Saturday, June 22, 2013

MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU. (SEHEMU YA KWANZA).



YESU KRISTO ASIFIWE!

Mpendwa msomaji wangu, siku ya leo tunaanza semina yetu ya mtandaoni ambayo tutatembea nayo kwa muda wa wiki zisizopungua tatu. Tafadhari jitahidi usikose sehemu hata moja ya somo letu lenye kichwa kisemacho “MAOMBI YENYE KIBALI NA NGUVU MBELE ZA MUNGU”.

Katika kipindi hiki cha semina hii tutakuwa tukiangalia maombi kwa jicho la tofauti, na ninakusihi ndugu msomaji wangu tegemea kukuta na Mungu katika kipindi hiki. Mungu mwenyewe atakwenda kukuhudumia, na hakika utapokea kitu kipya.

Kufikia kumalizika kwa somo hili tutakuwa tumejifunza vitu vifuatavyo:-

1. Maana ya maombi. 

2. Faida za maombi.

3. Vitu vya kuzingatia uwapo katika maombi. 

4. Aina kuu za maombi na faida zake.
  •      Maombi kabla.
  •      Maombi baada. 
  •         Maombi ya kawaida.
  •      Maombi ya kufunga.
5. Aina za maombi.


  • Maombi ya Roho Mtakatifu.
  • Maombi ya kufunga na kufungua.
  • Maombi ya kusukuma.
  • Maombi kwa adui.
  •  Maombi ya ushirika.
  •  Maombi kwa wengine.
  •  Maombi ya sifa.
  •  Maombi ya shukrani.

6    6. Kuomba kwa kuzitaja ahadi za Mungu na sababu za kuomba kwa kuzitaja ahadi za Mungu.



 Maana ya maombi.

Ni hitaji au tamanio la moyo wa mwanadamu ambalo yeye mwenyewe hawezi kujitosheleza, hivyo basi anahitaji msaada kutoka nje. Maombi ni moja ya silaha yenye nguvu sana katika ulimwengu wa roho; silaha inayoweza kuziharibu kazi za shetani, silaha inayoweza kufanya yasiyowezekana yawezekane.

Waefeso 6:11-13. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.

Kama neno la Mungu linavyotuambia, hatushindani kwa damu na nyama; bali tunashindana na falme na mamlaka, wakuu wa giza na majeshi ya pepo wabaya. Moja kwa moja vita hivi havihitaji mwili kama mwili na silaha zionekanazo kwa macho ziingiie kupambana, kwa sababu vitu hivi haviwezi kuingia katika ulimwengu wa roho. Kwa hiyo inahitajika silaha inayoweza kuingia katika ulimwengu wa roho ilihali mpiganaji amevaa mwili wa damu na nyama. Nielewe, wote tunatambua ya kwamba tuna miili ya damu na nyama na wakati huo tuna roho, miili ya damu na nyama itakapokufa tutaishi katika roho, sasa hauhitaji kufa iliueweze kupigana katika ulimwengu wa roho dhidi ya shetani.

Ukiwa bado unaishi na mwili wa damu na nyama, bado unaweza kupigana vita dhidi ya falme za giza na majeshi yake, sasa silaha pekee unayoweza kuitumia ili kupigana vita hiyo, silaha ambayo inapenya katika ulimwengu wa roho na kuharibu kazi za shetani na kuyasulubu na kuyapa kipigo mapepo ni maombi pekee. Silaha nyingine zinakulinda wewe na uvamizi wa ufalme wa giza na majeshi yake, lakini hazikufanyi wewe upigane na ufalme wa giza na kuushinda. Ni maombi peke yake.

Marko 9:28-29. Hata alipoingia nyumbani (YESU KRISTO), wanafunzi wake wakamuuliza kwa faragha, mbona sisi hatukuweza kumtoa (pepo bubu na kiziwi)? Akawaambia, namna hii haiwezi kutoka (vita hii hamuwezi kuipigana) kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba.

Yesu Kristo mwenyewe anatuthibitishia katika mistari ya Biblia hapo juu kwamba, kuna vita nyingine hatuwezi kupigana na kushinda pasipo maombi. Ni lazima tuwe waombaji ili tuweze kuzishinda vita za namna hiyo, vita dhidi ya ulimwengu wa roho.


Vitu vya kuzingatia katika maombi.
  
Kabla hujaingia kufanya maombi na wakati ufanyapo maombi lazima uzingatie mambo yafuatayo;
  • Mahali au sehemu ya kufanyia maombi. Chagua sehemu yenye utulivu, isiyo na kelele na shughuli za wanadamu, ambapo unaweza kumtafakari Mungu na kuongea naye kwa urahisi zaidi. Unapokuwa sehemu yenye kelele na shughuli za wanadamu, ufahamu wako unashindwa kuzama zaidi katika kumtafakari Mungu. Sehemu nzuri unayoweza kufanya maombi kwa utulivu zaidi ni kanisani au mlimani. Ukiangalia mitume wa zamani na watumishi wa Mungu wa sasa wenye nguvu ni wale wanaojitenga na wanadamu wanapotaka kufanya maombi. Mathayo 8:1-2, Mathayo 26:36-39, Luka 6:12, Walawi 25:1, Kutoka 34:1-4.
  •  Muda wa kufanya maombi. Muda mzuri wa kufanya maombi ni wakati wa usiku, kwa sababu ni wakati tulivu na vita vinapiganika kwa ushindi zaidi.
  • Muda wa kudumu katika maombi. Huu ni urefu wa maombi yako; kwa mfano unafanya maombi ya kufunga labda masaa 12 halafu unaomba nusu saa au saa moja kutwa nzima, au unafanya maombi ya masaa 24 halafu unaomba masaa mawili au matatu, hakika hapo huna unachokifanya bali umeamua kushinda njaa, hayo ni maombi ya kawaida. Kama umefunga masaa 12, angalau fanya maombi kwa muda usiopungua masaa manne na kama umefunga masaa 24 angalau ufanye maombi yasiyopungua masaa nane.
  • Utakatifu. Unapoanza kufanya maombi lazima utubu makosa yako yote kwanza ndipo uanze kupeleka hoja zako mbele za madhabahu ya Mungu. Ni lazima utubu kwa sababu Mungu anasema maombi ya wenye dhambi ni kelele mbele zake, na maombi ya mwenye haki ni kama manukato. Kwa hiyo Mungu hawezi kusikiliza kelele (maombi ya mwenye dhambi), bali hupendezwa na harufu nzuri ya manukato (maombi ya mwenye haki). Isaya 59:1-2, Ufunuo 5:8, Mithali 15:8, 29, Zaburi 34:15, Yohana 9:31.
  • Imani. Ni mkono wa kupokelea majibu ya maombi yako kutoka kwa Mungu, huwezi kupokea majibu ya maombi yako kama huna imani. Luka 11:24, Luka 9:2, Mathayo 17:19-20, Yakobo 5:15.
  • Usifanye maombi ya kujiinua au kujisifu.  Siku zote Mungu anapendezwa na mioyo iliyoshuka, mioyo inayonyenyekea. Moyo wa kujiinua ni chukizo mbele za Bwana. Luka 18:11-14.
  • Tunaomba kupitia Jina la Yesu Kristo. Ukiwa umejitakasa na umeambatanisha imani, ukilitumia Jina la Yesu Kristo hakika utayaona matokeo ya maombi yako. Hatuna jina jingine tuliloagizwa kulitumia katika maombi yetu, ni Jina la Yesu Kristo pekee. Yohana 14:13-14, Yohana 15:16.
  • Usilalamike, peleka hoja mbele za Mungu. Kuna baadhi ya watu wanapofika mbele za Mungu kwa ajili ya kuomba, badala ya kuomba wanaishia kulalamika. Kwa mfano umefikwa na ugonjwa, usilalamike bali muulize Mungu nini makusudi ya ugonjwa huo? Na mwambie kuwa unataka kupona, ili uendelee kuifanya kazi yake ambayo inasimama kwa sababu ya ugonjwa uliokupata. Unapopata nafasi ya kusimama mbele za Mungu, hakikisha unaongea hoja zenye nguvu na siyo unatoa lawama tu, Mungu hajawahi kujibu lawama za mtu hata siku moja. Isaya 43:26, Habakuki 2.
  • Kuna maombi hayaendi pasipo sadaka. Hapa ni lazima uwe makini kumsikiliza Mungu, unaweza ukawa umeombea jambo moja kwa muda mrefu halafu hupati majibu, huenda Mungu anasema na wewe kwa habari ya kumtolea sadaka lakini unashindwa kumuelewa. Mungu anaweza akasema na wewe kwa sauti ndani ya moyo wako uwapo katika maombi, ama akasema na wewe kupitia watumishi wake. Yona 2:1 na 9-10, hapa ni maombi ya Yona ndani ya tumbo la samaki, licha ya kuomba maombi marefu yule samaki hakumtapika Yona, lakini katika mstari wa 9, Yona alisema nitatoa sadaka an kuziondoa nadhiri zangu, Biblia inasema, Mungu akasema na yule samaki naye akamtapika Yona. Kwa hivyo, kuna maombi yanasukumwa na sadaka. Ukitaka kubalikiwa kwa habari ya mwili, toa fungu la kumi (zaka). Malaki 3:10-12.
  • Uvumulivu. Uombapo, mngoje Bwana akupe majibu sahihi kwa wakati sahihi. Kuna watu wamepokea majibu yasiyokamilika kwa sababu ya kukosa uvumilivu. Bwana anajua unatakiwa kupewa nini kwa wakati gani, ukiwa umefanya kwa sehemu yako ya kuomba, hapo mngojee Bwana naye afanye kwa sehemu yake, kukujibu. Zaburi 40:1, Warumi 8:25, Waebrania 6:15.



 Faida za maombi.

Njia ya kumjulisha Mungu haja za mioyo yetu. Tunapokuwa na mahitaji ya kiroho na kimwili mbele za Mungu, hatuwezi kumtuma mtu atupelekee hizo haja zetu mbinguni, bali tunazipeleka sisi wenyewe mbele za Mungu kwa njia ya maombi. Isaya 43:26, Isaya 1:18, Wafilipi 4:6.

Kupitia maombi, Mungu huongea nasi kwa njia ya maono au sauti ya wazi mioyoni mwetu. Matendo ya Mitume 10:9-15, hapa ni wakati Mungu anasema na Petro kwa habari ya mtumishi wake Kornelio. Mungu aliongea na Petro kwa njia ya maono wakati Petro alipokuwa katika maombi.

Maombi ni jibu la kila kitu. Maombi yakisindikizwa na vitu kama; utakatifu, imani na sadaka, hutoa jibu la kila jambo. Hufungua vifungo vya shetani, huponya magonjwa, huinua walemavu na hata magonjwa sugu na yasiyo na tiba hupata kupona. Mathayo 21:22.

Maombi hutufanya tukue kiroho. Tunapoongea na Mungu, na anapotufunulia siri za ufalme wake tuwapo katika maombi, na imani yetu inapokuwa kupitia matendo ya Mungu yatokanayo na maombi yetu, tunakuwa kiroho. Mathayo 17:14-21.


Huu ndiyo mwanzo wa somo letu zuri, ambalo nina hakika litakubariki. Wajulishe na wenzako ili nao wabarikiwe. "Share" na "like" somo hili katika ukurasa wako wa facebook na twitter ili uwabariki marafiki zako. Mungu akubariki sana, tukutane tena jumapili, tarehe 30/06/2013.

Friday, June 14, 2013

NDIPO UJITUNZE USIJE UKAMSAHAU BWANA MUNGU WAKO.



Bwana Yesu asifiwe!

Somo letu la leo ni lenye kichwa “NDIPO UJITUNZE USIJE UKAMSAHAU BWANA MUNGU WAKO”, hapo unaweza ukajiuliza ujitunze nini? Au ujitunzaje?

Cha kujitunza hapa ni moyo wako, kwa sababu tabia ya moyo wa mwanadamu ni kupata kile unachokihitaji kwa njia yoyote na gharama yoyote isipokuwa kitu hicho kiwe ni dhambi kwa Mkristo, lakini wapo Wakristo ambao wametimiza haja za mioyo yao ambazo ni chukizo mbele za Bwana.

Sasa baada ya kutimiza matamanio ya moyo, iwe kwa njia halali au isiyo halali, moyo hurizika. Baada ya moyo kuridhika mwanadamu husahau vyote nje na riziki ya moyo wake. Hiyo ndiyo tabia ya moyo.

Tuangalie neno la Mungu linavyosema;
Kumbukumbu la Torati 6:10-13. Tena itakuwa atakapokwisha Bwana, Mungu wako, kukuleta katika nchi aliyowaapia babu zako, Ibrahimu na Isaka na Yakobo, ya kuwa atakupa; miji mikubwa mizuri usiyoijenga wewe, na nyumba zimejaa vitu vyema vyote usizojaza wewe, na visima vimefukuliwa usivyofukua wewe, mashamba ya mizabibu na mizeituni usiyoipanda wewe, nawe utakula na kushiba; ndipo ujitunze usije ukamsahau Bwana aliyekutoa nchi ya Misri, nyumba ya utumwa. Mche Bwana, Mungu wako; ndiye utakayemtumikia, na kuapa kwa jina lake.

Moyo wa mwanadamu siku zote unawaza mafanikio ya mwili, kumiliki majumba, mashamba, magari, wanyama n.k na kwa juhudi zote mwanadamu huyu atahakikisha anatimiza matamanio ya moyo wake. Katika kipindi cha kutafuta, mwanadamu huyu hujitoa moyo wake wote kumpenda Bwana, Mungu wake na mchana na usiku humlilia Mungu ambariki. 

Inapotokea mwanadamu huyu amefanikiwa, moyo wake hurizika na kumsahau Mungu aliye chanzo cha baraka na mafanikio yake (Zaburi 24:1, 1 Wakorintho 10:26). Na hii ndiyo imekuwa sababu, kuna watu wamelia na kuomba baraka za mwili na mafanikio lakini wamekosa, Mungu anajua siku atakapokufanikisha, moyo wako utamsahau Mungu.

Siyo kwamba Mungu anatufundisha kutotafuta mali, la hasha, Mungu anatuonya kuwa tupatapo mali au utajiri, mioyo yetu isimsahau Mungu na kujaza mali katika nafasi ya Mungu. Yaani Mungu asiwe “substituted” na mali au utajiri ulionao. 

Luka 12:16-19. Akawaambia mithali, kuwa shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akasema, nifanyaje? maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, nitafanya hivi, nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu.  Kisha nitajiambia ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe na ufurahi.

Hapa tunapata somo kupitia huyu tajiri, alipofanikiwa alijiambia moyo wake kuwa atajenga ghala kubwa ya kuweka akiba vitu vyake vizuri, na akajiambia tena, ee nafsi yangu kula, unywe na ufulahi. Hapa tunatambua moja kwa moja kuwa tajiri huyu alilidhika nafsini mwake hata akamsahau Mungu. 

Kwanini nasema alimsahau Mungu; hakusema neno lolote la kumshukuru Mungu, nafasi ya Mungu moyoni mwake sasa ilikuwa imejaa utajiri na mali aliyonayo.

Vivyo hivyo na wanadamu wa siku hizi, wakipata mali, mioyo yao inamsahau Mungu na wanaanza kuitumikia mali waliyonayo (Torati 6:14-15). Mungu anasema utapofanikiwa, usisahau kumtumikia Mungu, Bwana wako. Unaweza ukasema mbona bado nampenda Mungu na ninamtumikia pia, ngoja nikwambie, amri kuu ya Mungu inasema umpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa akili zako zote na kwa nguvu zako zote.

Sasa wewe unampenda Mungu, Bwana wako kwa akili yako na nguvu zako, lakini moyo wako unapenda na kuitumikia mali uliyonayo. Hujatimiza amri kuu ya Mungu bado. Kwa sababu umejiinulia mungu mwingine mbali na huyo Mungu unayedai unamwabudu. Mungu, Bwana wetu alishatuonya kuwa hatuwezi kutumikia mabwana wawili, hatuwezi kumpenda Mungu na mali (Luka 16:13, Mathayo 6:24). 

Kama kwa akili zetu na nguvu zetu tunampenda na kumtumikia Mungu, lakini mioyo yetu inapenda na kutumikia mali tulizonazo, hatutendi kitu bado.

Kupitia mali zako unatakiwa umtumikie Mungu, ukiunganisha na akili na nguvu zako unakuwa kweli umempenda Mungu. Kwa sababu mali hukaa moyoni, ukiweza kumtumikia Mungu kwa mali zako na kumpenda Mungu kwa moyo wako, hapo unakuwa umetimiza amri kuu ya kwanza ya Mungu (Mathayo 22:37-38). Usimtoe Mungu ndani ya moyo wako na kuweka mali na utajiri ulionao, ukifanya hivyo hutoweza kuikwepa hasira ya Bwana, Mungu wako (Kumbukumbu la Torati 6:15).

Na kama umeamua kumtumikia Mungu kwa mali zako, usifanye kwa mashindano ili uonekane na watu na kupata sifa machoni mwao (Luka 18:9-14), hiyo ni habari ya Farisayo na mtoza ushuru waliokwenda hekaluni kuomba, maombi ya huyu Farisayo yanatuonesha kila alilofanya alifanya ilia pate sifa machoni mwa wanadamu na alifanya kwa mashindano (Filipi 2:3).                                                   
Unapomtumikia Mungu kwa mali zako, usito masalio ya mali/fedha yako au wanyama walemavu katika kundi la wanyama wako na kupeleka madhabahuni mwa Bwana, Mungu wako kwani hapendezwi na dhabihu ya aina hiyo (Mambo ya Walawi 22:21, Marko 12:41-44).

Kama ulikuwa ukiishi maisha ya aina hii; ulimtoa Mungu moyoni mwako na kujaza mali na fedha ulizonazo, ulimtumikia Mungu kwa mali na fedha zako ili uonekane na watu au ulimtolea Mungu masalio au ziada tu katika mali yako na fedh yako na labda ulitoa wanyama wenye ulemavu na magonjwa katika madhabahu ya Bwana, Mungu wako, leo hii Mungu anataka kutengeneza na wewe, nafasi ipo na neema ya Mungu yatosha, amua sasa kubadilika.

Na ikiwa upo kwenye mchakato na hatua za kuelekea mafanikio, usumsahau Bwana, Mungu wako. Usiache nafasi ya Mungu moyoni mwako ijazwe na mali utakayo ipata, ndipo mali yako itakuwa ni ya kudumu.

“Share somo hili kwa marafiki zako, na Mungu wa mbinguni akubariki sana”.

Saturday, June 8, 2013

KWA NINI YOHANA MBATIZAJI ALIULIZA, “WEWE NDIWE YULE AJAYE, AU TUMTAZAMIE MWINGINE?” MATHAYO 11:3.



Yohana Mbatizaji aliuliza swali hilo kana kwamba hamjui Yesu Kristo na hakuwahi kumuona bali alizisikia habari za ujio wake tu.

Lakini ukisoma maandiko utaona kuwa Yohana mbatizaji alikuwa akimjua Yesu Kristo na aliwahi kukutana naye;

Mathayo 3:11. Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto. 

Mstari huo wa Biblia unatueleza kuwa Yohana Mbatizaji aliutambua ujuo wa Yesu Kristo hata kabla hajaonana na Yesu Kristo mwenyewe.

Mathayo 3:13-14. Wakati huo Yesu akaja kutoka Galilaya mpaka Yordani kwa Yohana ili abatizwe. Lakini Yohana alitaka kumzuia, akisema, Mimi nahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu?

Mstari huo wa Biblia unathibitisha kuwa Yohana Mbatizaji aliwahi kukutana na kuongea na Yesu Kristo, na alimtambua kuwa ndiye Masihi wa Mungu kwa sababu alitaka kumzuia asimbatize bali yeye Yohana ndiyo abatizwe na Yesu. Pia sauti ya uthibitisho ilisikika kutoka mbinguni, na mkutano wote waliisikia (Mathayo 3:17).

Sasa iwaje Yohana Mbatizaji alipokuwa gerezani na alipozipata habari za Yesu Kristo na matendo ya miujiza aliyoifanya (alizijua nguvu zake pia, Mathayo 3:11b), aliwatuma wanafunzi wake wakamuulize Yesu Kristo swali hili; “Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine?” Mathayo 11:3.

Yohana Mbatizaji aliuliza swali hili kwa sababu; alitegemea Yesu Kristo angeenda kumuona gerezani, na alitegemea kupata kipaumbele kutoka kwa Yesu katika kipindi alichokuwa kizuizini, lakini Yesu Kristo aliwapa kipaumbele wenye dhambi na watoza ushuru (Luka 15:2).

Yesu Kristo alitambua makusudi ya Yohana Mbatizaji kuuliza swali hilo, ndipo alipowajibu wanafunzi wa Yohana Mbatizaji;

(a). “Nendeni mkamueleze Yohana mnayoyasikia na kuyaona; vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.” Mathayo 11:4, 5. 

Hapa Yesu Kristo alikuwa akimthibitishia Yohana Mbatizaji kuwa yeye ndiye.

(b). baada ya wanafunzi wa Yohana Mbatizaji kuondoka Yesu Kristo akaongezea, “Lakini nitakifananisha na nini kizazi hiki? Maana Yohana alikuja, hali wala hanywi, wakasema, Yuna pepo. Mwana wa Adamu alikuja akila na kunywa, wakasema, Mlafi huyu, na mlevi, rafiki yao watoza ushuru na wenye dhambi!” (Mathayo 11:16-19). 

Ukiangalia pia Luka 5:30-32. Ikawa mafarisayo na waandishi wao kuwanung’unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.

Hapo Yesu Kristo alitaka kutufundisha kuwa anachokipa kipaumbele zaidi ni kile kilichomleta duniani; kuutangaza ufalme wa Mungu na kuziokoa roho zinazopotea dhambini. Ndipo aliposema mfano huu, “ni nani kwenu aliye na kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone?”, “Nawaambia, vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu”. Luka 15:3-7.

Yesu Kristo anazidi kufafanua kuwa, yeye kuwa karibu na wenye dhambi ni ili aziokoe roho zao. Hawapi kipaumbele zaidi wenye haki, bali wenye dhambi.



Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts