Wednesday, December 25, 2019

SALAMU ZA KRISMASI NA MWAKA MPYA 2020

Salamu!

Krismasi ni nini na inapaswa kusherehekewa kwa namna gani?
Kumekuwa na mafundisho mengi sana kutoka kwa wapinga dini (atheists) na wenye dini tofauti na Ukristo kuhusu siku ya Krismasi. Mafundisho yao mengi yamekuwa ni kinyume na sherehe hii. Baadhi wamekuwa wakidai hakuna sehemu katika Biblia inayoturuhusu Wakristo kusherehekea Krismasi kama tunavyofanya. Na baadhi ya mafundisho yamediriki hata kusema hakuna mitume (watangulizi wetu wa Kanisa) waliowai kusherehekea sherehe hii.

Maswali tunayopaswa kujiuliza kabla hatujakubali kuyumbishwa na mafundisho haya ni:-
Kwanini malaika walikwenda kuwapasha habari za kuzaliwa kwake Yesu Kristo wachungaji usiku ule alipozaliwa?
Kwanini malaika alipowapasha habari wachungaji aliwaambia “I bring you good news of great joy” akimaanisha “habari njema zenye furaha kuu”?
Kwanini mamajusi na wachungaji walibeba zawadi (manemane, uvumba na mar’hamu) kumpelekea mototo Yesu?
Maswali hayo yanapatikana katika vitabu vitakatifu vya Biblia, Mathayo sura ya kwanza na ya pili pamoja na Luka sura ya kwanza. 

Inawezekana ndiyo Biblia haisemi chochote kuhusu sherehe za Krismasi lakini pia haijatukataza kusherehekea Krismasi. Na ikiwa walioshuhudiwa kuzaliwa kwa Yesu Kristo (mamajusi na wachungaji) walijawa na furaha na hata wakampelekea zawadi kwa nini sisi tusifanye sasa? Kwanini malaika alifanya kazi ya kuwapasha habari wachungaji kama kuzaliwa kwa Yesu Kristo halikuwa jambo linalostahili kusherehekewa?

Tarehe na majira sahihi ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo bado ni kitendawili katika maandiko mengi ya Kikristo na hata dini nyingine zinazomtambua Yesu Kristo. Tarehe 25 ya kila mwezi wa 12 wa mwaka ilibuniwa tu kwa sababu ya ufanano wa majira ya kuzaliwa halisi kwa Yesu Kristo na majira ya sehemu mbali mbali duniani. Kwa mujibu wa Teolojia, wakati wa kuzaliwa Yesu Kristo yalikuwa ni majira ya baridi na kuanguka kwa barafu katika nchi za ulaya na ndiyo sababu mwezi wa 12 kwa kila mwaka ukachaguliwa kuwa mwezi maalumu wa sherehe za Krismasi. 

Lakini ni namna gani tunapaswa kuisherehekea Krismasi? Krismasi siyo sherehe ya “birthday” kama inavyodhaniwa na watu wengi na hipaswi kusherehekewa kama sherehe za “birthday” zetu tunazozisherehekea mara moja kila mwaka. 

Krismasi ni sherehe ya kukubali kulipokea pendo la ukombozi wa mwanadamu anayepotea katika dhambi kupitia Yesu Kristo ambaye ni Bwana na Mwokozi wetu. Mwanzo wa pendo hili ni kuzaliwa kwa Mwokozi huyu, Yesu Kristo, na mwisho wa kukamilika kwa pendo hilo ni katika safari ya msalaba. Kupitia kifo cha msalaba, dhambi zetu zinatakaswa kwa damu yenye mamlaka ya Yesu Kristo. Na katika ufufuo wa Yesu Kristo tunakamilishwa na kufanywa wana wa Mungu tunaoubeba ushindi wa baba yetu manegani mwetu. Ushindi dhidi ya mateso, dhiki, mauti, magonjwa na shida zote katika dunia hii huku tukiwa na tumaini la wokovu na uzima wa milele pamoja na Bwana wetu. 

Hivyo basi, tunapaswa kuiona siku ya Krismasi kama pendo la Mungu kwetu wanadamu na hivyo kuisherehekea kwa nguvu zote kwa sababu tumekubali kulipokea pendo hilo na kufanyika wana wa Mungu. Mungu ameachilia pendo lake kwa wanadamu wote lakini siyo wote waliokubali kupendwa na wakapenda. Sisi tuliokubali kupendwa na tumependa hatuna budi kuisherehekea siku hii ya Krismasi.

Tunawatakia Krismasi njema, pendo la Mungu la zidumu ndani yetu zaidi tukifanyika baraka kwa wanadamu wenzetu ili wamuone Mungu kupitia maisha yetu. Amina.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts