Thursday, May 24, 2018

NGUVU YA MWANAMKE AOMBAYE


Nakusalimu mpendwa katika Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo

Utangulizi
Siku ya leo, Mungu anatufundisha somo lenye kichwa, “Nguvu ya mwanamke aombaye”. Ni maombi yangu Mungu afungue ufahamu na uelewa wako ili tunapokwenda kumaliza somo letu la leo, kuwe kuna kitu kipya kimejengeka na kuimarika katika fahamu zetu. Kitu ambacho hakitatuacha kubaki kama tulivyokuwa mwanzo, wote wanaume kwa wanawake. Wanaume tutajifunza nguvu walizonazo wanawake katika ulimwengu wa kiroho na namna Mungu anavyothamini, sikiliza na kujibu maombi yao. Wanawake watajifunza nguvu waliyonayo ndani ya Yesu Kristo, kupitia nguvu hiyo watavikwa utu mpya wa kujithamini na kufanya mambo makubwa katika ulimwengu wa roho na ulimwengu wa macho ya damu na nyama. 

Jamii karibu zote ulimwenguni zimemchukulia mwanamke kama kiumbe duni na dhaifu, kiumbe kinachostahili kutendewa ubaya wowote. Na hivyo ndivyo mwanamke alivyoaminishwa kuwa na kujichukulia. Katika kujikomboa kutoka dhana nzima ya mfumo dume, mwanamke anafanya kampeni za kutafuta haki sawa na mwanaume. Kutafuta haki sawa kati ya mwanamke na mwanaume siyo suluhu sahihi ya kumkwamua mwanamke. Suluhu sahihi ni mwanamke kuitambua nafasi yake mbele za Mungu na namna Mungu alivyomthamini mwanamke tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu. Pili, mwanamke kutambua wajibu wake sahihi kwa mwanaume. Tatu, mwanaume atambue nafasi ya mwanamke katika kumuimarisha maisha yake ya kiroho, kijamii na kiuchumi. 

Mwanamke ni nani?
“Bwana analitoa neno lake (na kusema), wanawake watangazao habari ni jeshi kubwa”, Zaburi 68:11. Kwa mujibu wa Biblia takatifu, kutangaza habari ni kulihuburi neno la Mungu au Yesu Kristo. Habari njema za Yesu Kristo zinatangazwa mahali kote, sehemu yoyote na wakati wowote. Asilimia kubwa ya wanawake, asiyeko na aliyeko ndani ya ndoa ni mtangaza habari njema za Mungu na Yesu Kristo, wengine pasipo hata wao wenyewe kujua. Ndiyo, unaweza kuwa unatangaza habari njema za Mungu na Yesu Kristo pasipo kujijua. Twende pamoja sasa kumtambua mwanamke ni nani kupitia 4M; msaidizi, mzazi, mlezi na mlinzi. Kupitia 4M utatatmbua namna mwanamke anavyoweza kutangaza habari njema za ufalme wa Mungu. 

Msaidizi
Mwanzo 2:20b na 18, “…..lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye. Bwana Mungu akasema, si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye”. Mwanamke ni msaidizi wa mwanaume, siyo msaidizi tu, ni msaidizi wa kufanana na mwanaume. Kufanana maana yake ni kuwa na viwango vinavyokaribiana katika ubora na nafasi. Fundi ujenzi wa nyumba hawezi kutafuta msaidizi mwenye ujuzi wa kutengeneza magari, ni lazima atatafuta msaidizi mwenye uwezo wa ujenzi wa nyumba. Hivyo basi mwanamke ni sawa na mwanaume mbele za macho ya Mungu. Hakuna aliye bora zaidi ya mwingine, si mwanume wala si mwanamke. Mbele za macho ya Mungu, sote tuna nafasi sawa. Mwanamke jithaminishe sawa na mwanaume, ndivyo Mungu anavyotuona. Mwanaume mthamini mwanamke kwa maana ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu (Mwanzo 1:26). Ukimuona mwanamke, ona utukufu wa uumbaji wa Mungu sawa na ule unaouona kwako. Siku zote za maisha yako mwanamke fanya majukumu yako kwa mwanaume ukimpendeza Mungu, hii ndiyo injili sahihi ikupasayo kuliko hata ile ya madhabahuni ilihali hautimizi wajibu wako kwa mumeo impendezavyo Mungu. 

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts