawa na watoto wanaofurahi kufika kwa kipindi hiki kwa sababu watanunuliwa nguo mpya na kula chakula kizuri. 

Katika kipindi hiki tunapaswa kufanya tafakari ya mwaka mzima katika mambo makuu manne; imani, uchumi, jamii, kurekebisha. 

Imani: je, wewe mKristo umeitunza na kuitetea imani yako pasipo kumtenda Mungu dhambi kwa kipindi chote cha mwaka unaoumaliza?

Uchumi: je, umepiga hatua kiuchumi kama ulivyopanga na/au kutegemea wakati unaanza mwaka unaoumaliza?

Jamii: je, uhusiano wako na jamii unayoishi nayo unakuwa mzuri au unaharibika? Kama una familia, je familia yako inapata mahitaji muhimu na yale ya ziada kutoka kwako?

Rekebisha: hiki ni kipindi cha kutambua makosa, mapungufu na kufanya tathmini kwa ujumla. Jitahidi kutambua ni wapi ulipokwama na tafuta ufumbuzi ili usonge mbele na inapohitajika ushari, tafuta ushauri kwa watu wanaoweza kukusaidia, usimwambie kila mtu mapungufu yako. Zaidi mtegemee Mungu. 

Mwisho kabisa, ni lazima umshukuru Mungu; wewe umefika mwishoni mwa mwaka lakini yupo aliyepoteza uhai mwanzoni mwa mwaka, wewe umejenga nyumba japo ndogo lakini yupo ambaye analala kibarazani mwa duka la mtu, wewe ulilala njaa usiku mmoja lakini yupo aliyelala na kushinda njaa kwa zaidi ya siku tatu, wewe unaishi katika nchi yenye amani lakini yupo anayeishi katikati ya vita, wewe upo huru japokuwa huna kitu lakini yupo asiye na kitu kama wewe amesingiziwa kesi na kufungwa jela. Huna sababu ya kukwepa kumshukuru Mungu.

 "NAWATAKIENI KHERI YA 'CHRISTMAS' NA FURAHA YA MWAKA MPYA, 2013"

Sunday, December 16, 2012

KANUNI ZA KUISHI MAISHA YA USHINDI NA BARAKA.



   Kila jambo analokutana nalo mwanadamu lina sababu ya kuwepo, na kuna nguvu inayolishikilia hilo jambo liendelee kuwepo. Endapo hiyo nguvu itakatwa, basi hilo jambo haliwezi kuendelea kuwepo. Na uwepo wa nguvu unaosababisha mambo kutendeka unategemea kanuni; ili usipate magonjwa ya kuambukiza, zipo kanuni za kujiepusha na magonjwa hayo.

   Na katika mambo ya rohoni, kuna kanuni za kuyapata hayo mambo ya rohoni; ili ubarikiwe, ule matunda ya kazi za mikono yako na upokee uponyaji ni lazima uzingatie kanuni. Na kanuni hizo ni; uwe mnyenyekevu kwa Mungu, na unyenyekevu huo uambatane na maombi, maombi yaliyokusudia kuutafuta na kuuona uso wa Mungu, na ili uweze kuuona uso wa Mungu ni lazima uachane na njia zote mbaya.

2 Nyakati 17:13-14 “Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi, au nikiwapelekea watu wangu tauni; ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao”.

   Hapa neno mvua linabeba maana mbili; mvua kwa maana ya mvua, na mvua kama baraka. Na katika baadhi ya vitabu vitakatifu vya Biblia, Mungu analithibitisha hilo; (Isaya 30:23 Naye atatoa mvua juu ya mbegu zako, upate kuipanda nchi hii; na mkate wa mazao ya nchi, nayo itasitawi na kuzaa tele; katika siku hiyo ng’ombe zako watakula katika malisho mapana), mvua kama baraka- Malaki 3:10 “. . . mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la”.

Kwa hiyo, mbingu zikifungwa kusiwe na mvua; mvua kama mvua inaweza isinyeshe na mvua kama baraka inaweza pia isipatikane. Na ukikosa baraka, basi una laana; inaweza ikawa ni laana ya ukoo, laana ya kutamkiwa (Mithali 11:26, 24:24,) au ya kujitamkia kwa kujua au pasipo kujua, au laana inayotokana na kutenda dhambi (Kumbukumbu la torati 28:15, Malaki 2:2, Zaburi 119:21).

   Nzige kula nchi; nzige hula mimea au mazao yaliyootayo juu ya nchi, wanapokula mazao hula chakula cha binadamu (Zaburi 105:34-35 “Alisema, kukaja nzige na tunutu wasiohesabika wakaila miche yote ya nchi yao, wakayala matunda ya ardhi yao”). 

Unaweza kuwa na huduma iliyodumaa au imekufa kabisa, unafanya kazi lakini huli matunda stahili ya kazi yako au wewe ni mkulima lakini mavuno ni hafifu. Katika hali hizo, nzige wamekula nchi, ni lazima ufanye jambo kuikomboa nchi hiyo; kuinua au kufufua huduma yako, kunufaika na kazi ya mikono yako na hata kupata mavuno bora ya mashamba yako. Jambo hili linaweza kusababishwa na nguvu  za ufalme wa giza au maisha ya dhambi (Zaburi 119:21), lakini unaweza kujikomboa katika utumwa huo, zingatia kanuni.

   Tauni; neno hili linawakilisha magonjwa, ambayo yanaweza hata kuondoa uhai au kukuacha na ulemavu. Magonjwa yasiyo na tiba au magonjwa yasiyoeleweka yanasababishwa na nini, na inaweza ikawa ni malipo ya dhambi (Ayubu 8:3-4, 2 Samweli 24:15) au ni kuonewa na shetani. Lakini hayo yote yanaweza kukuachilia huru tangu sasa, ikiwa yamekupata wewe au ndugu yako, Mungu ni mwaminifu hakuwahi kusema uongo hata leo asema uongo.

Katika mambo hayo matatu; kukosa mvua, nzige kula nchi na tauni, inawezekana ukawa umepitia jambo moja wapo au yote kwa jinsi tulivyoyaona maana zake katika mwaka huu (2012) unaomalizika hivi karibuni. Na hungependa kuingia na kutembea na mwaka unaofuata (2013) na mambo hayo, unatamani kufunguliwa na kuwekwa huru; upokee baraka kutoka kwa Mungu, kuinua na kufufua huduma yako, kula matunda ya kazi za mikono yako na kuishi maisha yasiyojua ugonjwa/magonjwa, INAWEZEKANA! Zipo kanuni alizoziweka Mungu mwenyewe ili tupone, zingatia kanuni hizo. Kanuni hizo ni:-

   Kunyenyekea; ni kutii na kukubali sauti ya Mungu na kufanya yanayoelekezwa na sauti hiyo (Isaya 1:19 “. . . mkikubali na kutii, mtakula mema ya nchi”). Sauti ya Mungu siku zote inatuelekeza kuifuata njia njema, na kuifuata njia njema ni kuchagua mema; baraka, uponyaji, ushindi, heshima, kuinuliwa na mengine mengi mazuri. Kunyenyekea kunamfanya Mungu atumie muda wa ziada kututegea sikio na kuyasikiliza maombi yetu, na Mungu akiyasikiliza maombi yetu lazima tuwe na uhakika wa kupokea majibu (Danieli 12:10, Isaya 66:2). 

Kutonyenyekea kunainua hasira ya Mungu juu ya wanadamu, na ndipo tunapatwa na mabaya (Yeremia 44:10). Kwa hiyo hii ni kanuni ya kwanza, ukitaka kuwa rafiki wa Mungu na kupokea mema kutoka kwake, lazima unyenyekee.

   Kuomba; ni njia ya mwanadamu kuzungumza na Mungu (Isaya 1:18 “. . . haya njooni tusemezane. . .”), Mungu anaposema ‘njooni tusemezane’ anatufundisha kuomba ili tupeleke mahitaji yetu kwake na yeye atujibu kulingana natulivyoomba au tunavyostahili (Yakobo 5:13). 

Kuomba ni kanuni ya pili, ambayo ni lazima iambatane na kanuni ya kwanza (unyenyekevu), huwezi kuwa muombaji kama hunyenyekei. Unyenyekevu unakupa haki mbele za Mungu, na maombi ya mwenye haki ndiyo yanayofaa sana (Yakobo 5:16 kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii). Na hii ni kanuni ya pili.

   Kuutafuta uso wa Mungu; kama tulivyoona, hizi kanuni zina mfuatano wa kutegemeana, unapokuwa mnyenyekevu na muombaji ni rahisi sana kukutana na Mungu. Unapoomba hakikisha umekutana (umekuwa-connected) na Mungu na ndipo ueleze mahitaji yako. Jambo hili si jepesi, unahitaji kujitoa na kudhamiria; kuwa mnyenyekevu na muombaji na ndipo utakapokutana na Mungu (Mithali 8:17 . . . na wale wanitafutao kwa bidii wataniona. Yeremia 29:13 . . .nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote). Kanuni ya tatu.

Kuacha njia mbaya; ni kurudi kutoka dhambini na kumrejea Mungu. Unyenyekevu, maombi na kuutafuta uso wa Mungu ni lazima viambatane na toba, kila unaposogea mbele za Mungu hakikisha unajitakasa hata kama hukumbuki kumtenda Mungu dhambi (Hosea 5:15 . . . hata watakapoungama makosa yao na kunitafuta uso wangu. . .). Ukiamua kuacha njia mbaya, usijiweke tena katika mazingira ya kuirudia hiyo njia mbaya; epukana na mazingira ya kutenda dhambi kwa kuangalia, kusikiliza au kuongea (Yeremia 36:7 na kurudi, kila mtu akiiacha njia yake mbaya. Yeremia 35:15 rudini sasa, kila mtu na aiache njia yake mbaya, mkatengeneze matendo yenu). Na siyo utende dhambi makusudi kwa kuwa utaomba toba!! Kanuni ya nne.

Ni wewe mwenyewe, unayeweza kuamua na kujitoa kutoka katika maisha ya mateso na kuonewa na yule mwovu. Zingatia kufuata, kutenda na kuzitimiza kanuni, amua leo kuingia mwaka mpya na maisha mapya. Mungu akubariki sana, kwa jina la Yesu Kristo.

Unahitaji kuokoka? Bonyeza hapa.

Friday, December 7, 2012

NJIA UTAKAYOICHAGUA NDIYO NJIA UTAKAYOPITA.

   Mwanadamu wa kwanza aliumbwa katika ukamilifu; kiroho na kimwili, mtakatifu asiyejua dhambi na mwenye mwili usioonja mauti. Baada ya kuasi agizo la Mungu na kutenda dhambi, akapoteza ukamiliu wa utakatifu, lakini kwa vile Mungu ni pendo, anatupenda wanadamu akatuandalia ukombozi ili atununue kutoka katika ufalme wa giza na kutuingiza katika Ufalme wa Mwana wa pendo lake, Yesu Kristo.

   Lakini kuupokea ukombozi huo, ni hiyari ya mwanadamu mwenyewe, kwani baada ya kuitambua dhambi mwanadamu huyu alipata utashi wa kutambua wema na uovu (Mwanzo 3:7).
Kumbukumbu la Torati 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimeweka mbele yako uzima na mauti… basi chagua uzima ili uwe hai, wewe na uzao wako”.
Yeremia 21:8 “Nawe waambie watu hawa, Bwana asema hivi, tazama naweka mbele yenu njia ya uzima na njia ya mauti”.

   Katika kitabu cha Torati, Mungu anaapa (anazishuhudiza) kwa mbingu na nchi kuwa ametuwekea wanadamu njia mbili mbele yetu, ambazo ni uzima na mauti. Na kwa sababu Mungu ni pendo, anatushauri kuichagua njia ya uzima.

   Na siyo anatushauri tu, pia anatupa na sababu ya kwanini anatushauri kuchagua uzima, anasema ili uwe hai. Kuwa hai ni kupokea uzima wa milele, baada ya hukumu yenye kutisha ya Mungu yenye haki, siku atakapo tuhukumu wanadamu sawa sawa na matendo yetu.
Na katika kitabu cha Yeremia, Mungu anarithibitisha neno lake kuwa ameweka njia mbili mbele yetu; moja ni njia itupayo uzima na nyingine ni njia ya mauti. Ni juu yetu kuamua tunachagua na kuifuata njia ipi.

   Kuchagua njia ya uzima ni lazima kwanza uifahamu hiyo njia, ni ipi na unawezaje kuichagua na kuifuata. Njia ya uzima ni Yesu Kristo, kuchagua njia ya uzima ni kumchagua na kumpokea Yesu Kristo kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako. Na kuifuata njia ya uzima ni kutimiza na kutenda mapenzi ya neno la Mungu, kufuata na kushika neno la Yesu mwenyewe kwa matendo dhahiri.

Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba ila kwa njia ya mimi”.

   Ile njia ya uzima ambayo Mungu aliziapia mbingu na nchi kuwa ameiweka mbele yetu na kutushauri kuichagua na kuifuata hiyo, ndiyo hiyo inafunuliwa katika kitabu cha Yohana Mtakatifu. Yesu mwenyewe anajidhihirisha kuwa yeye ndiye njia, na siyo njia tu, ina uzima ndani yake amboyo kupitia hiyo tunaurithi Ufalme wa Mungu.

   Kuchagua njia ya uzima kunapaswa kuendane na matendo ya uzima, tusikiri kwa maneno ya vinywa vyetu kuwa tunao uzima (tumempokea Yesu Kristo) na wakati huo huo matendo yetu ni kinyume na kukiri kwetu.

Mathayo 3:8 “Basi zaeni matunda yapasayo toba”, matunda ni matendo na toba ni kuupokea uzima, sasa matendo yetu yanapaswa kuenenda kama jinsi tulivyoupokea huo uzima.
Cha kushangaza, Wakristo wengi wa siku hizi wanatenda kinyume na wanavyokiri katika vinywa vyao. Na kusababisha jina la Mungu litukanwe.

Tito 1:16 “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana”, kukiri kuwa umempokea Yesu Kristo na unahudhuria katika nyumba za ibada lakini matendo yako ni kinyume na kukiri kwako ni sawa na kupoteza muda!

   Kuchagua njia ya uzima na kutoifuata kwa matendo njia hiyo kunamadhara yafuatayo;

Kulitukanisha jina la Yesu; watu wanapoyatazama matendo yetu wanategemea kuona maisha yetu yakiakisi maisha halisi ya Yesu Kristo, na inapokuwa tofauti ndipo jina la Yesu linapotukanwa (2 Petro 2:2).

Kurithi mauti na kuzimu; kutotembea katika njia ya uzima ni kutembea katika njia ya mauti, na kutembea katika njia ya mauti ni kuchagua mauti (Mithali 12:28, 15:24).

Njia utakayopita katika uhai wako ndiyo njia utakayo iendea baada ya kifo, ikiwa umechagua njia ya uzima lakini unapita katika njia ya uovu basi baada ya kifo pia utaiendea njia uliyokuwa ukiipitia. Hapa haijarishi ni dua, swala au maombi mengi kiasi gani utafanyiwa wakati wa mazishi yako.

 Unachochagua kuishi ndicho utakacho tunukiwa.
Mathayo 16:27 “… ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake”, kila mmoja wetu atalipwa kwa kadiri ya alivyotenda alipokuwa hai na siyo kwa kadiri ya sala za kumuombea awekwe pema peponi (Yohana 5:28-29).

Kama umechagua njia ya uzima, tembea katika njia ya uzima maisha yako yote kwa uaminifu.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts