Sunday, December 16, 2012

KANUNI ZA KUISHI MAISHA YA USHINDI NA BARAKA.



   Kila jambo analokutana nalo mwanadamu lina sababu ya kuwepo, na kuna nguvu inayolishikilia hilo jambo liendelee kuwepo. Endapo hiyo nguvu itakatwa, basi hilo jambo haliwezi kuendelea kuwepo. Na uwepo wa nguvu unaosababisha mambo kutendeka unategemea kanuni; ili usipate magonjwa ya kuambukiza, zipo kanuni za kujiepusha na magonjwa hayo.

   Na katika mambo ya rohoni, kuna kanuni za kuyapata hayo mambo ya rohoni; ili ubarikiwe, ule matunda ya kazi za mikono yako na upokee uponyaji ni lazima uzingatie kanuni. Na kanuni hizo ni; uwe mnyenyekevu kwa Mungu, na unyenyekevu huo uambatane na maombi, maombi yaliyokusudia kuutafuta na kuuona uso wa Mungu, na ili uweze kuuona uso wa Mungu ni lazima uachane na njia zote mbaya.

2 Nyakati 17:13-14 “Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi, au nikiwapelekea watu wangu tauni; ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao”.

   Hapa neno mvua linabeba maana mbili; mvua kwa maana ya mvua, na mvua kama baraka. Na katika baadhi ya vitabu vitakatifu vya Biblia, Mungu analithibitisha hilo; (Isaya 30:23 Naye atatoa mvua juu ya mbegu zako, upate kuipanda nchi hii; na mkate wa mazao ya nchi, nayo itasitawi na kuzaa tele; katika siku hiyo ng’ombe zako watakula katika malisho mapana), mvua kama baraka- Malaki 3:10 “. . . mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la”.

Kwa hiyo, mbingu zikifungwa kusiwe na mvua; mvua kama mvua inaweza isinyeshe na mvua kama baraka inaweza pia isipatikane. Na ukikosa baraka, basi una laana; inaweza ikawa ni laana ya ukoo, laana ya kutamkiwa (Mithali 11:26, 24:24,) au ya kujitamkia kwa kujua au pasipo kujua, au laana inayotokana na kutenda dhambi (Kumbukumbu la torati 28:15, Malaki 2:2, Zaburi 119:21).

   Nzige kula nchi; nzige hula mimea au mazao yaliyootayo juu ya nchi, wanapokula mazao hula chakula cha binadamu (Zaburi 105:34-35 “Alisema, kukaja nzige na tunutu wasiohesabika wakaila miche yote ya nchi yao, wakayala matunda ya ardhi yao”). 

Unaweza kuwa na huduma iliyodumaa au imekufa kabisa, unafanya kazi lakini huli matunda stahili ya kazi yako au wewe ni mkulima lakini mavuno ni hafifu. Katika hali hizo, nzige wamekula nchi, ni lazima ufanye jambo kuikomboa nchi hiyo; kuinua au kufufua huduma yako, kunufaika na kazi ya mikono yako na hata kupata mavuno bora ya mashamba yako. Jambo hili linaweza kusababishwa na nguvu  za ufalme wa giza au maisha ya dhambi (Zaburi 119:21), lakini unaweza kujikomboa katika utumwa huo, zingatia kanuni.

   Tauni; neno hili linawakilisha magonjwa, ambayo yanaweza hata kuondoa uhai au kukuacha na ulemavu. Magonjwa yasiyo na tiba au magonjwa yasiyoeleweka yanasababishwa na nini, na inaweza ikawa ni malipo ya dhambi (Ayubu 8:3-4, 2 Samweli 24:15) au ni kuonewa na shetani. Lakini hayo yote yanaweza kukuachilia huru tangu sasa, ikiwa yamekupata wewe au ndugu yako, Mungu ni mwaminifu hakuwahi kusema uongo hata leo asema uongo.

Katika mambo hayo matatu; kukosa mvua, nzige kula nchi na tauni, inawezekana ukawa umepitia jambo moja wapo au yote kwa jinsi tulivyoyaona maana zake katika mwaka huu (2012) unaomalizika hivi karibuni. Na hungependa kuingia na kutembea na mwaka unaofuata (2013) na mambo hayo, unatamani kufunguliwa na kuwekwa huru; upokee baraka kutoka kwa Mungu, kuinua na kufufua huduma yako, kula matunda ya kazi za mikono yako na kuishi maisha yasiyojua ugonjwa/magonjwa, INAWEZEKANA! Zipo kanuni alizoziweka Mungu mwenyewe ili tupone, zingatia kanuni hizo. Kanuni hizo ni:-

   Kunyenyekea; ni kutii na kukubali sauti ya Mungu na kufanya yanayoelekezwa na sauti hiyo (Isaya 1:19 “. . . mkikubali na kutii, mtakula mema ya nchi”). Sauti ya Mungu siku zote inatuelekeza kuifuata njia njema, na kuifuata njia njema ni kuchagua mema; baraka, uponyaji, ushindi, heshima, kuinuliwa na mengine mengi mazuri. Kunyenyekea kunamfanya Mungu atumie muda wa ziada kututegea sikio na kuyasikiliza maombi yetu, na Mungu akiyasikiliza maombi yetu lazima tuwe na uhakika wa kupokea majibu (Danieli 12:10, Isaya 66:2). 

Kutonyenyekea kunainua hasira ya Mungu juu ya wanadamu, na ndipo tunapatwa na mabaya (Yeremia 44:10). Kwa hiyo hii ni kanuni ya kwanza, ukitaka kuwa rafiki wa Mungu na kupokea mema kutoka kwake, lazima unyenyekee.

   Kuomba; ni njia ya mwanadamu kuzungumza na Mungu (Isaya 1:18 “. . . haya njooni tusemezane. . .”), Mungu anaposema ‘njooni tusemezane’ anatufundisha kuomba ili tupeleke mahitaji yetu kwake na yeye atujibu kulingana natulivyoomba au tunavyostahili (Yakobo 5:13). 

Kuomba ni kanuni ya pili, ambayo ni lazima iambatane na kanuni ya kwanza (unyenyekevu), huwezi kuwa muombaji kama hunyenyekei. Unyenyekevu unakupa haki mbele za Mungu, na maombi ya mwenye haki ndiyo yanayofaa sana (Yakobo 5:16 kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii). Na hii ni kanuni ya pili.

   Kuutafuta uso wa Mungu; kama tulivyoona, hizi kanuni zina mfuatano wa kutegemeana, unapokuwa mnyenyekevu na muombaji ni rahisi sana kukutana na Mungu. Unapoomba hakikisha umekutana (umekuwa-connected) na Mungu na ndipo ueleze mahitaji yako. Jambo hili si jepesi, unahitaji kujitoa na kudhamiria; kuwa mnyenyekevu na muombaji na ndipo utakapokutana na Mungu (Mithali 8:17 . . . na wale wanitafutao kwa bidii wataniona. Yeremia 29:13 . . .nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote). Kanuni ya tatu.

Kuacha njia mbaya; ni kurudi kutoka dhambini na kumrejea Mungu. Unyenyekevu, maombi na kuutafuta uso wa Mungu ni lazima viambatane na toba, kila unaposogea mbele za Mungu hakikisha unajitakasa hata kama hukumbuki kumtenda Mungu dhambi (Hosea 5:15 . . . hata watakapoungama makosa yao na kunitafuta uso wangu. . .). Ukiamua kuacha njia mbaya, usijiweke tena katika mazingira ya kuirudia hiyo njia mbaya; epukana na mazingira ya kutenda dhambi kwa kuangalia, kusikiliza au kuongea (Yeremia 36:7 na kurudi, kila mtu akiiacha njia yake mbaya. Yeremia 35:15 rudini sasa, kila mtu na aiache njia yake mbaya, mkatengeneze matendo yenu). Na siyo utende dhambi makusudi kwa kuwa utaomba toba!! Kanuni ya nne.

Ni wewe mwenyewe, unayeweza kuamua na kujitoa kutoka katika maisha ya mateso na kuonewa na yule mwovu. Zingatia kufuata, kutenda na kuzitimiza kanuni, amua leo kuingia mwaka mpya na maisha mapya. Mungu akubariki sana, kwa jina la Yesu Kristo.

Unahitaji kuokoka? Bonyeza hapa.

Friday, December 7, 2012

NJIA UTAKAYOICHAGUA NDIYO NJIA UTAKAYOPITA.

   Mwanadamu wa kwanza aliumbwa katika ukamilifu; kiroho na kimwili, mtakatifu asiyejua dhambi na mwenye mwili usioonja mauti. Baada ya kuasi agizo la Mungu na kutenda dhambi, akapoteza ukamiliu wa utakatifu, lakini kwa vile Mungu ni pendo, anatupenda wanadamu akatuandalia ukombozi ili atununue kutoka katika ufalme wa giza na kutuingiza katika Ufalme wa Mwana wa pendo lake, Yesu Kristo.

   Lakini kuupokea ukombozi huo, ni hiyari ya mwanadamu mwenyewe, kwani baada ya kuitambua dhambi mwanadamu huyu alipata utashi wa kutambua wema na uovu (Mwanzo 3:7).
Kumbukumbu la Torati 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimeweka mbele yako uzima na mauti… basi chagua uzima ili uwe hai, wewe na uzao wako”.
Yeremia 21:8 “Nawe waambie watu hawa, Bwana asema hivi, tazama naweka mbele yenu njia ya uzima na njia ya mauti”.

   Katika kitabu cha Torati, Mungu anaapa (anazishuhudiza) kwa mbingu na nchi kuwa ametuwekea wanadamu njia mbili mbele yetu, ambazo ni uzima na mauti. Na kwa sababu Mungu ni pendo, anatushauri kuichagua njia ya uzima.

   Na siyo anatushauri tu, pia anatupa na sababu ya kwanini anatushauri kuchagua uzima, anasema ili uwe hai. Kuwa hai ni kupokea uzima wa milele, baada ya hukumu yenye kutisha ya Mungu yenye haki, siku atakapo tuhukumu wanadamu sawa sawa na matendo yetu.
Na katika kitabu cha Yeremia, Mungu anarithibitisha neno lake kuwa ameweka njia mbili mbele yetu; moja ni njia itupayo uzima na nyingine ni njia ya mauti. Ni juu yetu kuamua tunachagua na kuifuata njia ipi.

   Kuchagua njia ya uzima ni lazima kwanza uifahamu hiyo njia, ni ipi na unawezaje kuichagua na kuifuata. Njia ya uzima ni Yesu Kristo, kuchagua njia ya uzima ni kumchagua na kumpokea Yesu Kristo kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako. Na kuifuata njia ya uzima ni kutimiza na kutenda mapenzi ya neno la Mungu, kufuata na kushika neno la Yesu mwenyewe kwa matendo dhahiri.

Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba ila kwa njia ya mimi”.

   Ile njia ya uzima ambayo Mungu aliziapia mbingu na nchi kuwa ameiweka mbele yetu na kutushauri kuichagua na kuifuata hiyo, ndiyo hiyo inafunuliwa katika kitabu cha Yohana Mtakatifu. Yesu mwenyewe anajidhihirisha kuwa yeye ndiye njia, na siyo njia tu, ina uzima ndani yake amboyo kupitia hiyo tunaurithi Ufalme wa Mungu.

   Kuchagua njia ya uzima kunapaswa kuendane na matendo ya uzima, tusikiri kwa maneno ya vinywa vyetu kuwa tunao uzima (tumempokea Yesu Kristo) na wakati huo huo matendo yetu ni kinyume na kukiri kwetu.

Mathayo 3:8 “Basi zaeni matunda yapasayo toba”, matunda ni matendo na toba ni kuupokea uzima, sasa matendo yetu yanapaswa kuenenda kama jinsi tulivyoupokea huo uzima.
Cha kushangaza, Wakristo wengi wa siku hizi wanatenda kinyume na wanavyokiri katika vinywa vyao. Na kusababisha jina la Mungu litukanwe.

Tito 1:16 “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana”, kukiri kuwa umempokea Yesu Kristo na unahudhuria katika nyumba za ibada lakini matendo yako ni kinyume na kukiri kwako ni sawa na kupoteza muda!

   Kuchagua njia ya uzima na kutoifuata kwa matendo njia hiyo kunamadhara yafuatayo;

Kulitukanisha jina la Yesu; watu wanapoyatazama matendo yetu wanategemea kuona maisha yetu yakiakisi maisha halisi ya Yesu Kristo, na inapokuwa tofauti ndipo jina la Yesu linapotukanwa (2 Petro 2:2).

Kurithi mauti na kuzimu; kutotembea katika njia ya uzima ni kutembea katika njia ya mauti, na kutembea katika njia ya mauti ni kuchagua mauti (Mithali 12:28, 15:24).

Njia utakayopita katika uhai wako ndiyo njia utakayo iendea baada ya kifo, ikiwa umechagua njia ya uzima lakini unapita katika njia ya uovu basi baada ya kifo pia utaiendea njia uliyokuwa ukiipitia. Hapa haijarishi ni dua, swala au maombi mengi kiasi gani utafanyiwa wakati wa mazishi yako.

 Unachochagua kuishi ndicho utakacho tunukiwa.
Mathayo 16:27 “… ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake”, kila mmoja wetu atalipwa kwa kadiri ya alivyotenda alipokuwa hai na siyo kwa kadiri ya sala za kumuombea awekwe pema peponi (Yohana 5:28-29).

Kama umechagua njia ya uzima, tembea katika njia ya uzima maisha yako yote kwa uaminifu.

Sunday, November 25, 2012

FANYA AGANO NA MUNGU KUPITIA SADAKA.

   Kutoa sadaka kama mazoea au desturi ni kupoteza fedha au mali yako pasipo na manufaa yoyote. Wapo wakristo ambao wamelelewa katika familia za dini na kukua wakijua ni lazima kwenda na sadaka ibadani lakini hawajui umuhimu na matunda wanayoweza kuyapata kwa kutoa sadaka. Wakristo wa namna hii ni kama watoto ambao wanapewa sadaka na wazazi wao, wakitoa au wasipotoa sadaka hiyo hawaoni mapungufu yoyote, zaidi ni faida kwao kwani watakula barafu.

   Na wapo wakristo wanaotoa sadaka kama ajali, wao huamua ni sadaka ya aina au kiasi gani watatoa muda mfupi baada ya kujianda kwenda ibadani au hata wakiwa njiani kuelekea ibadani. Wanatoa sadaka za kushtukiza, sadaka isiyo na maandalio yoyote.

   Sadaka inapaswa kuandaliwa, hata siku moja kabla ya kutolewa. Katika agano la kale utaona kuna siku zinapita tangu Mungu aombe kutolewa kwa sadaka na siku ya kuitoa hiyo sadaka, aliyeambiwa atoe sadaka anafanya maandalizi ya kuchagua sadaka nzuri ya kupendeza itakayopata kibali machoni pa Mungu.

   Sadaka utakayoitoa madhabahuni pa Mungu lazima uitamkie jambo. Kabla sijatoa sadaka yangu huwa namwambia Mungu hivi; “maadam, sadaka/dhabihu hii itafanya kazi shambani mwako ee Mungu wangu, fanya jambo (ninalitaja) katika maisha yangu”.
   Sadaka au dhabihu ni sawa na mbegu, ukipanda mbegu unategemea uzune kulingana na mbegu uliyoipanda. Sadaka au dhabihu ni mbegu ya kuvunia baraka zote za kiroho na kimwili, afya na uzima.

   Zaburi 50:5 “Nikusanyieni wacha Mungu wangu, Waliofanya agano nami kwa dhabihu (sadaka).
Agano ni makubaliano yasiyovunjika, kufanya agano na Mungu ni kujithibitishia makubaliano yako na Mungu kuwa yatatimia. Sasa unaweza ukafanya agano na Mungu kwa kutumia dhabihu au sadaka unayoitoa katika ibada zako, sadaka iliyoandaliwa na siyo sadaka ya kutolewa kama bahati mbaya. Agano hilo utalifanya pale utakapo itamkia neno sadaka unayoipeleka madhabahuni pa Mungu wako, ukitoa sadaka ambayo hukuitamkia neno utakuwa unatoa sadaka kama mtoto asiyejua nini maana ya sadaka na inatolewa kwa sababu gani.

Sunday, November 18, 2012

UPENDO.


   Upendo wa kweli ni kumpenda mtu yule anayekuchukia, siyo kwa sababu ya mali au vitu alivyonavyo bali kwa sababu moyo umeamua kumpenda.

Jambo hilo ni gumu sana kwa wengi wetu, kwani tunawapenda wanaotupenda tu na hata kukawa na msemo unaosema “mpende akupendaye, asiyekupenda achana naye”. Tabia hii imeingia hadi makanisani, upendo wa wapendwa wengi wa siku hizi ni kupendana wao kwa wao tu, kusaidiana wao kwa wao tu na hata kutembeleana ni wao kwa wao tu. Huu siyo upendo aliotufundisha Bwana Wetu Yesu Kristo, ni kosa!

Kama wewe ni mkristo au siyo mkristo na unampenda mtu kwa sababu ana kitu au mali inayokunufaisha kwa namna moja au nyingine, bado hauna upendo. Kwa sababu mtu huyo akiondokewa na hicho kinachokufanya umpende, upendo wako kwake utayeyuka wote.

Upendo ni nini?
 Mathayo 5:44 “lakini Mimi (Yesu Kristo) nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi”.

Upendo ni kuwapenda watu wote; rafiki zetu na adui zetu, na kuwaombea pia wapate mema na siyo mabaya.

Wakristo wa siku hizi ili wakuombee basi ni lazima yawe maombi ya kanisa kwa ujumla, au kuwe na jambo zuri umetenda kwa manufaa na faida yao. Ukimpa zawadi ya kitu au pesa, atakuombea Baraka hata kufunga atafunga. Lakini asipopewa kitu, mkristo huyu hana muda wa kukuombea. Huo siyo upendo tulioagizwa na Bwana wetu Yesu Kristo. (Luka 6:27)

Upendo huu ni kuwapenda watu wote kama nafsi zetu; kama vile tunavyojipenda sisi wenyewe ndivyo tuwapende na wenzetu.
Mathayo 19:19 “…mpende jirani yako kama nafsi yako”.
Kama wewe ukilala njaa siyo kwa sababu upo katika maombi ya kufunga, bali kwa sababu umekosa chakula utakavyoumia ndivyo uumie vile vile ukisikia jirani yako amelala njaa pasipo kujali kuwa ni mkristo mwenzako au siyo mkristo, ni rafiki yako au adui yako. Huu ndiyo upendo wa Yesu Kristo, tena ni amri (Marko 12:31).

Nini faida za upendo?
Sadaka pasipo upendo haifai kitu. Ukikosa upendo kwa jirani yako yoyote, sadaka unayoitoa madhabahuni si kitu. Upendo unafaa kuliko sadaka unayoiona ni nono, au inayogusa moyo wako.
Marko 12:33 “…na kumpenda jirani kama nafsi yako, kwafaa kuliko sadaka nzima za kuteketezwa na dhabihu zote pia”.

Kutukamilisha. Kama jinsi Baba yetu wa Mbinguni alivyomkamilifu kwa sababu alimtoa Yesu Kristo afe ili kutukomboa kwa sababu anatupenda, na sisi tukiwapenda wenzetu wote tunakamilishwa kama Mungu mwenyewe alivyo mkamilifu.
Mathayo 5:45,48 “ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”.

Pendo litawavuta wasiomjua Mungu, wamjue Mungu. Tukiwapenda wote; wakristo na wasio wakristo, frafiki zetu na adui zetu, tunamtambulisha Mungu wetu mwenye upendo kwa watu wote kwao. Na kwa njia hii ya upendo huu wa dhati, tunawafanya wasiomjua Mungu nao wamjue Mungu kupitia upendo wetu kwao.

Upendo wa namna hii hauji ila kwa neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, na endapo umekosa upendo huu siyo kosa kwani unaweza kuupata sasa. Yesu mwenyewe alisema, ombeni lolote mtakalo kwa jina langu na Baba wa mbinguni atawapa. Kama umekosa upendo aliotuagiza Yesu, omba na kwa imani Mungu wetu atakupa.
Yohana 14:13 “Nanyi mkiomba lolote (upendo) kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana”.

Mungu aliyetukuka, mtakatifu awabariki wote.


Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts