Friday, December 7, 2012

NJIA UTAKAYOICHAGUA NDIYO NJIA UTAKAYOPITA.

   Mwanadamu wa kwanza aliumbwa katika ukamilifu; kiroho na kimwili, mtakatifu asiyejua dhambi na mwenye mwili usioonja mauti. Baada ya kuasi agizo la Mungu na kutenda dhambi, akapoteza ukamiliu wa utakatifu, lakini kwa vile Mungu ni pendo, anatupenda wanadamu akatuandalia ukombozi ili atununue kutoka katika ufalme wa giza na kutuingiza katika Ufalme wa Mwana wa pendo lake, Yesu Kristo.

   Lakini kuupokea ukombozi huo, ni hiyari ya mwanadamu mwenyewe, kwani baada ya kuitambua dhambi mwanadamu huyu alipata utashi wa kutambua wema na uovu (Mwanzo 3:7).
Kumbukumbu la Torati 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimeweka mbele yako uzima na mauti… basi chagua uzima ili uwe hai, wewe na uzao wako”.
Yeremia 21:8 “Nawe waambie watu hawa, Bwana asema hivi, tazama naweka mbele yenu njia ya uzima na njia ya mauti”.

   Katika kitabu cha Torati, Mungu anaapa (anazishuhudiza) kwa mbingu na nchi kuwa ametuwekea wanadamu njia mbili mbele yetu, ambazo ni uzima na mauti. Na kwa sababu Mungu ni pendo, anatushauri kuichagua njia ya uzima.

   Na siyo anatushauri tu, pia anatupa na sababu ya kwanini anatushauri kuchagua uzima, anasema ili uwe hai. Kuwa hai ni kupokea uzima wa milele, baada ya hukumu yenye kutisha ya Mungu yenye haki, siku atakapo tuhukumu wanadamu sawa sawa na matendo yetu.
Na katika kitabu cha Yeremia, Mungu anarithibitisha neno lake kuwa ameweka njia mbili mbele yetu; moja ni njia itupayo uzima na nyingine ni njia ya mauti. Ni juu yetu kuamua tunachagua na kuifuata njia ipi.

   Kuchagua njia ya uzima ni lazima kwanza uifahamu hiyo njia, ni ipi na unawezaje kuichagua na kuifuata. Njia ya uzima ni Yesu Kristo, kuchagua njia ya uzima ni kumchagua na kumpokea Yesu Kristo kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako. Na kuifuata njia ya uzima ni kutimiza na kutenda mapenzi ya neno la Mungu, kufuata na kushika neno la Yesu mwenyewe kwa matendo dhahiri.

Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba ila kwa njia ya mimi”.

   Ile njia ya uzima ambayo Mungu aliziapia mbingu na nchi kuwa ameiweka mbele yetu na kutushauri kuichagua na kuifuata hiyo, ndiyo hiyo inafunuliwa katika kitabu cha Yohana Mtakatifu. Yesu mwenyewe anajidhihirisha kuwa yeye ndiye njia, na siyo njia tu, ina uzima ndani yake amboyo kupitia hiyo tunaurithi Ufalme wa Mungu.

   Kuchagua njia ya uzima kunapaswa kuendane na matendo ya uzima, tusikiri kwa maneno ya vinywa vyetu kuwa tunao uzima (tumempokea Yesu Kristo) na wakati huo huo matendo yetu ni kinyume na kukiri kwetu.

Mathayo 3:8 “Basi zaeni matunda yapasayo toba”, matunda ni matendo na toba ni kuupokea uzima, sasa matendo yetu yanapaswa kuenenda kama jinsi tulivyoupokea huo uzima.
Cha kushangaza, Wakristo wengi wa siku hizi wanatenda kinyume na wanavyokiri katika vinywa vyao. Na kusababisha jina la Mungu litukanwe.

Tito 1:16 “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana”, kukiri kuwa umempokea Yesu Kristo na unahudhuria katika nyumba za ibada lakini matendo yako ni kinyume na kukiri kwako ni sawa na kupoteza muda!

   Kuchagua njia ya uzima na kutoifuata kwa matendo njia hiyo kunamadhara yafuatayo;

Kulitukanisha jina la Yesu; watu wanapoyatazama matendo yetu wanategemea kuona maisha yetu yakiakisi maisha halisi ya Yesu Kristo, na inapokuwa tofauti ndipo jina la Yesu linapotukanwa (2 Petro 2:2).

Kurithi mauti na kuzimu; kutotembea katika njia ya uzima ni kutembea katika njia ya mauti, na kutembea katika njia ya mauti ni kuchagua mauti (Mithali 12:28, 15:24).

Njia utakayopita katika uhai wako ndiyo njia utakayo iendea baada ya kifo, ikiwa umechagua njia ya uzima lakini unapita katika njia ya uovu basi baada ya kifo pia utaiendea njia uliyokuwa ukiipitia. Hapa haijarishi ni dua, swala au maombi mengi kiasi gani utafanyiwa wakati wa mazishi yako.

 Unachochagua kuishi ndicho utakacho tunukiwa.
Mathayo 16:27 “… ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake”, kila mmoja wetu atalipwa kwa kadiri ya alivyotenda alipokuwa hai na siyo kwa kadiri ya sala za kumuombea awekwe pema peponi (Yohana 5:28-29).

Kama umechagua njia ya uzima, tembea katika njia ya uzima maisha yako yote kwa uaminifu.

Sunday, November 25, 2012

FANYA AGANO NA MUNGU KUPITIA SADAKA.

   Kutoa sadaka kama mazoea au desturi ni kupoteza fedha au mali yako pasipo na manufaa yoyote. Wapo wakristo ambao wamelelewa katika familia za dini na kukua wakijua ni lazima kwenda na sadaka ibadani lakini hawajui umuhimu na matunda wanayoweza kuyapata kwa kutoa sadaka. Wakristo wa namna hii ni kama watoto ambao wanapewa sadaka na wazazi wao, wakitoa au wasipotoa sadaka hiyo hawaoni mapungufu yoyote, zaidi ni faida kwao kwani watakula barafu.

   Na wapo wakristo wanaotoa sadaka kama ajali, wao huamua ni sadaka ya aina au kiasi gani watatoa muda mfupi baada ya kujianda kwenda ibadani au hata wakiwa njiani kuelekea ibadani. Wanatoa sadaka za kushtukiza, sadaka isiyo na maandalio yoyote.

   Sadaka inapaswa kuandaliwa, hata siku moja kabla ya kutolewa. Katika agano la kale utaona kuna siku zinapita tangu Mungu aombe kutolewa kwa sadaka na siku ya kuitoa hiyo sadaka, aliyeambiwa atoe sadaka anafanya maandalizi ya kuchagua sadaka nzuri ya kupendeza itakayopata kibali machoni pa Mungu.

   Sadaka utakayoitoa madhabahuni pa Mungu lazima uitamkie jambo. Kabla sijatoa sadaka yangu huwa namwambia Mungu hivi; “maadam, sadaka/dhabihu hii itafanya kazi shambani mwako ee Mungu wangu, fanya jambo (ninalitaja) katika maisha yangu”.
   Sadaka au dhabihu ni sawa na mbegu, ukipanda mbegu unategemea uzune kulingana na mbegu uliyoipanda. Sadaka au dhabihu ni mbegu ya kuvunia baraka zote za kiroho na kimwili, afya na uzima.

   Zaburi 50:5 “Nikusanyieni wacha Mungu wangu, Waliofanya agano nami kwa dhabihu (sadaka).
Agano ni makubaliano yasiyovunjika, kufanya agano na Mungu ni kujithibitishia makubaliano yako na Mungu kuwa yatatimia. Sasa unaweza ukafanya agano na Mungu kwa kutumia dhabihu au sadaka unayoitoa katika ibada zako, sadaka iliyoandaliwa na siyo sadaka ya kutolewa kama bahati mbaya. Agano hilo utalifanya pale utakapo itamkia neno sadaka unayoipeleka madhabahuni pa Mungu wako, ukitoa sadaka ambayo hukuitamkia neno utakuwa unatoa sadaka kama mtoto asiyejua nini maana ya sadaka na inatolewa kwa sababu gani.

Sunday, November 18, 2012

UPENDO.


   Upendo wa kweli ni kumpenda mtu yule anayekuchukia, siyo kwa sababu ya mali au vitu alivyonavyo bali kwa sababu moyo umeamua kumpenda.

Jambo hilo ni gumu sana kwa wengi wetu, kwani tunawapenda wanaotupenda tu na hata kukawa na msemo unaosema “mpende akupendaye, asiyekupenda achana naye”. Tabia hii imeingia hadi makanisani, upendo wa wapendwa wengi wa siku hizi ni kupendana wao kwa wao tu, kusaidiana wao kwa wao tu na hata kutembeleana ni wao kwa wao tu. Huu siyo upendo aliotufundisha Bwana Wetu Yesu Kristo, ni kosa!

Kama wewe ni mkristo au siyo mkristo na unampenda mtu kwa sababu ana kitu au mali inayokunufaisha kwa namna moja au nyingine, bado hauna upendo. Kwa sababu mtu huyo akiondokewa na hicho kinachokufanya umpende, upendo wako kwake utayeyuka wote.

Upendo ni nini?
 Mathayo 5:44 “lakini Mimi (Yesu Kristo) nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi”.

Upendo ni kuwapenda watu wote; rafiki zetu na adui zetu, na kuwaombea pia wapate mema na siyo mabaya.

Wakristo wa siku hizi ili wakuombee basi ni lazima yawe maombi ya kanisa kwa ujumla, au kuwe na jambo zuri umetenda kwa manufaa na faida yao. Ukimpa zawadi ya kitu au pesa, atakuombea Baraka hata kufunga atafunga. Lakini asipopewa kitu, mkristo huyu hana muda wa kukuombea. Huo siyo upendo tulioagizwa na Bwana wetu Yesu Kristo. (Luka 6:27)

Upendo huu ni kuwapenda watu wote kama nafsi zetu; kama vile tunavyojipenda sisi wenyewe ndivyo tuwapende na wenzetu.
Mathayo 19:19 “…mpende jirani yako kama nafsi yako”.
Kama wewe ukilala njaa siyo kwa sababu upo katika maombi ya kufunga, bali kwa sababu umekosa chakula utakavyoumia ndivyo uumie vile vile ukisikia jirani yako amelala njaa pasipo kujali kuwa ni mkristo mwenzako au siyo mkristo, ni rafiki yako au adui yako. Huu ndiyo upendo wa Yesu Kristo, tena ni amri (Marko 12:31).

Nini faida za upendo?
Sadaka pasipo upendo haifai kitu. Ukikosa upendo kwa jirani yako yoyote, sadaka unayoitoa madhabahuni si kitu. Upendo unafaa kuliko sadaka unayoiona ni nono, au inayogusa moyo wako.
Marko 12:33 “…na kumpenda jirani kama nafsi yako, kwafaa kuliko sadaka nzima za kuteketezwa na dhabihu zote pia”.

Kutukamilisha. Kama jinsi Baba yetu wa Mbinguni alivyomkamilifu kwa sababu alimtoa Yesu Kristo afe ili kutukomboa kwa sababu anatupenda, na sisi tukiwapenda wenzetu wote tunakamilishwa kama Mungu mwenyewe alivyo mkamilifu.
Mathayo 5:45,48 “ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”.

Pendo litawavuta wasiomjua Mungu, wamjue Mungu. Tukiwapenda wote; wakristo na wasio wakristo, frafiki zetu na adui zetu, tunamtambulisha Mungu wetu mwenye upendo kwa watu wote kwao. Na kwa njia hii ya upendo huu wa dhati, tunawafanya wasiomjua Mungu nao wamjue Mungu kupitia upendo wetu kwao.

Upendo wa namna hii hauji ila kwa neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, na endapo umekosa upendo huu siyo kosa kwani unaweza kuupata sasa. Yesu mwenyewe alisema, ombeni lolote mtakalo kwa jina langu na Baba wa mbinguni atawapa. Kama umekosa upendo aliotuagiza Yesu, omba na kwa imani Mungu wetu atakupa.
Yohana 14:13 “Nanyi mkiomba lolote (upendo) kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana”.

Mungu aliyetukuka, mtakatifu awabariki wote.


Thursday, November 15, 2012

SIRI YA MAFANIKIO.


   Mpendwa katika Kristo Yesu, nakusalimu kwa Jina la Yesu.
Kabla hatujaangalia neno la Mungu katika kitabu chake kitakatifu Biblia, ningependa tushirikiane jambo ambalo wewe pia utakuwa shahidi wa jambo hili. Katika jamii niliyopo au hiyo uliyopo, kuna watu wanafanya kazi kwa bidii na kujituma mchana na usiku na wengine wanapokea mishahara mikubwa au minono kama inavyojulikana na wengi lakini ukiyatazama maisha ya watu hawa hayafanani na mategemeo ya wengi. Ni maisha ya kawaida sana, ambayo hata ukiyafananisha na maisha ya mtu fulani ambaye anapokea mshahara wa kiwango cha kawaida au kiwango cha chini huwezi kuamini. Unakuta mtu anapokea mshahara mdogo lakini ana mafanikio tofauti na mategemeo ya wengi.
Wewe pia unaweza ukawa miongoni mwa wengi wanaodhani unono au ukubwa wa mshahara ndiyo mafanikio. Hapana, ipo siri katika mafanikio ya mtu yeyote, hata wewe ukiigundua siri hiyo ni lazima ufanikiwe na utashuhudia tu matendo makuu ya Mungu.
Siri ya mafanikio ni kutoa, unapotoa fedha na mali zako ili kuwasaidia wahitaji, Mungu anakubariki. Mungu atakubariki kwa sababu unapo msaidia muhitaji, hata kuripa fedha au mali, yeye atakuombea baraka kwa Mungu, na anaweza akakesha tena kwa machozi akimsihi Mungu akubariki na akuongezee maisha marefu. Hapo ninakuhakikishia kuwa ni lazima Mungu atasikia na kujibu maombi hayo, na lazima baraka za Mungu zikufuate, tena siyo wewe kuzitafuta bali zitakutafuta wewe. Kuna matajiri wengi wanadhani mafanikio waliyonayo ni jitihada zao binafsi, hapana kuna mkono wa Mungu kwa sababu wanawasaidia wenye kuhitaji na hawajui kama wale wenye uhitaji huwaombea baraka pasipo wao kujua.
Matendo ya Mitume 9:36,39 “Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumuonyesha zile kanzu na nguo alizoshona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao”.
Dorkasi alikuwa ni mwanamke aishiye Yafa, ni mwanamke aliyekuwa akitoa sadaka nyingi kwa njia ya kuwahudumia wajane wa mji ule kwa kuwashonea kanzu na nguo. Bila shaka wajane wale walimuombea, na ndiyo sababu alizidi sana katika kuwahudumia, hata alipokufa wajane wale walilia sana na kumsii Petro amfanyie maombi ya kufufuliwa. Sadaka tu, ndiyo ilitosha kutenda muujiza.
Kuna nyakati mtu unapata fedha nzuri na nyingi na inakwisha kabla ya wakati. Kama ni mshahara unakwisha kabla ya kukutana na mshahara unaofuata, na huwezi kuandika au kuonesha chochote cha maana ulichofanya kwa mshahara au fedha  hiyo. Hapo nataka ujue kuwa kuna kinachosaidiana na wewe katika kutumia fedha au mali yako, ni nguvu za yule adui mwovu. Lakini iwapo ungetambua siri, kuwa ukiikabidhi mali au fedha yako kwa Mungu itakuwa salama na utafanya maendeleo yasiyo elezeka zaidi utakuwa ukishuhudia kuwa ni matendo makuu ya Mungu na ni neema zake tu.
Unaweza ukajiuliza, je nitaikabidhi vipi fedha au mali niliyonayo kwa Mungu ili iwe salama? Jibu ni jepesi sana; toa fungu la kumi katika fedha au mali unayoipata.
Malaki 3:10-11 “Leteni zaka (fungu la kumi) kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema Bwana wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la. Nami kwa ajili yenu nitamkemea yeye alaye, wala hataharibu mazao ya ardhi yenu; wala mzabibu wenu hautapukutisha matunda yake kabla ya wakati wake katika mashamba, asema Bwana wa majeshi.”
Katika fungu la kumi huitaji kuomba baraka, bali unatakiwa kudai baraka zako. Hapo Mungu mwenyewe amehaidi kukubariki, ni lazima aitimize ahadi yake kwako.
Nitamkemea yeye alaye; nguvu zozote za adui hazitakuwa na nguvu tena katika kuichezea fedha na mali yako, kwani Mungu atailinda nayo itakuwa salama.
Mzabibu hautapukutisha matunda yake kabla ya wakati wake; matunda ni sawa na mali, fedha au mshahara unaoupata, utadumu hata uje ukutane na mshahara unaofuatia. Kipindi cha mavuno ya kwanza hadi yanayofuata au kipindi cha mshahara mmoja hadi mwengine ni sawa na kipindi cha mzabibu kutoa matunda uzao mmoja hadi uzao unaofuata. Katika kipindi hiki ni lazima matunda ya uzao wa kwanza yadumu hadi uzao unaofuata, hili linawezekana endapo utatoa fungu la kumi kwani Mungu ameahidi kutopukutisha mazao ya mizabibu yetu kabla ya wakati wake.
Ni zamu yako sasa, fanya upande wako na umwachie Mungu upande wake. Hakika utayaona matendo makuu ya miujiza ya Mungu, na ninakuhakikishia kuwa baraka za Mungu zitakutafuta kokote uliko  au uendako. Amina.

Friday, November 9, 2012

MSAMAHA.


   Msamaha ni kufuta au kuachilia mzigo wa makosa unayotendewa na mtu pasipo kuhesabu ni mara ngapi mtu huyo amekukosea.
Isaya 43:25 “Mimi, naam, mimi ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; wala sitazikumbuka dhambi zako”.
Hapo neno la Mungu linatufundisha kuwa; msamaha ni kuyafuta makosa (dhambi) na kutoyakumbuka tena.
Luka 6:37b “…achilieni, nanyi mtaachiliwa”.
Hapa tunaona kuwa maana nyingine ya msamaha ni kuachilia; mtu anaposhindwa kusamehe anabeba mzigo wa hasira ndani ya moyo wake, ambapo mzigo huu unaweza kumfanya mtu huyu akose raha, amani na hata furaha. Hapo Mungu anatuambia tuachilie na kutua mizigo iliyo ndani ya mioyo yetu.
AINA ZA MSAMAHA.
Kuna aina mbili za kusamehe, aina hizi ni;
(a). Msamaha wa kidunia.
Huu ni msamaha wa kusamehe na kutosahau. Msamaha huu hautokani na Mungu, na haukubaliki mbele za Mungu.
Ni msamaha wa kinafiki, mtu anakwambia amekusamehe lakini ndani ya moyo wake ana uchungu nawe. Msamaha huu unahesabu makosa, na wengu wameumia kwa sababu ya kusamehe kwa kutumia msamaha wa aina hii. Unapomwambia mtu nimekusamehe na kumbe bado una uchungu naye, yeye anapata amani na furaha lakini wewe unajawa na uchungu na hasira inayokufanya uumie moyo.
Wengi wetu tumekuwa na msamaha wa aina hii, Mungu atusaidie tuwe na msamaha wa Kimungu kwani msamaha huu una raha na faida. Kuna watu wamekonda na hawana raha siyo kwa sababu ya maisha magumu, bali ni kwa sababu wanavinyongo na mizigo mizito ndani ya mioyo yao.
(b). Msamaha wa Kimungu.
   Huu ni msamaha wa kusamehe na kusahau kabisa. Msamaha huu ni wa Mungu na unatokana na Mungu mwenyewe, kwani Mungu anasema yeye anatusamehe na kusahau kabisa makosa yetu (Isaya 43:25). Nasi kama watoto wa Mungu tunapaswa kuwa na tabia ya Mungu katika kusamehe, tunapaswa tusamehe na kusahau yote tunayokosewa na wenzetu.

Saturday, October 27, 2012

AHADI YA MUNGU HUTUJENGEA IMANI ITUPAYO HAKI.


Ahadi za Mungu.
   Mungu amefanya ahadi nyingi kwa mwanadamu; ahadi za uponyaji, mafanikio, heshima, hekima, ufaulu katika masomo na nyingine nyingi. Na wengi wetu tunazifahamu vizuri ahadi hizo alizotuahidi Mungu; tunazisoma katika neno lake takatifu, Biblia na pia tunazisikia kupitia watumishi mbalimbali wa Mungu.
Zaburi 23:4 “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya, Kwa maana wewe upo pamoja nami”,  na  Zaburi 119:50 “Hii ndiyo faraja yangu katika taabu yangu, Ya kwamba ahadi yako imeniuhisha”.
   Kupita kati ya bonde la uvuli wa mauti (Zaburi 23:4) na kuwa katika taabu (Zaburi 119:50) ni kuingia au kupitia katika hali zenye changamoto mbalimbali za kiafya; magonjwa na udhaifu wa mwili, kielimu; kushindwa kutimiza malengo yako, kiuchumi; hali ngumu ya kiuchumi au kukosa ajila licha ya kuwa na elimu stahiki, kijamii; kukosa watoto kwa miaka mingi katika ndoa na hata jamii inakuita tasa, kufiwa na watoto pale tu wanapozaliwa na changamoto za namna nyingine nyingi. Katika neno la Mungu hapo juu tunafundishwa kwamba kuna nyakati tutaingia katika changamoto, taabu au bonde la uvuli wa mauti katika maisha yetu. Jambo la kujiuliza hapa, je tuingiapo katika changamoto au taabu hizo tunachukua hatua gani? Je, tumekuwa ni watu wa kumlaumu Mungu kwanini ameruhusu tuingie katika taabu? Na kama tumekuwa ni watu wa kulaumu na tunasubiri majibu kutoka kwa Mungu hakika Mungu hata tujibu kamwe, kwa sababu Mungu hana majibu ya lawama. Mungu anayo majibu ya maneno au maombi yenye hoja zilizojengwa katika imani ya neno lake tu.
   Na ndiyo maana kupitia mistari ya neno la Mungu hapo juu anatufundisha kuwa na imani kwa ahadi zake kwetu.  Anaposema “sitaogopa mabaya, kwa maana wewe upo pamoja nami”, Mungu kuwa pamoja naye ni kwamba ahadi ya Mungu ya ukombozi imemfunika na ni lazima atatoka katika bonde hilo la uvuli wa mauti, na “ahadi yako imeniuhisha” anamaanisha hawezi kukata tama pasipo kujali anapitia taabu ya namna gani kwa sababu ukombozi wake unakuja tena uko karibu.
   Na sisi tunapopitia katika mahangaiko, taabu, shida na misukosuko ya maisha tusiwe ni watu wa kulaumu na kulalamika mbele za Mungu, bali tuwe ni watu wenye kusimama katika maombi yenye imani ya ukombozi tukiziangalia ahadi za Mungu katika taabu zetu.

Thursday, September 27, 2012

NGUVU YA MANENO.


  Katika maneno tunayoyazungumza kuna nguvu ya uumbaji wa kile tunachokizungumza. Kwa mfano mtumishi wa Mungu anapofanya maombezi kwa ajili ya mtu fulani, anatamka maneno ya uponyaji kwa imani, na yule anayeombewa akiyasikia yale maneno ya uponyaji anaamini katika maneno yale na ndipo anapokea uponyaji. Hii inatokea kwa sababu maneno tunayoyasikia yanatufanya tujenge picha ya kile tunachokisikia. Ukisikia maneno ya uponyaji unapata picha ya kupona, ukisikia maneno ya kukutia moyo unapata picha ya kutiwa moyo na ukisikia maneno ya kukukatisha tamaa utapata picha ya kukata tamaa na kushindwa. Na jambo hilo linasababishwa na jinsi tunavyojenga imani katika maneno tunayoyasikia ama kujisemea wenyewe.
Yakobo 1:19 “Basi kila mtu  na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema;”.
Mstari huo wa kitabu kitakatifu cha Biblia, unatufundisha kutokuwa wepesi wa kusema. Kwa sababu katika kusema sana tutasema maneno yenye kuvunja moyo, kukatisha tamaa, kulaani na hata maneno yasiyo na maana ili mradi tuonekane tumesema. Tunatakiwa tuseme au tuongee maneno ya kubariki, kutia moyo na kufariji; maneno ambayo mtu anayekusikia atatamani akusikie tena na kesho na siku inayofuata kwa sababu una kitu cha maana katika maisha yake.
   Baraka, kwa kutumia maneno ya vinywa vyetu tunaweza kubariki. Tukitaka kumbariki mtu au kumfariji tunatumia maneno. Tunatamka maneno yenye baraka au kufariji. Mwanzo 27:27-28 “…akambariki AKASEMA (maneno), Mungu na akupe  ya umande wa mbingu, na ya manono ya nchi, na wingi wa nafaka na mvinyo.”
   Laana, pia kwa kututmia maneno ya vinywa vyetu tunaweza tukatamka maneno ya kulaani. Ambapo tunaweza kujilaani wenyewe au wenzetu kwa kujua ama kutokujua. Tunapoongea jambo baya kwa maisha yetu au ya wenzetu tunakuwa tunatamka laana ambazo ni lazima zitatimia. Zaburi 10:7 “kinywa chake kimejaa laana, na hila na dhuluma, chini ya ulimi wake kuna madhara na uovu.”
   Ikiwa unatamka laana au baraka, ushindi au kushindwa katika maisha yako au ya mtu mwingine, ni lazima jambo hilo litakuja kutimia. Unaweza ukamwambia mtu fulani kuwa unataka uanze kufanya biashara, na mtu huyo akakwambia, “na wewe unataka kufanya biashara, ameshinwda fulani utaweza wewe?” badala ya kumjibu NITAWEZA, unamjibu ‘najaribu jaribu tu ndugu yangu’. Unaanza biashara alafu miaka inakatika huoni faida yoyote, ni kwa sababu uliyemshirikisha jambo lako aliongea kushindwa na wewe pia ukakiri kushindwa huko. Kwa maana hiyo unaweza ukawa umetamkiwa/umejitamkia laana au baraka katika maisha yako bila wewe kujua. Na falme zote mbili; ufalme wa giza na Ufalme wa Mungu zinafuatilia unayoyakili kwa ajili ya maisha yako au ya wenzako ili kuyatenda au kuhakikisha yanatendeka.
Isaya 59:17(a) “Mimi nayaumba matunda ya midomo;”. Hapa Mungu alimwambia nabii Isaya kuwa yeye (Mungu), anayaumba matunda ya midomo yetu, kwa maana nyingine ni kwamba Mungu anayaumba maneno tunayotamka kwa ajili ya maisha yetu au wenzetu.
Na kwa upande wa ufalme wa giza pia yapo mapepo yanayofuatilia na kutimiza maneno ya vinywa vyetu, hasa maneno ya laana ili kuhakikisha tunaishi maisha yenye mateso na dhiki.
Kwa hiyo ndugu mpendwa katika Kristo Yesu, unatakiwa kufanya maombi ya kufunga ili uvunje laana zote katika maisha yako, laana ulizojitamkia kwa kujua au kutokujua na zile walizokutamkia wengine. Na Mungu yupo atakujibu na kukubariki, muamini tu.

Featured Post

HAIJALISHI TUNAKOSEA MARA NGAPI? MUNGU NI MUAMINIFU KILA WAKATI

Nakusalimu kupitia Jina kuu lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wetu. Mungu wetu ni muaminifu, hajawahi kuse...

Popular Posts