Wednesday, March 12, 2014

HATUA ZA KUUKULIA WOKOVU NA NEEMA YA MUNGU



 Tangu kutungwa kwa mimba hadi mtoto anapozaliwa, kuna hatua mbali mbali za ukuaji na majina ya hatua hizo hutofautiana kutoka hatua moja hadi hatua nyingine. Inapotokea mtoto amezaliwa, lakini haongezeki kimo, uzito, ufahamu licha ya kuongezeka kwa idadi ya miaka, hicho ni kiashilia tosha kuwa mtoto huyo ana matatizo ya ukuaji kiafya. Ni lazima wazazi wa mtoto huyo watafute msaada wa kitabibu haraka sana iwezekanavyo.

Katika ulimwengu wa kiroho pia, mtu yoyote anapompokea Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wa maisha yake, anakuwa amepokea wokovu. Wokovu unalingana na ukuaji wa mwanadamu, ni lazima mtu huyu aukulie wokovu na neema ya Mungu kutoka hatua ya kwanza kabisa hadi kufikia hatua ya mwisho ambayo ni ufufuo wa uzima wa milele.

Katika somo letu hili lenye kichwa, “hatua za kuukulia wokovu na neema ya Mungu”, tutajifunza hatua kuu tatu ambazo mtu aliyeokoka ni lazima azipitie. Ni maombi yangu kwamba, Roho Mtakatifu akufundishe kwa utulivu na undani ili upate kuelewa na kujitambua uko hatua ipi na unatakiwa kwenda hatua ipi, na ufanye nini ili kuifikia hatua iliyopo mbele yako.

Hatua za kuukulia wokovu na neema ya Mungu, nimezigawa katika hatua kuu tatu ambazo zina hatua nyingine ndogo ndogo ndani yake kulingana na vile Roho Mtakatifu alivyonijalia;

Kuamini na kuokoka

Kumjua Mungu, kumjulisha Mungu kwa wengine na Mungu kukujua wewe

Kufanyika rafiki wa Mungu

1. KUAMINI NA KUOKOKA

(a). kuamini
Marko 16:16, aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini atahukumiwa
Yohana 3:16, kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu (mwanadamu), hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele (wokovu)
Katika mistari miwili hiyo hapo juu, kuna kitu tunajifunza. Kitu hicho ni lazima kuamini ndipo wokovu upatikane. Kwa sababu hiyo huwezi kupata wokovu pasipokumuamini Mungu na Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wa maisha yako.

Siyo kila mtu anayemjua Mungu na Yesu Kristo, anamuamini Mungu na Yesu Kristo. Na siyo kila anayemuamini Mungu anamuamini na Yesu Kristo. Na ndiyo sababu siyo wanadamu wote tunaolisikia neno la Mungu tumeokoka.

Kwa sababu hiyo, ni lazima mtu aamini kuwa Mungu yupo, anaishi milele, Yesu Kristo ni mwana wa Mungu (Mathayo 16:16, Luka 1:35), aliyekufa msalabani na kufufuka ili atuokoe (Mathayo 26:28).
Na siyo kuamini tu Mungu yupo, ni lazima ijulikane kuwa Mungu unayemuamini ni Yehova (ndilo Jina lake), tena anaishi milele. Ninasema hivi kwa sababu, hata wanaoabudu sanamu, wanyama au miti mikubwa nao pia wana Imani kuwa hivyo vitu wanavyoviabudu ndiyo miungu yao.

(b). kuokoka
Kuokoka ni kuamini kuwa Yesu Kristo ni Bwana na Mwokozi wa maisha yako, kukiri kwa kinywa imani hiyo na kubadilika kutoka kuishi maisha ya dhambi na kuishi maisha matakatifu ya kupendeza Mungu.

Kwa maana hiyo, imani peke yake haitoshi kumpa mtu wokovu, ni lazima aikiri imani hiyo kwa maneno ya kinywa chake pasipo kulazimishwa au kushawishiwa (Warumi 10:9)

Haitakiwi mtu apate wokovu kwa kulazimishwa au kushawishiwa; kwa mfano mtu anaamua kuokoka ili amuoe au aolewe na mtu fulani aliyeokoka. Wengi wa watu wa aina hii hawawezi kuukulia wokovu kwa viwango vinavyostahili, kwa sababu hawakuokoka ili kumpokea Yesu Kristo bali waliokoka ili wampate mtu fulani. Wengi wao wanakuwa na wokovu wa kifafa.

(c). Hatua za kuokoka
(i). kuisikia injili ya Yesu Kristo
Ni lazima uisikie injili ya Yesu Kristo kwanza ili upate kumjua Mungu na Yesu Kristo kisha ujenge Imani itakayo kupelekea kuupata wokovu (1 Petro 1:23, Marko 16:15-16).

(ii). Kuamini
Baada ya kuisikia injili, kinachofuata ni kujenga imani ya ile injili uliyoisikia (Wagalatia 3:26). Na hapa ndipo penye tatizo, kama umeisikia imani potofu basi utakuwa ukiamini na kuabudu watu, vitu, wanyama; vitu visivyo Mungu wa kweli aliye hai. 

Kwa sababu hiyo, kabla ya kuamini ni vema ukachunguza ni Mungu yupi anayehubiriwa hapo, siyo kila mungu anayehubiriwa anastahili kuabudiwa. Ni Mungu mmoja tu ndiye anayestahili kuabudiwa, jina lake Yehova ambaye kupitia Yesu Kristo tunapata wokovu na uzima wa milele.

(iii). Kuokoka
Baada ya kuisikia injili ya Yesu Kristo, unapata Imani ya injili uliyoisikia, hatua inayofuata ni kuokoka kwa kuikiri imani uliyoisikia na kufanyika mwanafunzi wa Yesu Kristo ukiacha njia zote ovu na kufuata njia ya haki kama lisemavyo neno la Mungu (Warumi 10:10).

(d). Imani ni lazima ikue au iongezeke
Baada ya kuamini na kupokea wokovu, hutakiwi kubaki pale pale kama jinsi siku ya kwanza ulipoamini na kuokoka ulivyokuwa. Unatakiwa kuilinda imani na wokovu wako, na imani yako ni lazima ikue au iongezeke, kutoka kiwango hadi kiwango, kutoka chini kupanda juu (2 Korintho 10:15 na 2 Thesalonike 1:3).

Mpendwa msomaji wangu ni imani yangu kuwa kuna kitu kipya Roho Mtakatifu amekufundisha, usikose sehemu ya pili ya somo hili. Mungu akubariki sana, na akubariki zaidi kwa kushiriki na wengine masomo haya. Amina. 

Friday, January 3, 2014

FIVE TIPS ON WEALTHY AND PROSPERITY FOR THE YEAR 2014.

1. Does not depends on how big your salary is, BUT it depends on how much you save for the future.

2. Does not depends on how many liabilities you possess, BUT it depends on how many assets you possess.

3. Does not depends on how many products you are marketing, BUT it depends on how worthy and quality your products are.

4. Does not depends on how much you spends for luxuries, BUT it depends on how wise you spend your money to make money.

5. Does not depends on how much money and expensive assets you possess, BUT it depends on how you are willing with loving heart in helping people in needs (poor people).
"HAPPY PROSPEROUS NEW YEAR, 2014"

Friday, December 6, 2013

MANUNG’UNIKO HUGEUZA BARAKA ZA MUNGU MAISHANI MWAKO NA KUWA LAANA



Manung’uniko ni dalili ya kukata tamaa na kukiri kukosa tumani la jambo au hali ngumu anayoipitia mtu. Japokuwa mtu huyo anaweza asikiri kukata tamaa kwa kinywa chake, lakini kwa kupitia manung’uniko anakiri kukata tamaa na kukosa msaada japo siyo kwa ukiri wa moja kwa moja.
Katika maisha ya kiroho haipaswi kunung’unikia hali ya maisha au majaribu unayopitia, hasa haipaswi kumnung’unikia Mungu. Kwa sababu, kama nilivyokwisha kueleza hapo mwanzo, manung’uniko ni dalili ya kukiri kukata tamaa na kukosa mwelekeo.

Ni afadhari ujilaumu na kujinung’unikia nafsi yako wewe mwenyewe na siyo kumnung’unikia Mungu. Mtumishi wa Mungu, Ayubu alipofikwa na jaribu zito la kupotelewa na watoto, wanyama na kupata ugonjwa mbaya wa ajabu hakuthubutu kumlaumu au kumnung’unikia Mungu kwa kinywa chake au kwa moyo wake. Hebu tuangalie maandiko yafuatayo;

Ayubu 1:20. Ndipo Ayubu akainuka akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake,  na kuanguka na nchi na kusujudia; akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, name nitarudi tena huko uchi vile vile; Bwana alitoa na Bwana ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe. Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.
Ni neno la kuajabisha sana, baada ya Ayubu kupata habari ya kupotelewa watoto wake wote na mali yake yote, alirarua joho lake, akanyoa kichwa chake, akaanguka na kusujudu.  Kwa kurarua joho lake na kunyoa kichwa chake alionesha utii na unyenyekevu mbele za Mungu. 

Ayubu alionesha utii kwa Mungu kwa sababu alijua, watoto wake na mali zake alivipata kwa sababu Mungu alimbariki vitu hivyo. Na ndani ya moyo wake, Ayubu alimsujudia Mungu kwa sababu huyo ndiye aliyebaki naye, na Mungu ndiyo tumaini na msaada wake tu.

Ayubu 3:1. Baada ya hayo Ayubu akafunua kinywa chake, na kuilaani siku yake.
Ilipofikia wakati moya wa Ayubu ulipotaka kunung’unika na kusononeka, Ayubu aliona ni vema ailaani siku yake ya kuzaliwa lakini hakuthubutu kumlaani au kumnung’unikia Mungu wa mbinguni aliyemuumba.

Unapomnung’unikia au kumlaani Mungu kwa mambo magumu unayoyapitia au unayokutana nayo katika maisha yako, unafanya kosa kubwa sana. Ni busara endapo utamuuliza Mungu nini makusudi ya mapito haya, ili kama ni vita dhidi ya shetani, Mungu atakuelekeza jinsi ya kuvipigana na kwa Jina la Yesu Kristo utashinda kwa ushindi mkubwa.
Hebu tuangalie neno la Mungu (kutoka kinywani mwa Bwana) linasemaje kuhusu manung’uniko;
Hesabu 14:26-38. 26. Kisha Bwana akanena na Haruni na Musa na kuwaambia, 27. Je nichukuliane na mkutano mwovu huu uninung’unikiao hata lini? Nimesikia manung’uniko ya wana wa Israeli, waninung’unikiayo. 28. Waambieni, kama niishivyo, asema Bwana, hakika yangu kama ninyi mlivyonena masikioni mwangu, ndivyo nitakavyowafanyia ninyi; 29. Mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili,
30. Hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.
34. kwa hesabu ya hizo siku mlizoipeleleza ile nchi, yaani, siku arobaini, kila siku kuhesabiwa mwaka, mtayachukua maovu yenu, ndiyo miaka arobaini, nanyi mtakujua kufarikana kwangu.

Katika kifungu hicho cha Biblia hapo juu tunajifunza vitu vikuu vipatavyo vine, navyo ni kama vifuatavyo;

Manung’uniko ni uovu mbele za Mungu
“Nichukuane na mkutano mwovu huu uninung’unikiao hata lini?”, maneno hayo ya Mungu yanapatikana katika Hesabu 14:26. Maneno na mawazo yanayoambatana na manung’uniko ndiyo hufanyika uovu mbele za Mungu. Watu wengi wanapo nung’unika hutamka maneno au huwaza mawazo ya kumlaani Mungu, na wakati mwengine kuwalaani na kuwaumiza wengine. Hapo ndipo manung’uniko yanapokuwa ni uovu mbele za Mungu.

Na mara nyingi, manung’uniko yanaambatana na kukata tamaa, na kukata tamaa mar azote huwa ni chanzo cha kutenda dhambi kwa namna moja au nyingine. Kwa maana hiyo; manung’uniko huzaa kukata tamaa na kukata tamaa huzaa dhambi, dhambi ni uovu na chukizo mbele za Mungu.
Kwa mfano; mwanadamu anapo kata tamaa kutokana na ugumu wa maisha, hutafuta njia haramu ya kumuwezesha kuishi kama kufanya ukahaba, wizi na ujambazi, mauaji n.k. hayo yote huja baada ya mtu huyu kunung’unika kuhusu ugumu wa maisha, baada ya kukosa majibu hufikia kukata tamaa inayopelekea kuchukua maamuzi yasiyo sahihi ambayo ni dhambi na chukizo mbele za Mungu kama tulivyoona katika mfano hapo juu.


Manung’uniko husababisha kifo
“mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili”, Hesabu 14:29. Kuna aina mbili za vifo; kifo cha kimwili na kifo cha kiroho.
Maisha ya dhambi yanayotokana na kukata tamaa baada ya manung’uniko ya muda mrefu, hupelekea kifo cha kimwili na kiroho. Kifo cha kiroho ni kurudi nyuma baada ya kupokea wokovu wa Yesu Kristo, unapoishi maisha ya dhambi unakuwa umerudi nyuma kiroho au umeanguka dhambini. Na kifo cha kimwili hufuatia kama matokeo ya maisha ya dhambi unayoyaishi.

 Haimaanishi wasiotenda dhambi hawafi, la hasha, bali maisha ya dhambi humpeleka mtu kaburini pasi na umri timilifu (Ayubu 5:26, Ayubu 42:16-17). Yohana 8:21(b), nanyi mtakufa katika dhambi yenu. Kama tulivyoona hapo juu; manung’uniko huzaa kukata tamaa, kukata tamaa huzaa dhambi na dhambi huzaa kifo, kinachoweza kuwa cha kiroho au cha kimwili.


Kutofikia au kutotimiza malengo yako au makusudi ya Mungu katika maisha yako
“hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo”, Hesabu 14:30.
Hayo yalikuwa ni maneno ya Mungu kwa wana wa Israeli, na kama tulivyoona hapo juu; manung’uniko husababisha kukata tamaa na kukata tamaa husababisha kutenda dhambi na dhambi hupelekea mauti ya kiroho au ya kimwili au vyote kwa pamoja.

Unapokufa kiroho, unauwa makusudi ya Mungu katika maisha yako. Na Mungu asivyo na hasara wewe mmoja unaporudi nyuma, anainua jeshi kubwa la watu kumtumikia. 

Yesu Kristo alipoambiwa awatulize wanafunzi wake waliokuwa wakimsifu, na Mafarisayo; alijibu; “Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele”, hapo Yesu alikuwa akitufundisha kuwa, tunapokata tamaa na kuuwa huduma zetu, Mungu anainua watu wengine ili kuiendeleza kazi yake. Kazi ya Mungu haifi hata siku moja, ukizira wewe, atafanya mwingine, maadam utukufu umrudie Mungu.

Aidha unapokuwa na malengo katika maisha yako, kunung’unika kunakopelekea kukata tamaa inayosababisha dhambi na hatimaye kifo cha kimwili, kunazima malengo yako na kufuta kabisa ndoto zako maishani. Na kusababisha kizazi chako kifuatacho kurithi laana zako, isipokuwa kitatubu na kutakaswa kutoka katika vifungu na maisha ya laana.


Manung’uniko huchelewesha makusudi ya Mungu au mafanikio yako katika maisha
“kwa hesabu ya hizo siku mlizoipeleleza ile nchi, yaani, siku arobaini, kila siku kuhesabiwa mwaka”, Hesabu 14:34
Wana wa Israeli waliipeleleza nchi ya ahadi kwa muda wa siku arobaini, waliporudisha habari ya nchi hiyo ndipo walipomlalamikia na kumnung’unikia Mungu na kusema ingekuwa heri kama wangalikufa katika nchi ya utumwa ya Misri ama wangalikufa jangwani (Hesabu 14:1-3).

Hata wewe mpendwa msomaji wangu, inawezekana uko katika wakati mgumu, unapitia majaribu mazito unayodhani huwezi kuyavuka. Unafikia hatua unakata tamaa, unamlaumu Mungu kwa nini alikuumba, ni heri ufe sasa. 

Ninakwambia sasa, acha kumlaumu Mungu, acha sasa kumlaani Mungu, acha kukata tamaa, usithubutu kurudi nyuma, kwa Jina la Yesu Kristo, yupo Mungu ili akusaidie na utasema hakika wewe Mungu umekuwa ni Ebeneza kwangu.

Ikiwa Mungu anayo makusudi na maisha yako, mafanikio yako au baraka zako ni lazima akupitishe katika kipimo cha uvumilivu na uaminifu, unapofuzu mtihani huo ndipo Mungu anapoachilia kibari katika maisha yako, huduma yako na baraka zako.

Nataka nikupe angalizo katika somo hili; siyo kila mtihani au magumu unayopitia ni makusudi ya Mungu. Muulize Mungu nini chanzo, sababu na makusudi ya hali unayopitia.

Ikiwa ni uonevu wa ibilisi, mwambie Mungu akupiganie na akupe kuyashinda yote katika Jina la Yesu Krsito.

Ikiwa ni makusudi ya Mungu upitie hatua uliyopo sasa, imekupasa kuvumilia yote, usilalamike, usinung’unike, usikate tamaa wala usimlaani Mungu. Simama imara kuitetea imani yako.
Tukichukua mfano wa wana wa Israeli, Mungu aliwapitisha jangwani katika hali ngumu kwa makusudi maalumu;

Kutoka 7:16. “Nawe umwambie, Bwana, Mungu wa Waebrania, amenituma nije kwako, kusema, wape watu wangu ruhusa, ili wapate kunitumikia jangwani”,
Mungu hakuwapitisha wana wa Israeli jangwani kwa bahati mbaya, aliwapitisha kwa makusudi maalumu. Kumbuka Mungu aliahidi kuwapa nchi yenye maziwa na asali (nchi ya ahadi), ili kuifikia ile nchi, iliwapasa kupitia mtihani mzito jangwani.

Kule kuenenda kwao jangwani; kwa kumsifu Mungu aliyewatoa utumwani na sasa anakwenda kuwapa nchi ya ahadi au kwa kumlalamikia na kumnung’unukia Mungu, ndiko kuliamua ni nani ataingia na nani hataingia katika nchi ya ahadi.

Na hii ni kwako pia mpendwa mwenzangu, vile unavyomuona Mungu katika mtihani unaoupitia ndio kunaamua ni jinsi gani utafikia ahadi ya ukombozi ya Mungu iliyopo mbele yako. Ikiwa unamlalamikia, unamlaani Mungu au unakata tamaa, ni dhairi utashindwa kufikia baraka na mafanikio yako ambayo Mungu ameyaweka mbele zako baada ya kuimaliza safari ya mtihani unaoupitia, ama utaifikia kwa wakati wa kuchelewa hadi hapo Mungu atakapojiridhisha kuwa umekomaa.

Hebu tuangalie neno la Mungu kuhusu mitihani tunayoipitia; “Amri hii ninayokuamuru leo mtaishika kuitenda, mpate kuishi na kuongezeka, na kuingia katika ile nchi amabayo Bwana aliwaapia baba zenu; nanyi mtaimiliki. Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako, aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu, kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo”, Kumbukumbu la Torati 8:1-2.

Nikupe mfano mfupi; matajiri wengi wanaotumia fedha na mali zao kuwatunza yatima na maskini, historia ya maisha yao ni watu waliotokea katika hali ngumu sana za kiuchumi. Mungu anapo wabariki na kuwapa mali, anawakumbusha kule walikotokea kisha anaweka mzigo wa watu hao kumtumikia Mungu kwa kutumia fedha na mali zao katika kuwatunza yatima na maskini.

Ili Mungu akubariki baraka za kiroho ni lazima akupitishe katika mtihani wa kukataliwa, watumishi wakubwa unaowaona leo kuna kipindi kigumu walichokipitia hata kufikia hapo unapowaona wamefika na unapotamani na wewe ufikie. Wapo wachungaji walioanza kanisa na watu wa familia zao tu kwa miaka kadhaa kabla hawajafikia kuwa na wafuasi zaidi ya miatano.

Na wapo wahubiri wakubwa ambao wakihubiri maelfu ya watu wanaokoka, walianza kwa mikutano ambayo walihubiri na hakuna mtu hata mmoja aliyeokoka.

Nataka nikwambie, hawakukata tamaa, hawakumlaumu wala kumnung’unikia Mungu, bali waliendelea kumtukuza, kumuhimidi na kumtumaini Mungu katika huduma zao.

Vivyo hivyo, ili Mungu akubariki baraka za kimwili kama fedha na mali, ni lazima akupitishe katika mtihani wa dhiki ya kukosa fedha na mali. Ili akupie moyo wako una mtazamo gani kumuelekea Mungu. Ikiwa unakata tamaa, unamnung’unikia Mungu, ujue hutafikia baraka ambazo Mungu ameziweka mbele yako, na ikiwa kwa neema ya Mungu utazifikia baraka hizo, basi utachelewa sana.

Katika kumalizia, ninataka nikutie nguvu mpendwa, usikate tamaa, usimlaumu wala usimnung’unikie Mungu. Simama imara katika mtihani unaoupitia, yupo Mungu jina lake anaitwa Yehova, atakusaidia na kukutetea ikiwa tu utamtumainia na kumtegemea yeye. Hakika upo ushindi na baraka baada tu ya kuumaliza mtihani wako, usithubutu kurudi nyuma kiimani na kumuacha Mungu na wala usithubutu kukata tamaa ya maisha, shindig upo, katika Jina la Yesu Kristo. Amina.

Kudownload somo hili katika PDF, bonyeza HAPA

Saturday, October 12, 2013

KWANINI YESU KRISTO ALIPOTAKA KWENDA FARAGHA, KATIKA MAOMBI, AU ALIPOAMUA KUFANYA JAMBO LA KIPEKEE ALICHAGUA KUAMBATANA NA PETRO, YOHANA NA YAKOBO?



 Ukiyachunguza maandiko katika vitabu vya Biblia vya Injili zile nne; Injili ya Mathayo, Marko, Luka na Yohana utakutana na vifungu vingi vikionesha jinsi Bwana wetu Yesu Kristo alivyopenda kuambatana na Petro, Yohana na Yakobo.

Na alipenda kuambata na wanafunzi wake hao watatu; Petro, Yohana na Yakobo sehemu muhimu au katika shughuli muhimu. Kwa mfano, alipotaka kwenda faragha kwa maombi au alipoamua kufanya jambo la uponyaji lililohitaji imani kubwa.

Kuna sababu nyingi sana zilizomfanya Bwana wetu Yesu Kristo apende kuambatana na wanafunzi wake hao watatu katika faragha na sehemu muhimu mbali mbali.

Petro, Yohana na Yakobo richa ya kwamba walikuwa ndugu (Yakobo na Yohana - Mathayo 4:21) na marafiki (Marko 13:3, Matendo ya Mitume 3:1) walikuwa wana sifa za pamoja zinazofana na sifa za kila mmoja wao, ambazo kwa umoja wao walitengeneza timu iliyompendeza Yesu Kristo.

Hebu tuangalie baadhi ya vifungu vinavyo thibitisha kuwa Bwana wetu Yesu Kristo alipenda kuongozana zaidi na Petro, Yohana na Yakobo kwa maombi ya faragha au katika jambo la kipekee na umuhimu zaidi.

Mathayo 17:1. Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu yam lima mrefu faraghani (kwa maombi).

Marko 1:29. Na mara walipotoka katika sinagogi, walifika nyumbani kwa Simoni na Andrea, pamoja na Yakobo na Yohana. Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia (Yesu Kristo) habari zake.  (Yesu Kristo) Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia.

Marko 5:37. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo.

Luka 22:8. Akawatuma Petro na Yohana, akisema, Nendeni, mkatuandalie pasaka tupate kuila.

Marko 14:32-33. Kisha wakaja mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa muda niombapo. Akamtwaa Petro na Yakobo na Yohana pamoja naye, akaanza kufadhaika sana na kuhangaika.

Wednesday, August 21, 2013

HATUA NNE ZA KUPATA AMANI YA MOYO NA NAFSI (INNER PEACE).




Msongo wa mawazo na ukosefu wa amani moyoni na/au nafsini imekuwa ni tatizo linaloongezeka kwa kasi na kuwapata watu wengi sana. Na ubaya ama ugumu wa tatizo hili ni kwamba linagundulika baada ya matokeo ya ukosefu wa amani moyoni au nafsini na msongo wa mawazo.

Yaani ni hivi; watu wengi wasio na amani moyoni na nafsini huishi maisha ya kuigiza  na huwa vigumu sana kuwatambua watu hao, unaweza kumtambua mtu mwenye msongo wa mawazo kwa tabia yake ya kujitenga na kutoshirikiana na watu. Lakini unaweza usimtambue mtu asiye na amani moyoni au nafsini kwa sababu wengi wa watu hawa huvaa sura zenye tabasamu na furaha wawapo mbele za watu.

Ni watu wanaoyabeba maumivu yao wao wenyewe na kujaribu kutafuta suluhisho pasipo kuwashirikisha watu wengine. Na ndipo utakaposhangaa kuona mtu fulani amefanya jambo usilolitegemea alifanye, kwa mfano; kuua au kujiua wao wenyewe, kutukana matusi, au kufanya jambo la hatari ilihali anajua madhara yake pasipo kujihadhari.

Ndiyo, matokeo ya ukosefu wa amani moyoni au nafsini pamoja na msongo wa mawazo matokeo yake siku zote huwa ni hasara au maumivu kwa muhusika au watu wanao mzunguka. Wengi hutafuta njia za kutua mizigo iliyomo mioyoni na nafsini mwao kwa njia za mkato ambazo wengi hudhani kujiua au kuwaua wale wailowasababishia maumivu hayo ndiyo jibu sahihi.

Kuna nyakati ukosefu wa amani ya nafsi au moyo kunaambatana na chuki na visasi, yaani muhusika hubebea chuki na/au visasi dhidi ya mtu au watu waliomsababishia maumivu hayo. Kubeba chuki na visasi vya muda mrefu ndani ya mioyo na nafsi zilizokosa amani hupelekea matatizo ya kiafya kama shinikizo la damu (hypertension), mshituko (stroke), kupooza (paralysis) na hata kuzeeka mapema (early aging). Hii hutokea kwa watu ambao wana msongo wa mawazo, wamekosa amani moyoni na nafsini na huku wamebeba mizigo ya chuki na visasi dhidi ya watu wasioweza kuwalipia hicho kisasi.

Sisemi inatupasa kubeba chuki na visasi mioyoni na nafsini mwetu, hiki ni kitu kinachotupata nje ya uwezo wetu (involuntary action). Na kama jinsi tumekosa amani mioyoni na nafsini mwetu pasipo kupenda sisi wenyewe, ndivyo ilivyo ni vigumu kuitafuta amani ya nafsi na mioyo yetu sisi wenyewe pasipo msaada wowote.

Ni lazima utafute msaada, na msaada pekee na wa kuaminika ni Mungu (Yehova) peke yake. Ndiyo, kuna wanasaikolojia waliobobea ambao wanaweza wakakusaidia, lakini msaada wa Mungu kupitia Yesu Kristo ndiyo una uhakika wa asilimia mia moja (100%).

Sunday, July 21, 2013

UNAWEZA KUWA UNATEMBEA CHINI YA LAANA PASIPO WEWE MWENYEWE KUJUA.



YESU KRISTO ASIFIWE!

Ashukuriwe Mungu aliyetupa kibali cha mimi na wewe msomaji wangu kukutana leo ikiwa ni kwa mara ya kwanza au kwa mara nyingine tena. Leo tuna somo lenye kichwa kisemacho “UNAWEZA KUWA UNATEMBEA CHINI YA LAANA PASIPO WEWE MWENYEWE KUJUA”, katika somo hili tutaangalia kwa undani mambo yafuatayo:-


  • Maana ya laana.

  • Laana inaletwa/sababishwa na nani?

  • Kwa nini ulaaniwe?

  • Je, unaweza kuwa umelaaniwa pasipo wewe kujua?

  • Ni vitu gani vinaweza kulaaniwa?

  • Kuvunja laana na mikosi, kuomba baraka za Mungu (Yehova).

Hili ni somo zuri sana ambalo ukilifuatilia kwa ukaribu zaidi na ukijenga imani kwa Mungu kuna vitu (laana), Mungu anakwenda kuzivunja, kuzifuta na kuziharibu (1 Yohana 3:8) na kuyabadilisha maisha yako kabisa. Unakwenda kuishi maisha ya baraka na ushindi, nakuhakikishia lazima utazishuhudia baraka za Mungu katika maisha yako baada ya kumaliza somo hili.

Maana ya laana.
Laana ni bahati mbaya au maneno mabaya ya maapizo yanayotamkwa kumuelekea mtu fulani yeye mwenyewe au kitu fulani kinachomuhusu, kwa mfano; kazi, shamba, watoto, masomo n.k kwa makusudi ya kumdhuru mtu huyo au kitu kinachomuhusu. Kwa kifupi laana ni kinyume cha baraka.

Laana inaweza ikasababishwa kwa makusudi maalumu (mfano: laana ambayo ni matokeo ya dhambi za wanadamu) au pasipo kujua (mfano: laana ya kujitamkia sisi wenyewe), kwa njia zote hizi mbili laana inafanya kazi iwe kwa makusudi au pasipo kujua.

Laana, ili itende kazi ni lazima iwe imeunganishwa na nguvu fulani zisizo za kawaida, nguvu za ziada “supernatural powers”,  nguvu hizo ni lazima ziwe zinazidi nguvu za mtu au kitu kinacholaaniwa. Nachomaanisha hapa ni kwamba, mdogo hawezi kumlaani mkubwa; shetani hawezi kumlaani Mungu, na mtu aliyesimama katika kweli na haki ya Mungu hawezi kulaaniwa na shetani kutokana na ile nguvu ya Mungu iliyomo ndani yake.

Kwa maana hiyo, kwa maneno yetu wenyewe au ya watu wa karibu nasi na matendo ya maisha yetu ndiyo sababu kubwa ya laana katika maisha yetu na vizazi vyetu vijavyo. Kwa sababu kila tunachokitamka na tunachokitenda kinafuatiliwa kutimilizwa na falme mbili tofauti; ufalme wa Mungu na ufalme wa shetani. Ni hakika na kweli, ufalme wa shetani hufuatilia hasa mambo ambayo ni hasi kuyatimiliza katika maisha yetu, kuwa mwangalifu sana.

Monday, July 15, 2013

HII SI YA KUKOSA!!!

Nakusalimu kwa Jina la Yesu Kristo!

Natumaini u mzima wa afya, kama mimi nilivyo mzima pia, shukrani zimrudie Mungu mwenyewe anayetupa uhai bure.

Kuanzia jumapili ya tarehe 21/07/2013, tutaanza somo jingine lenye kichwa kisemacho;

"UNAWEZA KUWA UNAISHI NA LAANA PASIPO WEWE MWENYEWE KUJUA"

ni somo zuri sana, lenye pumzi ya Mungu. na kupitia somo hilo, Mungu anakwenda kukutoa mahali ulipo ambapo haustahili kuwepo na anakuinua na kukuketisha meza moja na wafalme, kwa kifupi utakwenda kuziona baraka za Mungu zakianza kufuatana na wewe kwani laana na mikosi yote inakwenda kuvunjwa na wewe kuwekwa huru, katika jina la Yesu Kristo, Amina.

Katika somo hilo tutakwenda kuangalia kwa undani zaidi mambo yafuatayo:-

  1. maana ya laana
  2. laana inaletwa/sababishwa na nani?
  3. kwanini ulaaniwe?
  4. vitu gani vinaweza kulaaniwa katika maisha yako?
  5. je unaweza kuwa umelaaniwa pasipo wewe mwenyewe kujua?
  6. kuvunja laana na mikosi kwa Jina la Yesu Kristo.
Hivyo basi usithubutu kulikosa somo hili, mtaarifu na mwenzako ili Mungu akubariki sana kwa kushiriki katika kuutangaza ufalme wake.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts