Sunday, August 19, 2012

MIMI NDIMI BWANA NIKUPONYAYE


  Kutoka 15:26 “…kwa kuwa Mimi ndimi Bwana nikuponyaye.” Watu wengi wamekuwa wakihangaika kwenda huku na huko wakitafuta uponyaji wa magonjwa na madhaifu ya namna mbali mbali yanayowasumbua katika afya za miili yao, inawezekana ukawa wewe au ndugu yako wa karibu. Na mara nyingine utawakuta watu wa namna hii wamefikia hata hatua ya kwenda kwa waganga wa kienyeji. Ngoja nikufungue akili utambue kitu; ili mtu awe daktari ni lazima afundishwe na madaktari masomo yanayohusu udaktari, na ili mtu awe mganga wa kienyeji ni lazima afundishwe uganga wa kienyeji na mganga wa kienyeji. Na ukikuta mganga wa kienyeji anasema ngoja tuiulize mizimu ama kwa lugha nyingine wanawaita waungwana utambue moja kwa moja kuwa uganga wake una mahusiano na nguvu za giza (uchawi). Ni vema kutumia chakula; mboga za majani na matunda kwa kujenga na kulinda afya yako na hata kutibu baadhi ya magonjwa kama masomo yapatikanayo katika ukurasa wa dondoo za afya (Health Tips)  yanavyokuelekeza.
  Napenda nikwambie kama jinsi Mungu anvyosema, “Mimi ndimi Bwana nikuponyaye” anamaanisha anachokisema na kamwe Mungu hajawahi na hatawahi kusema uongo. Hebu tuangalie ahadi nyingine za neno la Mungu kuhusu kutuponya na magonjwa na madhaifu yanayotupata:-

Kutoka 23:25 “…,Nami nitakuondolea ugonjwa kati yako.”,  Zaburi 103:3 “Akuponya magonjwa yako yote.”, Isaya 33:24 “Wala hapana mwenyeji atakaye sema, Mimi mgonjwa.”, Yeremia 30:17 “Maana nitakurudishia afya, name nitakuponya jeraha zako, asema Bwana.”, Mathayo 4:23 “na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu.”, Luka 9:11 “akawaponya wale wenye haja ya kuponywa.”
Hizo ni chache katika ahadi za Mungu nyingi zinazoahidi uponyaji wa magonjwa na madhaifu yanayo kusumbua. Na kama Bwana asemavyo, “Mimi ndimi Bwana nikuponyaye, akuponya magonjwa yako yote(Zaburi 103:3), maana nitakurudishia afya (Yeremia 30:17)”. Katika mistari hiyo Mungu anatuonesha kuwa anao uwezo wa kuponya kila namna au aina ya ugonjwa na udhaifu ndani ya miili yetu. Na katika neno lake amesema “akawaponya wale wenye haja ya kuponywa (Luka 9:11)”, hapo Mungu anatufundisha kitu kinachoitwa imani na kumtegemea yeye. Ili uweze kupokea uponyaji unapaswa uwe na imani na umtegemee Mungu asilimia mia moja, kwa sababu imani hutupatia haki ya kupokea kutoka kwa Bwana Mungu (soma: Mwanzo 15:6 “Akamwamini Bwana, naye akamuhesabia jambo hili kuwa haki”). Kwa hiyo imani inakupa haki ya kupokea kile unachokiamini, endelea kumwamini Bwana na kuomba uponyaji wako uko njiani usikate tama kwani Mungu yuko karibu akuponye.
  Ikiwa umelipokea neno hili kwa imani, na utaamua kulifanyia kazi nakuhakikishia utapokea uponyaji wako kwa Jina la Yesu Kristo Bwana wetu, Amina.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts