Friday, November 9, 2012

MSAMAHA.


   Msamaha ni kufuta au kuachilia mzigo wa makosa unayotendewa na mtu pasipo kuhesabu ni mara ngapi mtu huyo amekukosea.
Isaya 43:25 “Mimi, naam, mimi ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; wala sitazikumbuka dhambi zako”.
Hapo neno la Mungu linatufundisha kuwa; msamaha ni kuyafuta makosa (dhambi) na kutoyakumbuka tena.
Luka 6:37b “…achilieni, nanyi mtaachiliwa”.
Hapa tunaona kuwa maana nyingine ya msamaha ni kuachilia; mtu anaposhindwa kusamehe anabeba mzigo wa hasira ndani ya moyo wake, ambapo mzigo huu unaweza kumfanya mtu huyu akose raha, amani na hata furaha. Hapo Mungu anatuambia tuachilie na kutua mizigo iliyo ndani ya mioyo yetu.
AINA ZA MSAMAHA.
Kuna aina mbili za kusamehe, aina hizi ni;
(a). Msamaha wa kidunia.
Huu ni msamaha wa kusamehe na kutosahau. Msamaha huu hautokani na Mungu, na haukubaliki mbele za Mungu.
Ni msamaha wa kinafiki, mtu anakwambia amekusamehe lakini ndani ya moyo wake ana uchungu nawe. Msamaha huu unahesabu makosa, na wengu wameumia kwa sababu ya kusamehe kwa kutumia msamaha wa aina hii. Unapomwambia mtu nimekusamehe na kumbe bado una uchungu naye, yeye anapata amani na furaha lakini wewe unajawa na uchungu na hasira inayokufanya uumie moyo.
Wengi wetu tumekuwa na msamaha wa aina hii, Mungu atusaidie tuwe na msamaha wa Kimungu kwani msamaha huu una raha na faida. Kuna watu wamekonda na hawana raha siyo kwa sababu ya maisha magumu, bali ni kwa sababu wanavinyongo na mizigo mizito ndani ya mioyo yao.
(b). Msamaha wa Kimungu.
   Huu ni msamaha wa kusamehe na kusahau kabisa. Msamaha huu ni wa Mungu na unatokana na Mungu mwenyewe, kwani Mungu anasema yeye anatusamehe na kusahau kabisa makosa yetu (Isaya 43:25). Nasi kama watoto wa Mungu tunapaswa kuwa na tabia ya Mungu katika kusamehe, tunapaswa tusamehe na kusahau yote tunayokosewa na wenzetu.

FAIDA ZA KUSAMEHE.
Unaposamehe wengine unapa faida zifuatazo ambazo hakuna njia nyingine ya mkato ya kuzipata faida hizi zaidi ya kusamehe kwa dhati (kasamehe na kusahau, kusamehe na kutohesabu makosa).
(a). Kusamehewa.
   Tunapo wasamehe waliotukosea na kutokumbuka waliyotukosea, Mungu wetu naye anatusamehe sisi makosa yetu.
Luka 11:4 “Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye”. Hii sehemu ya sala aliyotufundisha Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba tunapaswa kumuomba Mungu msamaha ikiwa tu, nasi tunawasamehe wanaotukosea. Kwa maana hiyo Mungu huwasamehe watu makosa yao endapo watu hao nao wanawasamehe wenzao wanao wakosea.
(b). Kuyapa kibali maombi yetu mbele za Mungu.
   Tunapo wasamehe wenzetu kwa dhati, naye Mungu wetu anatusamehe sisi na akiisha tusamehe anayakubali maombi yetu tunayoyapeleka mbele zake. Hivyo tunapata uhakika wa kujibiwa.
Marko 11:25 “Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu”. Hapa pia Bwana wetu Yesu Kristo anatufundisha kuwa kila tunapoingia katika maombi ni lazima tuwasamehe kwa dhati na kusahau makosa yao wale wote walio tukosea na ndipo tuendelee na maombi yetu.
HASARA YA KUTOSAMEHE.
   Unapokosa msamaha wa kweli kwa wanaokukosea unjifungia mlango wa kusamehewa na Mungu, unayanyima kibali maombi yako mwenyewe mbele za Mungu, na unabeba mzigo ambao utakuumiza na kuutesa moyo wako.
Na pia unapokosa msamaha kwa wakosaji wako, unamfanya Mungu asipokee sadaka yako hata ingekuwa kubwa kiasi gani au umejitoa kwa moyo wote kiasi gani. Samehe kwanza na ndipo utoe sadaka yako tena kwa moyo wa kupenda nayo itapata kibali mbele za Mungu naye ataitakabali na kukubariki kwa hiyo.
Mathayo 5:23 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako na neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kasha urudi uitoe sadaka yako”. Hayo ni maneno ya Mungu mwenyewe kupitia Mwana wake, Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba endapo tumefarakana au tumekosana na mtu yoyote ni lazima tupatane naye kabla ya kutoa sadaka zetu. Haipo maana kama tunatoa sadaka nasi tumeshindwa kuwasamehe wenzetu.
Ndugu yangu mpendwa katika Kristo Yesu, ninakusihi uwe mwepesi wa kusamehe na kusahau. Na kama unaona huwezi kusamehe na kusahau, muombe Yesu Kristo akusaidie kwani yeye ndiye Bwana wa yote, name ninakuhakikishia kuwa kwa Jina la Yesu Kristo wa Nazareti mambo yatakuwa sawa. Amina.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts