Saturday, October 12, 2013

KWANINI YESU KRISTO ALIPOTAKA KWENDA FARAGHA, KATIKA MAOMBI, AU ALIPOAMUA KUFANYA JAMBO LA KIPEKEE ALICHAGUA KUAMBATANA NA PETRO, YOHANA NA YAKOBO?



 Ukiyachunguza maandiko katika vitabu vya Biblia vya Injili zile nne; Injili ya Mathayo, Marko, Luka na Yohana utakutana na vifungu vingi vikionesha jinsi Bwana wetu Yesu Kristo alivyopenda kuambatana na Petro, Yohana na Yakobo.

Na alipenda kuambata na wanafunzi wake hao watatu; Petro, Yohana na Yakobo sehemu muhimu au katika shughuli muhimu. Kwa mfano, alipotaka kwenda faragha kwa maombi au alipoamua kufanya jambo la uponyaji lililohitaji imani kubwa.

Kuna sababu nyingi sana zilizomfanya Bwana wetu Yesu Kristo apende kuambatana na wanafunzi wake hao watatu katika faragha na sehemu muhimu mbali mbali.

Petro, Yohana na Yakobo richa ya kwamba walikuwa ndugu (Yakobo na Yohana - Mathayo 4:21) na marafiki (Marko 13:3, Matendo ya Mitume 3:1) walikuwa wana sifa za pamoja zinazofana na sifa za kila mmoja wao, ambazo kwa umoja wao walitengeneza timu iliyompendeza Yesu Kristo.

Hebu tuangalie baadhi ya vifungu vinavyo thibitisha kuwa Bwana wetu Yesu Kristo alipenda kuongozana zaidi na Petro, Yohana na Yakobo kwa maombi ya faragha au katika jambo la kipekee na umuhimu zaidi.

Mathayo 17:1. Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu yam lima mrefu faraghani (kwa maombi).

Marko 1:29. Na mara walipotoka katika sinagogi, walifika nyumbani kwa Simoni na Andrea, pamoja na Yakobo na Yohana. Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia (Yesu Kristo) habari zake.  (Yesu Kristo) Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia.

Marko 5:37. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo.

Luka 22:8. Akawatuma Petro na Yohana, akisema, Nendeni, mkatuandalie pasaka tupate kuila.

Marko 14:32-33. Kisha wakaja mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa muda niombapo. Akamtwaa Petro na Yakobo na Yohana pamoja naye, akaanza kufadhaika sana na kuhangaika.


Hivyo ni baadhi ya vifungu vya Biblia vinavyo thibitisha jinsi Yesu Kristo alivyopenda kuwa karibu na Petro, Yakobo na Yohana.

Kama nilivyotangulia kusema hapo juu, Petro, Yohana na Yakobo walikuwa na sifa za ujumla na sifa za pekee kwa kila mmoja. Ukaribu wao uliosababishwa na undugu na urafiki uliwafanya watengeneze umoja wa pekee kwani waliunganisha sifa zao na kufanyika kitu kimoja. 

Sifa zao kwa ujumla ndizo zilizomfanya Yesu apende kufanya nao mambo kwa umoja. Hebu tuziangalie sifa za wanafunzi hao kwa umoja na kwa upekee.

Sifa za pamoja;

Historia moja. Petro, Yohana na Yakobo walikuwa wanafunzi wa Yesu Kristo wenye historia ya aina moja kuhusu mahali walipoishi, aina ya kazi waliyofanya (uvuvi) na sehemu au mahali walipofanyia kazi yao (bahari ya Galilaya). Hii inapatikana katika; Mathayo 4:18-20, Marko 1:16-20 na Luka 5:4-11.

Wenye imani kubwa na thabiti. Walikuwa ni wanafunzi wa Yesu wenye imani iliyosimama imara, walioamini uwezo wa Yesu wa Kiungu pasipo na shaka yoyote. Hawakuwa na swali juu ya utendaji kazi wa Yesu. Na hata wengine walipotindikiwa imani, wanafunzi hawa waliendelea kuamini kuwa Yesu Kristo anao uwezo na nguvu za Kiungu. Hii inathibitishwa na Mathayo 14:28-29 na Matendo ya Mitume 3:3-8. 

Na kutokana na imani yao, Yesu Kristo alikwenda nao kufanya uponyaji wenye kuhitaji imani kubwa pia. Hii inapatikana katika Luka 8:50-51. Katika kifungu hicho cha Biblia, Yesu Kristo alipoingia ndani ya chumba cha yule binti marehemu aliingia na Petro, Yohana na Yakobo pamoja na wazazi wa yule binti kutokana na imani yao thabiti isiyokuwa na shaka.

Walipenda kuwa na Yesu kwa faragha. Wanafunzi hawa wa Yesu walipenda kumdadisi Yesu mambo fulani, na mara nyingi walipoamua kumdadisi Yesu jambo walilifanya kwa faragha. Walijichukua wao na kumfuata Yesu na kumuuliza duku duku lao. Soma vifungu vifuatavyo; Marko 10:35, Marko 13:3.

Marafiki. Wanafunzi hawa wa Yesu Kristo walipenda zaidi wao na walikuwa ni marafiki. Ukisoma katika Biblia utaona walikuwa wakifuatana sehemu nyingi hata walipokuwa hawako na Yesu, Marko 13:3 na Matendo ya Mitume 3:1. Na hata neno linasema watu hawawezi kuongozana isipokuwa wamepatana (Amosi 3:3). Kwa hiyo wanafunzi hawa watatu wa Yesu walikuwa wanapatana zaidi.

Sifa za mmoja mmoja;

Petro (Simoni Petro).

Historia fupi ya Mtume Petro;
Mtume Petro alizaliwa Betsaida, mjini Galilaya katika nchi ya Israeli. Yeye na baba yake, Yona walikuwa wavuvi katika bahari ya Galilaya. Alikuwa na kaka aitwaye Andrea, alikuwa miongoni mwa Mitume wa Yesu Kristo.

Yesu Kristo alimwita Simon Petro mwamba, na kumfanya kuwa msingi wa kanisa imara ambalo milango ya kuzimu hailiwezi. Mathayo 16:18.

Na siku ya Pentekoste, wanafunzi wa Yesu Kristo walipojazwa nguvu za Roho Mtakatifu, Simoni Petro alisimama kwa ujasiri na kusema na makutano waliokusanyika wakishangaa. Matendo ya Mitume 2:14-21.

Simoni Petro alifungwa gerezani mara kadhaa kwa kumuhubiri Yesu Kristo baada ya kifo na ufufuko wa Yesu Kristo. Kisha Petro alihamia mjini Roma ili aihubiri injili ya Yesu Kristo ambapo alifia huko kwa kusulubishwa kichwa chini miguu juu.

Mdadisi. Katika wanafunzi wote 12 wa Yesu Kristo, ni Petro peke yake aliyekuwa haachi jambo limpite endapo hakulielewa. Mara nyingi alipenda kujua maana ya mafumbo/mifano aliyoiongea Yesu, na hata kuna wakati alitaka kujua faida ya wao kuacha vyote na kumfuata Yesu Kristo. Mathayo 15:15, Marko 10:28 na Luka 18:28.

Alijiamini. Petro ni mwanafunzi wa Yesu ambaye hakuteteleka kwa jambo lolote na kwa hali yoyote. Alijiamini na alijua anaweza hata katika nyakati ambazo wanafunzi wengine wote waliporudi nyuma, Petro alisimama peke yake na kusonga mbele. Marko 14:27 na 29, Luka 22:54, Yohana 18:10.

Asiyekatishwa tamaa. Kuna nyakati Petro alikutana na mambo ya kukatisha tamaa na kurudishwa nyuma, lakini alisimama imara, hakutetereka. Kuna kipindi Yesu Kristo alimtamkia “rudi nyuma shetani” lakini Petro alitambua haikuwa kauli elekezi kwake, bali ilikuwa ni kauli iliyotumwa kwa shetani kupitia yeye, Marko 8:33. Wanadamu wengi wakiambiwa kauli hii watakata tamaa mara moja.

Yohana.

Historia fupi ya Yohana;
Yohana mwana wa Zebedayo, pamoja na ndugu yake Yakobo walikuwa wavuvi katika bahari ya Galilaya. Walifanya kazi hiyo pamoja na Simoni Petro na ndugu yake Andrea.
Yohana na ndugu yake Yakobo walipewa jina la Boanerge na Bwana wetu Yesu Kristo, ikimaanisha wana wa ngurumo. Marko 3:17.

Yohana ni mwanafunzi au mtume wa Yesu Kristo aliyeshuhudia mateso hadi kifo cha Yesu Kristo, pasipo kujificha wala kuogopa.

Yohana ni mtume pekee aliyependwa sana na Yesu Kristo, na hata siku ya kifo cha Yesu Kristo msalabani alimkabidhi mama yake (bikira Mariamu) kwa Yohana. Yohana 19:26-27.
Yohana ni mtume wa Yesu Kristo aliyeandika Injili ya Yohana na Nyaraka tatu za Yohana wa 1, 2 na 3.

Alipendwa sana na Yesu Kristo. Kuna mistari kadhaa katika Biblia inasema kuna mwanafunzi alipendwa sana na Yesu, japo haitaji jina la mwanafunzi huyo. Lakini wana Theologia wanamtaja mwanafunzi huyo kuwa ni Yohana. Yohana 13:23, Yohana 20:2.

Alidhamiria kumfuata na kumtumikia Yesu Kristo. Yohana alijitoa mwili na roho kumtumikia Yesu Kristo na alitamani sana kuona siku moja anaketi pamoja na Yesu Kristo katika ufalme wa Mungu. Na kuna wakati aliomba kuketi karibu na Yesu katika ufalme ujao wa Mungu, Marko 10:35-36.

Yakobo.

Historia fupi ya Yakobo;
Alikuwa ni miongoni mwa wanafunzi wa kwanza kuchaguliwa na Bwana wetu Yesu Kristo, yeye pamoja na ndugu yake Yohana. Alifanya kazi ya uvuvi katika bahari ya Galilaya pamoja na ndugu yake na baba yao Zebedayo.

Yakobo alikuwa ni mzaliwa wa Kapernaum, baada ya kifo na ufufuo wa Yesu Kristo, Yakobo aliendelea kuihubiri Injili ya Yesu Kristo. Aliuawa na mfalme Herode kwa kukatwa kichwa kwa upanga. Matendo ya Mitume 12:1-2.

Hitimisho.
Katika jumla ya wanafunzi wote kumi na wawili (12) wa Yesu Kristo, ni wanafunzi watatu tu waliopata nafasi ya kuwa karibu na Yesu Kristo na kufanya kitu kinachoitwa “Christ’s inner circle”, wanafunzi hao ni Petro, Yohana na Yakobo.

Wanafunzi hawa walipata bahati au nafasi ya kushuhudia matendo makuu ya Yesu Kristo pasipo uwepo wa wanafunzi wengine. 

Matendo au nyakati hizo ni; ufufuo wa binti Yairo (Marko 5:35-42), kubadilika uso na mavazi yake (Mathayo 17:1-3) na maombi ya mwisho ya Yesu Kristo kabla ya mateso ya msalaba (Mathayo 26:36-38).

2 comments:

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts